Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Fedha na Mipango

Hon. Zainab Athuman Katimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Fedha na Mipango

MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia kwenye hoja iliyopo mbele yetu. Awali ya yote nianze kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa anayofanya katika kuhangaika kuwaletea maendeleo wananchi wake. Tuendelee kumuombe afya, umri na uwezo zaidi wa kufanya kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, natoa pongezi kubwa sana kwa Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Naibu Waziri, Katibu Mkuu, Manaibu Katibu Mkuu na timu yake nzima ya Wizarani kwa kazi kubwa anayofanya katika kumsaidia Mheshimiwa Rais kutimiza malengo.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo nataka kuanza kuzungumzia suala muhimu sana ambalo lipo kwenye Sheria ya Manuuzi (Public Procurement Act). Sheria hii ya Manunuzi inataka kwamba Maafisa Masuuli wote watenge asilimia 30 ya Manunuzi ya Taasisi zao wanazozisimamia ziende kwenye makundi ya vijana, wanawake na watu wenye ulemavu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Sheria haijaishia hapo. Sheria chini ya Kanuni zake, kwenye Kanuni ya 30(c)(2), inasema kwamba, Maafisa Masuuli watakaoshindwa kutekeleza Sheria ya kutenga asilimia 30 watoe maelezo kwa nini wameshindwa kutekeleza? Haiishii hapo, inasema kwamba Maafisa Masuuli ambao hawatasimamia sheria hii watapewa adhabu, yaani watawajibishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Mheshimiwa Waziri atueleze leo hii kwamba utekelezaji wa Sheria hii uko vipi? Maafisa Masuuli wangapi wametoa maelezo na wangapi wamewajibishwa? Tupate ripoti ya utekelezaji wa sheria hii. Kwa sababu sheria zimetungwa na Bunge, inabidi zisimamiwe. Kanuni imeenda kukazia na kuweka msisitizo. Hii ni sehemu ambayo Mheshimiwa Rais anataka kuwasaidia wananchi wake, anatengeneza mazingira ya kuwawezesha, kila siku anazungumza. Sasa fursa kama hizi ambazo zimewekwa vizuri kwenye sheria, kwa nini hatusimamii utekelezaji wa sheria zetu ili tuweze kuwanufaisha wananchi wetu?

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili, nataka kuzungumzia maelekezo ya Mheshimiwa Rais wetu mpendwa Mama Samia Suluhu Hassan. Tumemsikia katika majukwaa tofauti tofauti, katika mikutano tofauti tofauti akisisitiza na akiweka mkazo kabisa anataka wananchi waweze kutengenezewa mazingira mazuri ya kufanya biashara ili waweze kujitengenezea kipato. Imefika hatua tulimsikia Mheshimiwa Waziri wa Viwanda na Biashara amesema kwamba Mheshimiwa Rais ametoa ruhusa ya msamaha wa kodi kwa biashara mpya zilizo kuanzia miezi sita mpaka mwaka. Tunataka kufahamu utekelezaji kwenye suala hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, msingi wa kulipa kodi ya mapato ni kufanya biashara na kupata faida. Ile faida ndiyo inatozwa kodi ya mapato. Sasa mtu anayeanza biashara, kabla tu hajaanza biashara, anapopewa makadirio ya kodi, anaambiwa aanze kulipa kwanza robo ya kwanza ya yale makadirio, kabla hata hajafanya biashara, atumie mtaji wake kulipa kodi, msingi wa hiyo kodi unatokana na nini? Kwa sababu sheria inataka kodi ya mapato itokane na faida. Ndivyo sheria inavyosomeka leo hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais anatengeneza mazingira mazuri sana ya kuwawezesha wananchi wake, mbona hatuoni sheria zikiletwa zifanyiwe marekebisho?

MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Taarifa.

TAARIFA

MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, nami naomba nimpe taarifa mchangiaji, Mheshimiwa Zainab Katimba, kwamba siyo tu huyo mfanyabiashara anatakiwa akadiriwe hiyo kodi wakati anaanza, lakini pia atatakiwa kufanyiwa mahesabu na wahasibu, nao anatakiwa awalipe kabla hajaanza hata hiyo biashara.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Katimba.

MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nashukuru kwa taarifa yake, naipokea.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, msingi wa hayo maboresho yote ni kwamba tunataka tutengeneze mazingira rafiki na mepesi ya kufanya biashara ili watu wengi waweze kuingia katika mfumo rasmi, warasimishe biashara zao, tuongeze wigo wa walipa kodi, na tuongeze mapato ya Serikali. Kwa hiyo, naomba nisikie kutoka kwa upande wa Waziri kwenye eneo hili, wamejipanga vipi? Kwa sababu hapo tayari ni tatizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ambalo nataka kuchangia ni kuhusiana na Mfumo wa Usimamizi wa Mali za Serikali (Government Asset Management Information System - GoMIS). Kwanza Sheria ya Manunuzi (Public Procurement Act) na Public Finance Act inaeleza bayana kabisa kwamba Mlipaji Mkuu wa Serikali ndiye ambaye amepewa dhamana ya usimamizi wa mali zote za Serikali. Utaratibu mzuri wa usimamizi wa mali za Serikali umewekwa kwenye sheria hizi nilizotaja na pia kwenye mwongozo ule wa Public Asset Management Guideline ya 2019.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwongozo uko vizuri, lakini kwenye eneo moja la kuuza mali chakavu zile za Serikali, mfumo wa kitehama upo, lakini mfumo ule bado haujaweza kusomana na mifumo mingine muhimu. Kwa mfano mfumo wa malipo ya GePG lakini bado mfumo ule kuna Maafisa Masuuli ambao hawajapewa access, hawawezi kuutumia. Kwa hiyo, inapofika wakati wa mali chakavu za Serikali, inabidi ziuzwe, kuna hatua moja ambayo Pay Master General inabidi amwelekeze mhakiki aende akafanye verification ya zile mali kwamba ni chakavu ili utaratibu wa kuziuza zile mali/wa kuzi-dispose uendelee.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye process hiyo ndiyo tayari kuna mkwamo, kwa sababu mfumo huu wa Tehama hauna teknolijia ya kuweza kufanya verification kwa kutumia Tehama. Tumeona hapa, sisi tumeanza hapa Bungeni tukiwa tuko kwenye Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania hapo nje, tumeweza kuona Bwawa la Mwalimu Nyerere live, utafikiri tuko huko site. Kwa nini? Kwa sababu tumetumia Tehama, ile teknolojia ya virtual reality.

Mheshimiwa Naibu Spika, Tehama imefikia katika hatua ambayo kuna vitu vingi vinaweza kufanyika bila kuhitaji mtu kufika yeye mwenyewe site. Kwa hiyo, naomba waboreshe mfumo huu kwanza uweze kusomana na mifumo muhimu na hasa mfumo huu wa GePG, pia waweze kutumia teknolojia hii kama za Tehama ili kuweza kurahisisha utaratibu wa verification wa uhakiki wa zile mali ili kuondoa mlundikano wa mali za Serikali Tanzania nzima ambazo zinasubiri kuuzwa.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante kwa mchango mzuri.

MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Baada ya mchango huo, naomba kuunga mkono hoja.