Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Fedha na Mipango

Hon. Zaytun Seif Swai

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Fedha na Mipango

MHE. ZAYTUN S. SWAI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa ili niweze kuchangia bajeti hii ya Wizara muhimu, bajeti ya Wizara ya Fedha na Mipango ya Mwaka 2023/2024.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia nimpongeze sana na nimshukuru Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan kwa kuweza kuendeleza miradi mbalimbali ya kimkakati na nimshukuru pia katika Mkoa wa Arusha tumeona miradi mbalimbali ya maendeleo ikitekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niwapongeze Wizara ya Fedha wakiongozwa na Waziri wetu, Naibu wake pamoja na Watendaji wote wa Wizara hii wamekuwa wakiipa Kamati ya Bajeti ushirikiano mkubwa katika kutekeleza majukumu yetu ya kila siku. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niongelee suala moja la mifumo yetu ya ukusanyaji wa mapato pamoja na usimamizi wa mapato yetu hususan mapato ya ndani. Natambua jitihada kubwa sana zinazofanywa na Mamlaka yetu ya Serikali Mtandao yaani e-GA katika kuratibu na kusimamia mifumo ya TEHAMA Serikalini, lakini bado changamoto ni nyingi na wana kazi kubwa ya kufanya katika kuhakikisha basi mifumo yetu ya matumizi mbalimbali ya Serikali inatumiwa kwa usahihi ili kuondokana na hizi changamoto nyingi ili basi tuweze kudhibiti makusanyo yetu tunayopata.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto za mifumo hii bado ni nyingi, utakuta makusanyo mengi yanafanyika nje ya mifumo. Mifumo yetu bado haisomani kama walivyosema wenzangu, lakini vile vile hata mapato yale inayokusanya yanacheleweshwa kupelekwa benki, lakini vile vile mengine hayaendi benki kabisa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kamati ya bajeti imeweza kukutana na Wizara mbalimbali pamoja na taasisi mbalimbali za Serikali na moja ya changamoto walizonazo ni makusanyo hafifu ya mapato ya taasisi hizo. Hii imetokana na ukosefu wa mifumo imara ya kuhakikisha makusanyo yetu yanadhibiwa kikamilifu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto hii imetokana kwa kiasi kubwa na bajeti finyu inayotengwa kwa ajili ya kuhakikisha tunakuwa na mifumo imara ya kudhibiti na kusimamia mapato yetu ya Serikali. Ukiangalia hadi Aprili 2023 ni taasisi 968 tu zimeunganishwa na mfumo wa GePG, bado taasisi nyingi sana hazijaunganishwa na mfumo huu wa GePG.

Mheshimiwa Naibu Spika, Taasisi ya Mfumo wa Usimamizi wa Mali za Serikali (GAMIS) bado haisomani na mifumo mingine, lakini bado mifumo ya forodha haisomani na mifumo ya bandari na hii inaleta changamoto kubwa sana ya Serikali yetu kupoteza mapato kwa kiasi kikubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama Kamati ilivyoshauri basi ni lazima Serikali ije na mipango mikakati na mipango mahsusi ya kuweza kuwa na mifumo imara, mifumo inayosomana ili tuweze kudhibiti mapato yetu tunayopata. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia tu kwenye uwiano wa kodi kwa pato la Taifa yaani Tax to GDP Ratio utaona kabisa Tanzania bado tuko chini sana ya wastani ukilinganisha na kanda zingine ambazo tumejiunga nazo kama Kanda ya Afrika Mashariki na Kanda ya SADC. Hadi Aprili, 2023 Tanzania tuna wastani wa asilimia 11.7 tu. Ukiangalia wastani wa Afrika Mashariki ina wastani wa asilimia 13, SADC asilimia 24 na hii inatupa tafsiri gani? Inatuonesha kwamba ukusanyaji wa mapato bado uko chini ukilinganisha na ukuaji wa pato la Taifa. Kwa hiyo ukusanyaji wa mapato ya ndani bado hautoshelezi Serikali kukidhi mahitaji yake ambayo yanaongezeka kila siku.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hayo niliyosema, naungana na maoni ya Kamati kwamba Wizara hii iweze kufanya kazi na iweze kuja na mpango mahsusi katika kuhakikisha kwamba tunakuwa na ukusanyaji wa mapato imara, lakini tunadhibiti mapato ambayo tunayapata.

Mheshimiwa Naibu Spika, namuomba sana Waziri wakati anahitimisha hapa tusichukulie suala la mifumo ni kawaida, naomba sana tuondoke kwenye masuala ya kawaida tuje kwenye mpango mkakati basi ili Wizara zote ziweze kuwa na mifumo imara tuweze kuongeza mapato yetu. Tukiweza kuongeza mapato yetu kupitia mifumo hii, tutaweza pia kuwezesha bajeti yetu kwenye mapato ya ndani kwa kiasi kikubwa kuliko sasa hivi tunavyotegemea kuwezesha bajeti yetu kwa mapato ya nje.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)