Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Fedha na Mipango

Hon. Daniel Baran Sillo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Fedha na Mipango

MHE. DANIEL B. SILLO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili nichangie katika Wizara yetu hii ya Fedha na Mipango. Awali ya yote, nichukue nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu, lakini pia nimpongeze Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa anayoifanya katika Taifa letu. Tunamwombea afya njema ili aendelee kututumikia. Pia niwapongeze Waziri wa Fedha na Mipango, Naibu Waziri pamoja na Timu nzima ya Wizara hii kwa kazi kubwa wanayofanya kusimamia fedha na sera za fedha za kikodi katika Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nimpongeze Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti pamoja na Wajumbe kwa kazi kubwa tuliyofanya katika kukamilisha taarifa hii ya Kamati.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitachangia mambo machache. La kwanza ni mfumo wa TEHAMA wa ukusanyaji wa mapato ya TRA pamoja na TPA. Sisi wote ni mashahidi kwamba mifumo ya ukusanyaji mapato ni ya muhimu sana katika kukusanya mapato ya Taifa letu. Mifumo yetu hii ina changamoto zifuatazo:-

(i) Mfumo wa kodi za ndani bado haujakamilika, unasuasua;

(ii) Mfumo wa kodi za ndani kutokusomana na mfumo wa kodi za forodha; na

(iii) Mfumo wa forodha kutosomana na mfumo wa TOS wa TPA. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokamilika kwa mfumo wa kodi za ndani ni risk kubwa sana katika kupotea kwa mapato ya Taifa letu. Kwa hiyo niombe sana Wizara ya Fedha kuhakikisha inasimamia kukamilisha mfumo wa kodi za ndani ili kuweza kuimarisha mapato yetu ya ndani ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wote ni mashahidi kwamba asilimia 40 ya mapato yote ya TRA yanakusanywa kwenye Idara ya Forodha, lakini kutokusomana kwa mfumo wa kodi ya forodha na Bandari ni changamoto kubwa sana ya upotevu wa fedha hapa nchini. Kwa hiyo nishauri sana Serikali, Wizara ya Fedha na Mipango wahakikishe mifumo yetu ya mapato inasomana ili kuboresha mapato ya Serikali yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Mpango wa Maendeleo wa Tatu wa Miaka Mitano wa Mwaka 2021/2022-2025/2026 yako mambo ambayo yameainishwa. Kwanza, mchango wa kodi kwenye pato la Taifa kufikia asilimia 13, lakini bajeti yetu ya Serikali karibu asilimia 60 inategemea mapato ya kodi zetu hapa nchini, lakini Ilani yetu ya Uchaguzi ya CCM mwaka 2025 ukisoma ukurasa wa 16 imezungumzia kuboresha mapato ya Taifa letu. Ili kufikia malengo haya ni lazima kuwekeza katika mifumo ya ukusanyaji mapato hapa nchini ili nchi yetu iweze kufikia hatua hii ya asilimia 13 ya pato la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, takwimu kwenye nchi zinazotuzunguka, mchango wa kodi kwa Nchi ya Kenya kwa pato la Taifa ni asilimia 16.9, mchango wa kodi pato la Taifa kwa Nchi ya Rwanda ni asilimia 14.1, lakini sisi Tanzania asilimia 11. Kwa hiyo kama nchi tuna kazi ya kufanya kuhakikisha kwamba tunaimarisha mifumo yetu ili tufikie malengo haya kwa manufaa makubwa ya Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili, ni mikataba ya kutokutoza kodi mara mbili, yaani double taxation agreement na nchi yetu na nchi mbalimbali. Mwaka jana nilichangia jambo hili pia na narudia tena. Nchi yetu iliingia mikataba ya kutotoza kodi mara mbili na nchi mbalimbali kwa lengo la kuondoa vikwazo vya kibiashara lakini na kuongeza biashara baina ya nchi hizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mikataba ilikuwa ni kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Nchi yetu na Canada kwenye income and capital tax treatment ya mwaka 1995, Finland na Tanzania Income tax and Capital tax ya mwaka 1976, Denmark na Tanzania Income and Capital Tax ya mwaka 1976, India na Tanzania Income Tax Treaty ya Mwaka 1979, Italy na Tanzania Income Tax Treaty ya mwaka 1973, Norway na Tanzania Income and Capital Tax Treaty ya mwaka 1976, South Africa na Tanzania Income Tax Treaty ya mwaka 2005 na Sweden na Tanzania Income and Capital Tax Treaty ya mwaka 1976 na Zambia na Tanzania Income Tax Treaty ya mwaka 1968.

Mheshimiwa Naibu Spika, mikataba hii tunajua ni muhimu lakini ya muda mrefu sana. Aina ya biashara leo zimebadilika, mazingira ya biashara yamebadilika, teknolojia imekua na tuko kwenye digital economy. Kwa hiyo kutokana na mazingira niliyotaja hapo juu ni muhimu sana mikataba yetu hii ya kikodi ikarejewa ili kuona nchi zetu zote zinapata manufaa ya mapato yanayostahili ya kikodi katika nchi zetu hizo. Kwa hiyo naomba jambo hili, Wizara ya Fedha walichukue kwa umakini mkubwa. Mikataba hii ni ya muda mrefu, mikataba ya miaka 50. Tuna kila sababu ya ku-review kuangalia ni namna gani nchi yetu inanufaika kupata kodi stahili katika mikataba hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo nimpongeze sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wetu. Ndani ya uongozi wa miaka miwili imesaidia mikataba hii ya kikodi ya tozo mara mbili ya Nchi za Falme za Kiarabu pamoja na Oman, kwa hiyo hatua hii ni muhimu, itaongeza uwekezaji hapa nchini lakini itapanua wigo wa kodi na kwa kukuza uchumi wa Taifa letu. Kwa hiyo tunaipongeza Serikali kwa hatua hii nzuri na Wizara ya Fedha waendelee kusimamia jambo hili kubwa la kukuza uchumi wa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la tatu ni kuboresha Kitengo cha Ukaguzi wa Kodi (Tax Audit). Tax Audit ni kitengo ambacho kinasaidia sana:-.

(i) Kuimarisha ulipaji wa kodi ya hiari (voluntary tax compliance);

(ii) Kuongeza mapato ya Taifa letu; na

(iii) Inatoa elimu kwa walipakodi wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo hili lazima liende sambamba na hawa wakaguzi wenyewe, lazima wapate exposure kwa maana ya kupata mafunzo ndani na nje ya nchi ili kuwajengea uwezo. Leo hii tuko kwenye teknolojia ya hali ya juu. Elimu imebadilika biashara zinafanywa kidigitali, kwa hiyo ni lazima na wataalam wetu tuwafundishe, wapate ujuzi wa kutosha. Ziko nchi zilizoendelea zaidi katika eneo hili la ukaguzi. Waende kule wakajifunze kwa ajili ya manufaa makubwa ya Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema haya, naunga mkono hoja na nashukuru sana ka kupata nafasi. (Makofi)