Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Francis Kumba Ndulane

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Spika, napenda kuchangia hotuba ya bajeti ya Wizara ya Maliasili na Utalii iliyotolewa siku ya Ijumaa tarehe 2 Juni, 2023 kwa kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi nzuri anayoifanya ya kuitangaza nchi yetu ya Tanzania kupitia filamu ya Royal Tour hali iliyopelekea watalii wengi kuja Tanzania kutembelea vivutio via utalii.

Pia napenda kumpongeza Mheshimiwa Mohamed Omari Mchengerwa, Waziri wa Wizara hii ya Maliasili na Utalii pamoja na timu nzima ya Wizara yake kwa usimamizi wa Wizara hii. Pamoja na mambo mengi mazuri yanayotekelezwa na Wizara hii naomba kuishauri Serikali katika maeneo yafuatayo; kwanza malikale na maadhimisho; napenda kuishauri Serikali iweze kuyapa GN Maadhimisho ya Majimaji ya Nandete Kilwa mkoani Lindi ili yaweze kuingia katika urithi wa Taifa. Pia itenge bajeti kila mwaka kuanzia mwaka 2023/2024 na kupangiwa taasisi simamizi smbamba na kujenga miundombinu muhimu ya kutunzia kumbukizi muhimu zilizotumika wakati wa vita hivi vilivyopiganwa chini ya wakoloni wa Kijerumani kuanzia mwaka 1905 hadi 1907.

Mheshimiwa Spika, maboresho katika kumbukizi hii yataboresha na kuongeza mapato ya Serikali na kuinua uchumi hapa nchini kwa kuwa kumbukizi hizi zipo karibu na vivutio vingi vya utalii kama vile pango kubwa kuliko yote Afrika Mashariki la Nang’oma lililopo Kijiji cha Nandembo. Boma la wakoloni wa Kijerumani la Kibata, ziwa lenye viboko wengi la Maliwe lililopo katika Kijiji cha Ngea, magofu ya kale ya Kilwa Kisiwani, Songomnara na Kivinje, viboko albino waliopo katika Mto Nyange, Jiwe la Jahazi Kilwa Kisiwani na Pori la Akiba la Selous.

Mheshimiwa Spika, pili ni kuhusu urejeshaji wa malikale zilizochukuliwa na wakoloni, naishauri Serikali ifanye jitihada za dhati ili kuhakikisha malikale mbalimbali zilizochukuliwa na wakoloni ziweze kurejeshwa kama vile kurejeshwa kwa mjusi mkubwa (dinosaur) ambaye alichukuliwa katika Kijiji cha Tendeguru Wilayani Lindi mkoani Lindi na urejeshaji wa mafuvu ya machifu na kadhalika.

Kuhusu malipo ya fidia zinazotokana na athari za vita vya Majimaji, naishauri Serikali isimamie na kuweka mkakati wa kulipwa fidia za vita ya Majimaji kwa kuwashirikisha wananchi wa jamii zilizohusika na vita hivyo. Naishauri Serikali ianzishe mchakato wa kudai fedha hizo ili zikipatikana ziweze kutumika kwa kujenga miundombinu ya kijamii kama hospitali, shule na barabara.

Mheshimiwa Spika, uwepo mpango (succession plan) kwa watumishi wa Idara ya Makumbusho kwa kuanzia na makumbusho mbili za Dkt. Livingstone za Tabora Kwihala, Tabora na Kigoma Ujiji; Tabora Kwihala kuna Mzee wa miaka 73 anaendelea kuhudumu na Kigoma Ujiji kuna Mzee wa miaka 69 anahudumu pale.