Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Ally Mohamed Kassinge

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujaalia neema ya uhai na uzima. Nitumie fursa hii kumpongezaza Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kujitoa yeye mwenyewe kwa kucheza filamu ya Royal Tour ambayo imeinua sekta ya utalii hapa nchini. Nipongeze pia uongozi wa Wizara kwa kazi za kutumikia Watanzania kwa moyo na bidii kubwa.

Mheshimiwa Spika, nianze kuchangia bajeti ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kuwakumbusha kuwa Wizara hii imepewa jukumu kubwa la uhifadhi wa maliasili zetu. Uhifadhi huu ni kwa aijili ya matumizi na manufaa kwa Watanzania. Tungependa kuona kuwa uhifadhi huu unawasaidia Watanzania na usiwe kero kwa wananchi.

Mheshimiwa Spika, pale Kilwa Kisiwani kumetangazwa kuwa ni sehemu ya urithi wa dunia na Mamlaka ya Uhifadhi wa Wanyamapori (TAWA) imepewa jukumu la usimamizi wa eneo hili la utalii ambapo Serikali imeboresha miundombinu ili iwe rafiki kwa aijili ya watalii wanaokuja Kilwa kujionea historia ya Kilwa Kisiwani mji ambao ulikuwa wa kwanza katika Pwani ya Afrika Mashariki kujitengenezea fedha zake yenyewe. Tunachokumbusha hapa ni kwamba Serikali itimize wajibu wake wa kutoa CSR kwa Wana-Kilwa Kisiwani kwa kuwajengea miundombinu ya shule ya msingi na zahanati kama ambavyo tumetarajia.

Mheshimiwa Spika, Kilwa Kivinje ni miongoni mwa maeneo yenye historia kubwa hapa nchini; Kilwa Kivinje ndipo palipokuwa na soko la watumwa; Kilwa Kivinje ndipo palipokuwa ni njia ya kusafirisha watumwa; na Kilwa Kivinje ndipo palipokuwa makazi ya Waarabu na baadae Makao ya Wajerumani. Serikali ichukue hatua ya kukarabati soko lile lililokuwa la watumwa ili liendelee kubaki katika uhalisia wake kulinda historia. Pia Serikali ikarabati na kuhifadhi magofu ya Kilwa Kivinje ili kulinda historia na kuifanya Kilwa Kivinje kuwa ni sehemu ya utalii katika nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, mwisho, katika Kijiji cha Mchakama, Mavuji, kuna msitu wa hifadhi unaosimamiwa na TFS kwa upande wa Kusini Mashariki mwa kijiji. Kwa upande wa Kusini-Magharibi, kijiji kimepitiwa na Mto Mavuji ambao ni chanzo cha maji na tunachoendelea kukihifadhi kwa kuzingatia sheria ya kutoingilia eneo la mita 60 kutoka ukingo wa mto. Kwa muktadha huo, kijiji kimebakiwa na eneo dogo la makazi na taasisi za pale kijijini. Wananchi wanakosa eneo la kufanya shughuli za kiuchumi. Wananchi wangu kutoka Mchakama walituma uwakilishi wao mwaka jana kuja Dodoma kukutana na Waziri wa Maliasili na Utalii kwa lengo la kuomba wapatiwe sehemu ya hifadhi ya msitu kwa ajili wa shughuli za kiuchumi. Niliongozana na uwakilishi huo hadi ofisini kwa Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii Mheshimiwa Mary Masanja na kukabidhi barua ya maombi yetu yakiambatana na muhtasari wa kijiji.

Mheshimiwa Spika, hadi sasa bado Wana-Mchakama hawajajibiwa ombi lao na hatujaona hatua ya Wizara ya kugawa eneo la hifadhi ili wanakijiji wapate kufanya shughuli za kiuchumi ikiwemo kilimo bila kukiuka sheria. Tunakumbusha hapa, maombi yetu yafanyiwe kazi ili wananchi wale wapate eneo kufanyia shughuli za kiuchumi.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja ya Wizara hii.