Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Spika, nachukua nafasi hii kuungana na Watanzania wenzangu wote kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kutujalia baraka zake katika nyanja mbalimbali za ustawi wa kijamii, kiuchumi, kiplomasia, kisiasa na mshikamano wa Taifa letu wakati wote.

Mheshimiwa Spika, nachukua nafasi hii kuungana na wananchi wa jimbo langu la Mbulu Mjini kumpongeza sana Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, na Serikali nzima ya Awamu ya Sita kwa jinsi wanavyoliongoza Taifa letu na kutatua changamoto nyingi sana zinazowakabili wananchi hususan utekelezaji wa Ilani ya CCM 2020-2025 kwa kila sekta, Mwenyezi awabariki sana.

Mheshimiwa Spika, nachukua nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Mohamed Mchegerwa, Waziri wa Wizara hii, Naibu Waziri Mheshimiwa Mary Masanja na watendaji wakuu wote wa taasisi zilizo chini ya Wizara hii kwa jinsi wanavyotumikia nafasi zao.

Mheshimiwa Spika, nampongeza sana Mheshimiwa Dkt. Tulia Ackson - Spika wetu, Mheshimiwa Mwenyekiti wa Kamati yetu ya Kudumu ya Bunge, Wajumbe wa Kamati hii, Katibu wa Bunge na watendaji wote wa Bunge kutokana na mipango yao mizuri ya kufanikisha maandalizi ya taarifa hii.

Mheshimiwa Spika, naomba nitoe mchango wangu kwa kupitia hotuba ya mapendekezo ya bajeti ya Wizara hii muhimu sana ya Maliasili na maoni ya Kamati yetu ya Kudumu ya Bunge letu.

Mheshimiwa Spika, Serikali iangalie uwezekano wa kuchimba mabwawa ya maji katika hifadhi zetu au kujenga mabwawa kwenye mito ndani ya hifadhi zetu, kwa sababu dunia inakabiliwa na mabadiliko ya tibianchi na ukame mkubwa hivyo basi tatizo la ukosefu wa upatikanaji wa maji katika hifadhi zetu siyo suala litakalopungua kwa haraka bali litazidi kuongezeka sana.

Mheshimiwa Spika, Serikali iajiri Maafisa Wanyamapori katika Halmashauri zote nchini ambazo zinapakana na Hifadhi za Taifa. Kwa kuwa kumeongezeka tatizo la wanyama wakali na waharibifu kutoka ndani ya hifadhi zetu na kwenda kwenye maeneo ya makazi ya watu na kupoteza maisha na kuharibu mali za wananchi, hali hii imekuwepo katika Halmashauri ya Mbulu Mji, ninaomba tupatiwe mtumishi huyu muhimu.

Mheshimiwa Spika, kutokana na kutowepo kwa mahusiano mazuri kati ya wananchi na askari wa hifadhi zetu hali inayosababisha athari nyingi ikiwemo vifo na kupoteza mali, naiomba Serikali iangalie uwezekano wa kuwepo kwa ratiba ya vikao vya ujirani mwema kila robo mwaka kwenye maeneo yanayopakana na hifadhi zetu nchini kwa kuunganishwa na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya na sisi Wabunge tushiriki kwa maslahi mapana ya Taifa letu kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika, Serikali iangalie upya uhalisia wa sheria za fidia na kifuta machozi kwa wananchi wanaoathiriwa na wanyama wakali na waharibifu wa mazao yaliyoko mashambani na kwenye maghala yao hali ambayo imesababisha umaskini mkubwa kwa jamii.

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Wizara hii iangalie uwezekano wa kuwepo kwa kitengo cha kuratibu, kubaini na kutangaza vivutio kwenye tovuti za halmashauri ili kukuza na kuchochea utalii wa ndani na nje ya nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, pia Wizara iangalie utaratibu mzuri wa kutoa michango ya miradi ya maendeleo kwa jamii katika huduma za sekta kwenye maeneo hayo ya hifadhi ambayo yanapakana na wananchi wetu ili kuongeza mahusiano na hamasa ya kuthamini uendelevu wa hifadhi za taifa letu.

Mheshimiwa Spika, naomba kukumbushia umuhimu mkubwa sana wa ziara ya Mheshimiwa Waziri au Naibu Waziri katika jimbo langu la Mbulu Mjini kwenye Kata za Gehandu, Bargish, Daudi na Marangw ambazo zinapakana na hifadhi ya Ziwa Manyara na Hifadhi ya Msitu wa Marang kwa ajili ya kufanya mikutano ya hadhara ya ujirani mwema na ufafanuzi wa sheria za hifadhi na kuhamasisha jamii kuwa sehemu ya walinzi na wahifadhi wa rasilimali hiyo muhimu.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja na naomba kuwasilisha.