Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, napenda kuwashukuru na kuwapongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Dkt. Philip Isdor Mpango, Makamu wa Rais wa wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mawaziri na viongozi wote wa Wizara ya Maliasili na Utalii, kwa uongozi wao na utendaji uliotukuka.

Mheshimiwa Spika, napenda pia kutumia fursa hii kukupongeza wewe binafsi, Naibu Spika na uongozi wote wa Bunge kwa uongozi wenu mahiri na wenye ubunifu wa hali ya juu katika kuongoza mhimili wa Bunge.

Mheshimiwa Spika, napenda kumpongeza Waziri wa Maliasili na Utalii, kwa hotuba nzuri iliyojaa ubunifu mkubwa na imedhihirisha utayari wa Serikali katika utekelezaji wa ustawi wa jamii na maendelo endelevu, na hii ni mojawapo ya nguzo kuu katika utayari wetu wa Ushindani wa Kimataifa (National Competitiveness). Bajeti hii inaenda sambamba na Dhima ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2021/2022 – 2025/2026 ambayo ni Kujenga Uchumi Shindani na Viwanda kwa Maendeleo ya Watu.”

Mheshimiwa Spika, pamoja na programu ya kutunza maliasili zetu, Serikali iweke usimamizi wa msitu hasa ya asili, ambayo inaendelea kupotea kwa matumizi ya nishati. Katika kupangilia matumizi mazuri ya ardhi, ihusishe Wizara zote zinazosimamia Maliasili, Ardhi, Kilimo, Wizara za Maji na pia Wizara inayosimamia Mazingira. Kwa vile binadamu tunaongezeka ni muhimu kuhakikisha ulinzi kwa kuhifadhi mazingira yetu na kuwepo msukumo zaidi kwenye kuboresha mazingiara.

Mheshimiwa Spika, napongeza hatua zinazochukuliwa na Serikali kurejesha mahusiano mazuri kati ya TANAPA (Hifadhi ya Kitulo) na wananchi wa Kata za Ilungu, Igoma, Ulenje na Inyala. Kuna mgogoro wa miaka mingi wa mpaka kati ya TFS na wananchi wa Kijiji cha Mwashoma, Kata ya Inyala. Kutokana na mgogoro huu kuchukua muda mrefu na kusababisha hata uvunjifu wa amani, kuna ahadi ya mwaka 2015 alitoa Mheshimiwa Hayati Magufuli na kumwelekeza Waziri wa Ardhi na pia Waziri wa Maliasili na Utalii wa wakati huo kupitia upya mipaka ili wananchi wa kata za Inyala, hususani Kijiji cha Mwashoma waachiwe maeneo yao.

Mheshimiwa Spika, maeneo yenye mgogoro ni mashamba ya wananchi na wamekuwa walinzi wazuri wa misitu na vyanzo vya maji, ni imani yangu wakiachiwa hayo maeneo yanayogombewa na TFS, kuna maslahi mapana kwa Taifa.

Mheshimiwa Spika, napongeza juhudi za Serikali kuweka umuhimu wa kipekee na kupewa kipaumbele kwa sekta ya utalii ili iendelee kuchangia pato la Taifa, uhifadhi wa mazingira, na ustawi wa jamii kupitia fursa za matumizi endelevu ya rasilimali za utalii. Mheshimiwa Rais amekuwa mstari wa mbele kutangaza utalii kwa kutumia mikakati mbalimbali ikiwemo Programu ya Tanzania - The Royal Tour ambapo kwa mwaka 2022, idadi ya watalii imeongezeka kwa asilimia 58 kufikia watalii 1,454,920. Kwa mwaka 2022 mapato yatokanayo na watalii yameongezeka kwa asilimia 93 hadi kufikia dola za Marekani milioni 2,527.72.

Mheshimiwa Spika, mchango huu wa sekta ya utalii bado ni mdogo sana kulinganisha na nchi shindani na hata kulingana na maoteo ya Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi na Mpango wa Tatu wa Taifa wa Maendeleo. Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2020 na Mpango wa Tatu wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano (FYDP III 2021/2022-2025/2026) umeelekeza kufikia idadi ya watalii wapatao milioni tano na kukusanya mapato ya kiasi cha dola za Kimarekani bilioni sita kufikia mwaka 2025/2026.

Mheshimiwa Spika, mchango wa sekta ya utalii unakabiliwa na changamoto ya ushindani mkubwa katika soko la utalii wa kimataifa hasa kutokana na miundombinu na hata mazingira ambayo siyo rafiki kwa wawekezaji ikiwemo utitiri wa tozo. Biashara ya utalii ni sawa na biashara zingine za nje zinazotegemewa katika mapato ya fedha za kigeni, lakini inakabiliwa na utitiri wa tozo katika mnyororo mzima na kupelekea kuwa mzigo mkubwa kupambana na ushindani wa kimataifa.

Mheshimiwa Spika, watalii kama ilivyo kwa biashara zingine wanaangalia sana ubora wa huduma pamoja na gharama katika mnyororo mzima wa utalii. Pamoja na nchi yetu kubarikiwa utajiri wa vivutio vya aina mbalimbali, inatakiwa kuwepo na mkakati madhubuti wa kuhakikisha uendelezaji wa vivutio ili kuongeza wigo wa shughuli za utalii na hata kuondoa tozo ambazo ni mzigo kibiashara. Serikali iangalie kuondoa kodi zote ambazo hazotozwi na nchi shindani na pia mnyororo wa biashara ya utalii ichukuliwe kama biashara ya nje (export).

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.