Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Dr. John Danielson Pallangyo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Arumeru-Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami nichangie kwenye bajeti hii ya Maliasili na Utalii, Wizara ambayo kwa kweli ni nyeti, ambayo inachangia percent 25 ya fedha zote za kigeni pia percent 17.5 Pato la Taifa.

Mheshimiwa Spika, nawapongeza sana Waziri, Mheshimiwa Mchengerwa, Naibu wake, Mheshimiwa Mary Masanja pia na Naibu Katibu Mkuu na Katibu Mkuu, kwa kazi nzuri ambayo wanafanya Wizarani pamoja na watumishi wote ambao kwa kweli wote wanachangia katika kazi nzuri ambazo zinafanywa na Wizara hii, ikiwa ni pamoja na Wakuu wa Taasisi ambazo ziko chini ya Wizara.

Mheshimiwa Spika, nilibahatika kutembea wakati wa ziara za Kamati kukagua miradi, tulikwenda Ngorongoro, tulikwenda TANAPA kule Mkomazi, tulikwenda TANAPA Rubondo. Kwa kweli kazi zinazofanyika ni za uhakika. Nikupongeze sana Mheshimiwa Waziri kwa kazi nzuri ambayo mnafanya, wewe tunakufahamu, ni mtu mwema pia ni mchapakazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nijikite kwenye Hifadhi ya Arusha. Hii hifadhi ilianzishwa mwaka 1960, mwaka mmoja kabla hatujapata Uhuru wetu. Nimekuwa nashangaa kwamba ni kwa nini hii hifadhi ilitwa Arusha mpaka leo inaitwa Arusha, lakini kumbe hifadhi yenyewe ni sehemu ya Msitu wa Mlima Meru. Watalii wengi wanakuja wanapanda ule Mlima, nikaona heri leo nishauri Mheshimiwa Waziri ile hifadhi badala ya kuiita Arusha National Park, kuanzia leo ibadilike uiite Hifadhi ya Taifa ya Mount Meru (Mount Meru National Park). Nakuomba ikiwezekana leo wakati wa kuhitimisha hapa utangaze kwa Watanzania kwamba sasa ile hifadhi itakuwa ni Hifadhi ya Taifa ya Mlima Meru.

Mheshimiwa Spika, kwenye ile hifadhi kuna mgogoro. Niliwahi kufika kwenye ofisi ya Waziri nikamwambia kwamba tupange angalau tende kule Jimboni aende azungumze na wananchi, bahati mbaya ile timu ya Mawaziri Nane ambayo ilizunguka nchi nzima haikuweza kufika pale hifadhini iweze kuzungumza na wananchi. Kwa hiyo nakuomba ile agenda ya kwenda Momela ukazungumze na wananchi wa kile kitongiji usiiache. Upange twende ukazungumze na wale wananchi kwa sababu ule mgogoro ulianza siku nyingi na ulitokana na mashamba mawili, Na. 40 na Na. 41 kutwaliwa na Serikali ambayo mashamba haya yalikuwa yanamilikiwa na wawekezaji, mwekezaji wa kwanza akafa, akachukua mwingine baadaye yakamshinda akaya-abandon akayaacha pale.

Mheshimiwa Spika, wakati ulipokuja mpango wa vijiji na vijiji vya ujamaa, wananchi waambiwa wajipange kule wajikimu na kufanya kazi za kilimo na ufugaji. Mwaka 2017 Serikali iliwatoa kwa nguvu na baada ya pale hakuna kilichofanyika, wananchi wale wameachwa wanateseka wametupwa kwenye lindi la umaskini, niseme ukweli kwamba Serikali ina haki ya kuchukua ardhi yake kwa sababu ndiyo yenye mamlaka, lakini inavyotoa wananchi bila kujua wanawapeleka wapi, kidogo hiyo haiko sawa. Naamini kabisa kwamba Serikali ina nia njema, haiko hapa ku-displace wananchi wake lakini inapaswa ifanye relocation. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri nakuamini wewe ni mtu mwema hili tatizo nina uhakika utalimaliza.

Mheshimiwa Spika, pia nadhani nilishawahi kuzungumza tena hapa kuhusu cable cars. Wakati unabadilisha jina la ile hifadhi uweke pia na cable car pale kwenye lango la kuingia hifadhini ambayo itakwenda mpaka Miliakamba. Nakuhakikishia ukiweka hiyo cable car idadi ya watalii wa ndani itaongezeka mara dufu. Nakuomba uliweke kwenye mpango ili tuweke huo mpango wa cable car.

Mheshimiwa Spika, naona unataka kunisemesha, basi niseme tu kwamba nakushukuru sana kwa muda huu mfupi, naunga mkono hoja. (Makofi)