Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Innocent Sebba Bilakwate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyerwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia Wizara hii muhimu.

Mheshimiwa Spika, awali ya yote kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu ambaye amenipa afya na nguvu ya kuendelea kuwatumikia wananchi wangu wa Jimbo la Kyerwa, pia nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa na nzuri aliyoifanya ya kutangaza vivutio vyetu na tumeanza kuona faida kubwa ya Royal Tour ambayo imeanza kuleta watalii wengi na kuongeza fedha za kigeni.

Mheshimiwa Spika, pia nimpongeze Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Waziri sasa hivi hii ni Wizara ya tatu na kila ulikoenda kwa kweli ulienda na matumaini na uliacha matumaini na ninaamini Wizara hii ambayo imeleta makovu mengi, imeleta huzuni na masikitiko kwa watanzania sasa naamini imepata mwenyewe.

Mheshimiwa Spika, tumeongelea suala la tembo, kwa kweli tembo tunawapenda na wanadamu tunawapenda, jambo hili Mheshimiwa Waziri lazima ujipange. Watu wamejeruhiwa, watu wameteseka muda mrefu sasa ni wakati wako kuleta majibu ambayo yanaenda kuponya haya majeraha ya muda mrefu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunapouliza hapa Bungeni wanakwambia tembo hawa ni njia yao walipita miaka 200, lakini jambo ambalo linasikitisha maeneo hayo ambayo yamevamiwa na tembo ni maeneo ambayo yametengwa kwenye vijiji kwa mujibu wa sheria. Wakati wanatenga haya maeneo Serikali haikujua hapa ni njia ya tembo? Kwa nini watenge haya maeneo wawapeleke wananchi, waende kuendeleza maeneo hayo, wana mashamba wamejenga nyumba. Kwa mfano, kule kwangu Kyerwa katika Kata ya Businde, Kata ya Bugara Kata ya Kibare wanaendelea maeneo mengi. Hawa tembo walikuja kama 20 sasa hivi wameshazidi 100, hivi Mheshimiwa Waziri kama mmeshindwa kuwafukuza hata mmeshindwa uzazi wa mpango? Leteni uzazi wa mpango wa hawa tembo, tembo hawa wanaua wananchi, wanatesa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, maeneo mengi kwenye kitongoji kimoja wameondoka wananchi zaidi ya 200, walikuwa na mashamba walikuwa wanafanya kazi zao vizuri. Nyumba zao zote zimeteketezwa halafu mnakuja mnasema kuna kifuta jasho. Mheshimiwa Waziri tunaomba hili uliangalie.

Mheshimiwa Spika, kifuta jasho mtu ana shamba zaidi ya heka 10, zaidi ya heka 20 ana migomba amejenga nyumba zaidi ya Shilingi milioni 20 unampa milioni moja, unampa 100,000 moja hiyo hela inamsaidia nini? Tumewafanya Watanzania kuwa maskini kwa sababu ya hawa tembo. Kwa hiyo ninakuomba sana Mheshimiwa Waziri unapokuja hapa kumalizia bajeti hii unapojumuisha hapa utueleze ni mikakati ipi umekuja nayo ili kuhakikisha mnadhibiti hawa tembo, vinginevyo hali ni mbaya na wanazaliana sijui namna gani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri niongelee jambo jingine kuhusu suala la mipaka ya hifadhi pamoja na wananchi. Tulisikia Serikali imeunda timu ya Mawaziri Nane, Mheshimiwa Waziri kama unataka kufanya hili jambo kwa ufanisi ile taarifa ya Mawaziri Nane usiende nayo. Jiridhishe wewe mwenyewe kwa sababu haiwezekani hawa Mawaziri Nane wanaenda kwenye Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, shida iko Kyerwa nyinyi mnaishia pale Bukoba Mjini. Haiwezekani! Kwa hiyo Mheshimiwa Waziri jiridhishe na taarifa hii, lakini maeneo mengine walikuwa wanafika kwa vitisho kuwaambia hawa hapa hampati kitu lazima muondoke.

Mheshimiwa Spika, hawa wananchi mnaowafukuza kama siyo Watanzania hawa, hawa ndiyo ninaoamini wanaweza wakawa wahifadhi wazuri wa kulinda vivutio vyetu na kulinda maeneo yetu. Lakini mnavyowafukuza namna hii mnajenga chuki na uadui mkubwa. Kwa hiyo, niombe sana Mheshimiwa Waziri hili uliangalie na ulifanyie kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine Mheshimiwa Waziri nilikuwa najaribu kuangalia bajeti za nchi nyingine hasa kwenye mambo ya utalii. Mungu ametujalia vivutio vingi katika Taifa letu, lakini hivi vivutio tumevitangaza namna gani? Tunaona ile Royal Tour kitu ilichokifanya lakini tuombe na sisi kama Serikali lazima tujipange kuhakikisha tunatenga bajeti kubwa ya kutosha. Ukiangalia niwasomee kidogo Waheshimiwa Wabunge muone nchi yetu ilivyo na bajeti za nchi nyingine.

Mheshimiwa Spika, ukienda Rwanda, Rwanda naona kama Mkoa wa Kagera. Rwanda bajeti yao ya utalii ni Dola Milioni 4.5. Ukienda Afrika Kusini Dola Mil. 75. Ukienda Kenya majirani zetu Dola Mil. 3.5. Ukienda Tanzania kwetu Dola 1.5, jamani hata Rwanda? Hata Rwanda kwa kweli, hii hapana! Kwa hiyo, niombe sana Serikali ijipange kuja na bajeti kubwa tutangaze hivi vivutio ambavyo Mwenyezi Mungu ametujalia ili Tanzania tupate pesa. Tunaanza kukimbizana na wafanyabiashara, tunakimbizana na watu wengine wakati tunavvyo vitega uchumi pesa iko nyingi. Tuitumie fursa hii ambayo Mungu ametujalia ili tuone tutakavyopata pesa nyingi.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, ninakushukuru naunga mkono hoja.

SPIKA: Ahsante sana. Sijaelewa hapo umetaja Kagera halafu ukataja Rwanda ili nielewe vizuri mchango wako.

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Spika, yaani nilichokuwa nalinganisha ukiiangalia nchi ya Rwanda ni kama ina lingana lingana na Mkoa wa Kagera lakini wanatuzidi mara nne.