Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Kavejuru Eliadory Felix

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Buhigwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. KAVEJURU E. FELIX: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru sana kwa kunipa fursa hii na mimi kuchangia kwenye hoja ya Maliasili na Utalii. Awali ya yote nichukue nafasi ya pekee kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuwa mhifadhi namba moja na mtangazaji wa vivutio vya utalii namba moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pili ninampongeza Makamu wa Rais Dkt. Philip Isdor Mpango kwa juhudi kubwa na kazi kubwa anayoifanya ya kuhifadhi mazingira hapa nchini. Kipekee nishuke kwa Mheshimiwa Waziri nimpongeze rafiki yangu Mchengerwa mtu kazi pamoja na Dada Mheshimiwa Mary Masanja, Naibu Waziri, Katibu Mkuu Dkt. Hassan Abbasi Said, Naibu Katibu Mkuu Anderson Mutatembwa kwa kazi kubwa wanayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja waliyoiandaa ambayo sasa tunaijadili kuna mikakati mikubwa sana. Katika mchango wangu nitachangia mambo mawili tu. Moja ni maombi kwenye sehemu mbili ambazo zina migogoro kule Mkoani Kigoma. Mgogoro wa kwanza lipo eneo ambalo lina itwa Kagerankanda iko Kasulu, eneo hilo ni tegemeo kwa kilimo cha mahindi na maharage kwa Wilaya karibu tatu za Kasulu, Buhigwe na Kigoma Kaskazini. Uko mgogoro ambao umedumu kwa muda mrefu kati ya TFS na wakulima. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mgogoro huu chanzo chake ni TFS. Mvua zinapoanza kunyesha wakulima huruhusiwa kwa sababu hawajui mipaka na mipaka haijajulikana, TFS wanawaacha wanalima, wanapalilia, wanaweka mbolea ikifika wakati wa kuvuna kiangazi kama hiki, wanawazuia kuvuna mazao yao au wakienda kwa kujificha wanawanyang’anya mazao yao, hiyo ni dhuluma! Ninakuomba Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii Mchengerwa mtu kazi ushuke pale ndani ya Wilaya ya Kasulu uwasikilize wakulima utatue mgogoro huo na mipaka iwekwe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mgogoro wa pili ni wa Kijiji cha Karirani kiko katika Wilaya ya Uvinza, kinapakana na Hifadhi ya Milima ya Mahale. Kijiji hiki kilisajiliwa mwaka 1995 na kina barua ya usajili ya tarehe 5 Juni, 1995 na kina usajili wa Namba 244. Kuna taharuki kubwa sasa hivi katika kijiji kile. Tarehe 13 Machi mliwapelekea barua kuwaonesha katika vitongoji vinne kati ya vitongoji vinne katika Kijiji cha Karirani vitongoji viwili mnasema viko kwenye sehemu ya hifadhi. Vitongoji hivyo ni Mahasa na Kabukuyungu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vitongoji hivi vina kaya 479 zenye idadi ya watu 1,721. Kuna taharuki kubwa, hawa ni Watanzania, wamekaa pale zaidi ya miaka 28. Eneo hilo ambalo mnarudisha kwenye hifadhi ya Milima ya Mahale lina Shule ya Msingi, lina makanisa sita, lina misikiti miwili na taasisi zingine za Kiserikali wana nyumba za kudumu. Mmepeleka barua mwezi wa Tatu tarehe 30 mnatuma Kamati ya Ulinzi na Usalama kuwajazisha fomu waondoke bila kuongea nao. Hiyo siyo halali, haikubaliki! (Makofi)

Mheshimiwa Spika, haiwezekani hifadhi yoyote ile conservation is for human development ni kwa ajili ya maendeleo ya watu. Ni lazima mshuke muwashirikishe wananchi. Hatukatai, tunajua mnayo programu ya kuhakikisha kwamba zile shoroba ambazo zilijengwa sasa ziwe wazi lakini muende kwa utaratibu wa kiutu. Tunataka fedha lakini hatutaki migogoro. Hatutaki kuona kila mwaka kwenye taarifa au kwenye ripoti kwamba askari wangapi wameuawa, au wananchi wangapi wameuawa. Hatutaki fedha tutakazozipata kutoka kwenye Wizara hii zingine ziwe zimeambatana na damu ya watu. Itakuwa ni dhuluma, hatuwezi kubarikiwa kama Taifa na hatuwezi kupata baraka. Ninakuomba sana ushuke pale Karirani uwasikilize wananchi wako, ni Watanzania uwasikilize muyaweke mambo sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sehemu ya pili ni ya ushauri. Nimesoma bajeti yako ukurasa ule wa 27 kuna biashara ya hewa ya ukaa, nami ninaenda kuungana na Mheshimiwa Reuben kwamba makusanyo yanayokusanywa na Wizara yako bado ni madogo. Sasa hivi kuna biashara ya hewa ya ukaa na nimeona mmeingia mkataba na kampuni mbili. Ipo Kampuni hii moja ya Singapore ambayo inaonekana tayari mmekwisha ingia mkataba na mmelipwa shilingi bilioni 8.4. Je, mmeshindanisha? Bado mmeingia tayari kwenye mkataba na Falme za Kiarabu kuna Kampuni hapo inaitwa Carbon Cop; je, mmeshindanisha? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika nchi hii kwenye maliasili kwenye misitu tunayo misitu ambayo ni natural forest zaidi ya 452 na tunayo misitu ambayo iko chini ya Halmashauri ambayo inamilikiwa na Halmashauri 46 lakini inatia aibu mpaka sasa hivi katika nchi nyingi wenzetu majirani wa Kenya wanavuna fedha nyingi kutokana na biashara hii ya ukaa, sisi bado tuna misitu hii miwili. Je, mmekwisha fanya tathmini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, biashara hii ya hewa ya ukaa imezungumzwa kwenye Wizara ya Mazingira na ninyi mmeizungumza. Je, fedha ambayo sasa mmepanga au kwenye mkataba huu ni Wizara ipi itakayohusika na makusanyo hayo? Ninaomba utakapokuja ku-finalize mtuelekeze ni Wizara gani hasa itakayohusika kwa sababu Wizara ya Mazingira ndiyo imetoa mwongozo namna gani hiyo biashara inaweza ikafanyika lakini tunaona tayari kwenye mikataba tayari iko ndani ya Wizara ya Maliasili na Utalii na tunaomba hawa TFS ambao wanatumia nguvu kubwa kupitia Askari Wanyamapori ambao wanatumia nguvu kubwa ya kuonea wananchi waumize kichwa sasa hivi wasaidie namna ya kuwashirikisha wananchi kwa sababu wananchi ndiyo wahifadhi namba moja. Hakuna usalama bila kushirikisha wananchi. Hao ndiyo wahifadhi namba moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya hayo mimi ninakushukuru sana, ninaunga mkono hoja na ninakuombea sana kwenye lile jambo lako ambalo umeomba tunakuombea ushindi wako itakuwa ni heshima kwetu. Uthubutu wako ni heshima kwetu na Mungu akutangulie na akubariki sana. (Makofi)