Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Eng. Stella Martin Manyanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nyasa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa hii nafasi.

Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu lakini la pili nimpongeze sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, mtalii na muongoza watalii namba moja. Vilevile, naomba nikupongeze wewe mwenyewe na kukushukuru sana, pia nakushangaa una nguvu za ajabu, unakaa Bungeni na sisi kama haupo kwenye kiti unamaliza majukumu yako yote mezani, mambo yetu yote yanaenda vizuri, hakika hutashindwa pia kuongoza hilo Bunge la Dunia. Hutashindwa kwa sababu uwezo wako ni mkubwa sana, tunakuombea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile nichukue nafasi hii kuwapongeza sana Mheshimiwa Waziri, Ndugu yetu Mchengerwa pamoja na Naibu wake Ndugu yetu Mary Masanja, wakati huo huo nawapongeza Katibu Mkuu pamoja na timu yao yote siyo rahisi kumtaja kila mmoja sasa hivi kwa kazi kubwa wanayoifanya katika Wizara hii. Kwa namna hiyo pia ninavipongeza vyombo vya habari bila vyombo vya habari mambo ya utalii kwa vyovyote vile yatadorora. Kwa hiyo, nawapongeza Safari Channel wa TBC, wanapongeza Channel Ten, nawapongeza ITV na vyombo vyote kwa kweli, Azam Tv na vyombo vyote ambavyo vinajihusisha katika kuhakikisha kwamba wanahamasisha utalii na hasa katika maeneo yale ambayo bado yapo nyuma ki utalii ikiwemo Wilaya yangu ya Nyasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda pia kuungana na ndugu zangu kule Mwanza kufuatia kifo cha Mwanahabari Magreth Tengule ambaye alikuwa ni mpenzi sana wa uandishi katika nakala za afya na utalii, Mwenyezi Mungu amrehemu. Mheshimiwa Naibu Waziri kuna wakati alikua amekuja kwenye Wilaya yangu ya Nyasa na kule kulikuwa na mgogoro mkubwa sana kwenye Pori la Liparamba na jirani zao ambao ni vijiji vinavyozunguka lakini alivyoondoka alituahidi atalifanyia kazi na kwa kutumia kikundi kazi kilichoundwa cha Mawaziri leo mgogoro ule umeisha, mipaka imeshawekwa, imebakia sehemu moja tu kutokea Ndondo mpaka Liparamba ambayo ninaomba pia wakamalizie, naamini chini ya uongozi madhubuti ya Mheshimiwa Kaka yetu Mchengerwa Mjukuu wa Bibi Titi, Mama yetu jambo hilo pia litaisha salama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sambamba na hiyo pia nitoe taarifa ambayo siyo nzuri, mamba wetu wa maajabu ambaye tulikuwa tunampenda sana alikuwa mpole akiitwa anakuja, kwa bahati mbaya alinaswa kwenye nyavu na wale ndugu zangu wakamuona ni kitoweo basi hatuna naye tena. Kwa kweli tunashukuru tu kwamba alikuwa ameshakuwa na watoto basi ndiyo habari hiyo kwa sababu alikuwa anajulikana Dunia nzima ni maajabu.

Mheshimiwa Spika, napenda pia kuzungumzia kuhusu umuhimu wa kupanga maeneo ya ardhi yetu hasa katika Wilaya ya Nyasa. Sasa hivi Wilaya ya Nyasa inakua vizuri kiutalii, tumehamasisha kwa muda mrefu wadau wamekuwa hawajitokezi sana. Sasa hivi wametokea TAWA ambao wamechukua Mlima wa Mbamba Bay, Tumbi na Kile Kisiwa cha Lundo. Tunashukuru wameanza kazi nzuri na hivi juzi nimeambiwa tayari boti limeshaenda kwa ajili ya kuwapeleka wataliii kule Kisiwa cha Lundo. Niwaombe sana Wizara kupita TAWA muendelee kuiangalia Wilaya ya Nyasa kwa sababu vivutio vyake ni vingi sana, vinahitaji uwekezaji. Sisi tunapata wivu sana tunaposikia Ngorongoro kuna jambo hili, Serengeti kuna jambo hili, sijui fukwe za wapi jambo hili na kule sisi kunabaki kumekaa kama vile hakuna wa kutumia hizo fukwe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo jitihada zilizoanza tunaomba muendelee nazo na ninazidi kuwasihi wale wote ambao wanatabia ya kuvamia maeneo kwenda kuleta vurugu kusema kwamba mlima huu wanasema na wenyewe ni wa kwao lazima tufuate taratibu na sheria za nchi. Kwa hiyo, ninawaomba sana mtu yeyote anayetaka kuwekeza kwenye milima hiyo basi hii milima yote ambayo tayari imeshakabidhiwa kwa TAWA wahakikishe wanawasiliana nao ili taratibu zifuatwe na uwekezaji ufanyike bila migogoro. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ninalotaka nilizungumzie ni kuhusu asali. Nimeona hapa katika taarifa zetu ukiangalia toka mwaka 2005 asali tulikuwa tunavuna kiasi cha tani 465 ambayo thamani yake ilikuwa tu kama milioni 550. Sasa hivi asili katika miaka kuanzia 2017 mpaka 2022 imeendelea kuongezeka na hata pale ilipokuwa inapungua imekuwa bado thamani yake ni kubwa. Kwa hiyo, niwaombe Wizara kuendelea kulisaidia zao hili la asali pamoja na nta, kwa sababu zao hili linamgusa mwananchi mmoja mmoja ukiacha hayo mambo mengine ambayo fedha yake inaenda moja kwa moja kwenye mifuko mikubwa ya Kitaifa, lakini kwenye asali na nta inaenda moja kwa moja kwa wale wananchi wa kawaida. Kwa hiyo, niwaombe sana kulitilia mkazo zao hili lakini pia linatusaidia sisi katika kuapata afya.

Mheshimiwa Spika, wakati ule ilikuwa ukienda sokoni unataka asali unapewa asali iko kwenye chupa ya konyagi tena hiyo chupa sijui imeokotwa vipi shida tupu na hupati wakati mwingine, lakini sasa hivi asali ni zao ambalo unalipata kiurahisi kila mahali na kwa kweli kwa namna ya kipekee kabisa inaandikwa kwenye historia Mheshimiwa Mzee Pinda, Waziri wetu Mkuu Awamu ya Nne anastahili pongezi katika mdudu huyu anayeitwa nyuki pamoja na asali yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nazidi kuomba kwamba tuwe na utamaduni wa kuandika historia za watu. Kama ambavyo leo tunamuona Mama, Mheshimiwa Rais alivyohangaika na Royal Tour aandikwe historia yake vizuri kwa sababu anayetenda jema apongezwe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia, nikiendelea katika hili suala la makumbusho, makumbusho ukiangalia ni kama vile eneo la utalii ambalo halipendezi pendezi hivi, lakini sisi wenyewe tunashuhudia kila wakati wanapokuja viongozi wa Kitaifa kutoka nchi mbalimbali sehemu wanayokimbilia kwenda ni kwenye makumbusho. Ina maana wanataka kujua historia yetu wanataka kujifunza mambo mbalimbali lakini pia kupitia historia kama hizo zinatoa kipimo namna gani watu wamepiga hatua za kimaendeleo kutokea wakati huo mpaka sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa misingi hiyo nataka kufahamu Wizara imejipanga vipi katika kuhakikisha kwamba makumbusho haziishii tu ziwe za siku nyingi, kwa sababu kila siku zinazaliwa historia nyingine. Wamejipanga vipi katika kuendeleza masuala ya kimakumbusho. Kuna mwongozo wowote ambao upo kwa ajili ya kuendelea makumbusho? Nasema hivyo kwa sababu hata CAG ameuliza swali hili. Kwa hiyo, nimeona na mimi niongeze mbele lakini pia hata nikifuatilia katika baadhi ya maeneo naona makumbusho ziko maeneo machache sana. Hapa Dodoma sijui lini sasa tutaijenga makumbusho kubwa kabisa ya Kitaifa. Kwa hiyo, niwaombe sana suala la makumbusho ni muhimu kwa sababu watu tunakuja, tunapita, vitu vinakuja vinapita, historia zetu zinakuja zinapita lakini tunapokuwa tumeziweka vizuri zinasaidia hata watoto wetu kujifunza hatua kwa hatua za mabadiliko na maendeleo yetu katika nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sambamba na suala la Makumbusho ya Taifa ninazidi kuwaomba kwamba katika makumbusho mojawapo ambayo ni ya Majimaji kule Songea bado pamoja na kwamba sasa hivi tunaona kila mwaka ina adhimishwa inapofikia tarehe 27 mwezi wa Pili lakini ile jitihada ya Serikali ya kuwekeza bado ni kidogo, ndiyo maana hata wenzetu wa kule Nandete Rufiji wanalalamika. Kumbe tungeunganishwa sasa hivi tukawa kama circuit moja, makumbusho kimsingi, kisheria, ikishakuwa imekaa zaidi ya miaka 100 automatically inakuwa imeshaingia kwenye kuwa ni Makumbusho ya Kitaifa. Sasa wale Nandete kwa nini kila siku wanakumbusha jambo hilo hilo? Kwa hiyo, mimi niwaombe sana Wizara katika suala hili la kuunganisha hizi historia zetu hizo hazitaki mjadala mrefu. Kinachotakiwa ni sisi kuhakikisha kwamba tunajipanga na kuona kwamba makumbusho hizo zinawekwa katika historia yake inavyotakiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la mwisho ni kwamba, Wizara hii imepata viongozi vijana, kuna kufanikiwa katika wanayofanya, kuna kukosea kutokana na ujana wao na sisi kila siku tunasema kwamba vijana wapewe nafasi, basi pale wanapokuwa wameteleza tuwaelimishe kwa upole, tuwasaidie ili waendelee kufanya vizuri, hiyo itakuwa ndiyo Tanzania tunayoitaka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa maneno hayo nashukuru, naunga mkono hoja. (Makofi)