Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Daimu Iddi Mpakate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi mchana huu kuongea mambo mawili, matatu kuhusu Wizara ya Maliasili na Utalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, nimshukuru Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuifanya hii sekta ifufuke na iweze kufanya kazi vizuri kwa kutuletea kipato na kuongezeka kwa watalii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi leo nitaongelea jambo moja tu ambalo ni tembo. Wilaya ya Tunduru kuna hifadhi za misitu za TFS ziko nne, Wilaya ya Tunduru kuna Mbuga ya Selous, Wilaya ya Tunduru kuna Hifadhi za WMAs za wananchi ambazo zina kilometa za mraba 2,288. Hizi hifadhi Nne za TFS zina hekta 711,834.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hifadhi hizi karibu Kata 13 za Jimbo la Tunduru Kusini kati ya 15 zimepakana na hifadhi hizi, WMAs pamoja na Selous. Kata zaidi ya 15 zimepakana na hizi hifadhi upande wa kaskazini. Kwa hiyo Tunduru maeneo makubwa ni sehemu ya mapito ya tembo, ushoroba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tembo wanaotusumbua Tunduru wanatoka Msumbiji, wanapitia Mbuga ya Mwambesi – Chingweli – Nalika wanaingia Selous. Wengine wanatoka Selous, wanapita Mbuga ya Nalika – Chingweli, wanapita Hifadhi ya Sadawara na kwenda Msumbiji. Kwa hiyo miaka yote hii ndiyo tabia ya hawa tembo ambao wanapita maeneo haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya adha hii ya tembo kila mwaka inapofika mwezi Aprili au Mei, Tunduru hatuna amani. Kipindi cha mwezi Mei peke yake Jimbo la Tunduru Kusini limepoteza watu wanne. Kijiji cha Kazamoyo wawili, pale Mbati mmoja na Kijiji cha Masuburu mmoja, wote wamekanyagwa na tembo, zaidi ya watu 2,000 wameathirika mashamba yao kwa sababu ya tembo kula mazao ya wakulima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na adha hii watumishi wa Halmashauri Maafisa Wanyamapori wako sita tu, na hifadhi ziko nne ambazo ni za TFS na humo ndimo ushoroba hawa tembo wanamopita. Hawa TFS watumishi wako saba tu na walio wengi wamesomea mambo ya majani na miti, wakiona hata nyoka wanaruka na kukimbia. Kwa hiyo, hii kero ni kubwa, hawa wenzetu wa TANAPA na TAWA wamejenga kituo pale, tunashukuru, kina watu nane. Kule Kalulu wapo kama sita, nao wanaendelea na Mbuga yetu ya Selous, sasa utakuta maeneo makubwa hayana askari wa kuweza kusaidia kufukuza hawa tembo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu kwa Serikali. Adha ya Tunduru kufa watu, watu kuliwa mazao yao imekuwa ni kubwa, tuongezewe askari na vituo vya kuweza kuwafukuza hawa tembo. Naomba sana Wizara hii iangalie kwa kweli Serikali Tunduru inatukanwa sana, hasa Jimbo la Kaskazini upande ule unaopakana na Selous na hasa Jimbo langu mimi kwenye Kata 15 ambazo ni zaidi ya vijiji 45, wote hawa wanaathirika na tembo. Mazao yao yanaliwa. Anatukanwa Rais, anatukanwa Waziri Mkuu, anatukanwa Mbunge, anatukanwa DC na Madiwani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka juzi wakati tunaandikisha sensa kuna vijiji walikataa kujiandakisha wakasema nendeni mkawaandikishe tembo ambao wanatusulubu kila siku. Ndipo tulipofika Tunduru! Naomba sana, hili jambo kwa Serikali ni dogo sana, ni kuongeza askari waweze kusaidia kuwafukuza hawa tembo, vilevile kuongeza vituo ambavyo askari watakuwa wengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi…

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa Mheshimiwa Kuchauka.

TAARIFA

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Ninampa taarifa mzungumzaji kwamba katika michango yangu hata mimi nilisema kwamba tupatiwe askari kwenye kila Kata ambayo inaonekana ina ushoroba wa hawa tembo ili tuweze kuwadhibiti, Serikali wakasema kwamba utaratibu huo unaendelea kufanywa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nampa hiyo taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Daimu Mpakate, unaipokea hiyo taarifa?

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea taarifa hii kwa kweli na ninapendekeza katika hilo kwenye Jimbo langu kila Tarafa angalau kuwe na kituo kimoja ambacho kitakuwa na platoon, siyo askari watatu au wanne, waweke platoon kwa sababu hili tatizo ni la kudumu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa tembo wa Msumbiji wapo kwa sababu tunapakana na Hifadhi ya Nyasa. Hii hifadhi ni ya muda mrefu na kipindi kirefu na kutoka Mto Ruvuma hiyo hifadhi ina zaidi ya kilometa 100 kwenda Msumbiji, kwa hiyo tembo wanakuja Tanzania kutalii, kuzaana na kula mazao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi Tembo hawa wameshakuwa na ratiba ya mavuno yetu. Kipindi cha mavuno wanatoka Msumbiji wanakuja wanashambulia mazao ya wakulima. Njaa Tunduru ni kubwa sana. Nashukuru mwaka jana Serikali ilitupa mahindi ya msaada ya bei nafuu, tunaomba hali mwaka huu ni mbaya zaidi kuliko mwaka jana, haya mahindi yapelekwe tena mapema sana kuanzia mwezi wa nane wa tisa kwa sababu mazao yao mengi tayari yameshaharibiwa na tembo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na upungufu wa wafanyakazi wa wanyamapori kuwa sita na huko TFS kuwa saba yaani wawili ni Maafisa wa Nyuki, watatu wanakwenda na miti hiyo na wawili hawa ni Maafisa wao kwa maana ya kwamba ni ma-in charge. Maeneo yote ya hifadhi hizi ni mapito ya ushoroba wa tembo sasa naomba hata TFS waajiri watu ambao watasaidia kufukuza hawa tembo au watoe mafunzo zaidi kwa hao waliokuwepo kwa sababu kama anamuona nyoka anakimbia. Kuna askari mmoja kule safari hii wakati wanafukuza Tembo amekimbia ameacha bunduki amekimbia kwa sababu ya kumwogopa tembo. Ni kwa sababu hana mafunzo yale ya kufukuza tembo. Naomba sana Mheshimiwa Mchengerwa, unajua nimekusumbua mara nyingi. Nashukuru wiki iliyopita umepita umeleta askari angalau wamefukuza wale Tembo wameenda Msumbuji lakini juzi wamehamia upande mwingine kwenye Kata nyingine. Nashukuru na jana wameenda, leo hii nimepata taarifa kuna sehemu nako wamevamia kwenye Tarafa nyingine. Naomba sana tupelekeeni hivi vituo haraka pelekeni askari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa uchache wake kwa Tunduru peke yake tunahitaji zaidi ya askari 40, lakini bajeti iliyopita mlisema mtaajiri VGS 600, tunashukuru tumepewa VGS nane tu, wanne Pori la Ngorika halafu na wengine pori lingine la Nyarika. Jambo hili kwa kweli bado halina afya. Kila pori linatakiwa angalau askari 20 watasaidia kwa sababu mapori haya ya vijiji yana wanavy vijiji Zaidi ya 26 ambavyo vinahudumia vinapakana na hivi na nikwambie ukweli Tunduru Kata zaidi ya 28 kati ya Kata 39 zote zimepakana na hifadhi, aidha TFS au WMA au Mbuga ya Selous, kwa hiyo umuhimu wa kupeleka askari kule kwa ajili ya kusaidia kuwafukuza hawa wanyama ni mkubwa kwa sababu hiki kilio kipo kila siku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hapa sasa hivi nikikuletea meseji niliyoletewa kwa kweli utasikitika sana, najua tunataniana na uliniambia babu yangu utakoma safari hii. Naomba uniokoe hali kule ni mbaya chama kinaharibika Serikali inatukanwa. Tunaomba mtusaidie kupeleka Askari. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili kwa kuwa hawa tembo tumeshindwa kuwadhibiti basi tunaomba kibali, kule siku hizi wenzetu Wangoni, sisi Waislam hatuli lakini wenzetu Wangoni wanakula nyama ya Tembo. Tupeni kibali tuwapunguze wale tuwavune au wachukueni wengine muwapeleke huko ambako tembo hawapo kwenye hifadhi hizo. Kwa hiyo, kuna umuhimu wa jambo hilo kulifanyaia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kuhusu waathirika. Mpaka sasa tulilipa mwisho mwaka 2021, tumelipa 2020 na 2021, 2022 bado lakini katika hao waliolipwa wale walioathirika na wanyama wakali hawajalipwa. Kipindi hicho wamekufa watu kama 14 wote hao hawajalipwa katika ile milioni moja moja. Mabadiliko yale ya Sheria hebu ifanyeni haraka. Huwezi kulinganisha uhai wa binadamu kwa kumlipa kifuta jasho kwa milioni moja. Mheshimiwa Waziri kwa kweli hili ulifanye haraka, sheria ibadilike na hata fidia ya kwenye mazao kila heka mmoja mtu analipwa laki moja, ikiwa chini ya heka moja hawapati chochote. Kwa kweli tunaomba sana hii sheria iletwe mara moja, ibadilishwe watu wetu wanaathirika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana kwenye jambo la askari mlifanyie hima, zaidi ya askari 40 tunahitaji ili wakatusaidie kuokoa hali ya maisha ya watu wetu. Nakushukuru sana naunga mkono hoja. (Makofi)