Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Prof. Palamagamba John Aidan Mwaluko Kabudi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilosa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. PROF. PALAMAGAMBA J. A. M. KABUDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu rahimu kwa ruzuku ya uhai na afya, pia nikushukuru sana kwa kunipa nafasi nami nichangie katika Wizara hii ya Maliasili na Utalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa dhati kabisa kumpongeza Mheshimiwa Mohamed Mchengerwa Waziri, CPA Mary Masanja Naibu Waziri, Katibu Mkuu Dkt. Hassan Abbas na Naibu Katibu Mkuu Anderson Mutatembwa na Watumishi wote katika Wizara hii kwa kazi nzuri mnayoifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuanza na suala ambalo linatupa usumbufu mkubwa sana katika Jimbo la Kilosa nalo ni tembo kuharibu mazao na miji ya watu na kwa muda mrefu wananchi wetu hawajapewa kifuta machozi kwa uharibifu huo wa tembo na maeneo ambayo yameathirika sana ambayo ningeomba Wizara itusaidie kuwalipa kifuta machozi kwa haraka ni Kata ya Kimamba A katika maeneo ya Soko Msuya, Mkwajuni na Sikutari, Kimamba B, maeneo ya Uhindini, Kigamboni, Pusa na Mji Mwema, Kata ya Ludewa eneo la Peapea na Kata ya Madoto eneo la Mbwade na Kata ya Parakwio eneo la Mkata Stesheni na Mkata. Tutashukuru sana kupata kifuta jasho kwa wananchi lakini pia tupewe kituo cha kupambana na tembo hao kwa sababu tembo kutoka Hifadhi ya Mikumi wanakuja sana katika eneo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo ningependa kuchangia ni kuhusu Dodoma. Dodoma sasa ni Makao Makuu ya Nchi yetu, Dodoma sasa ni Jiji na ningependa kabisa kutoa ushauri kwa Wizara ya Maliasili na Utalii. Makao Makuu ya Nchi yanastahili kuwa na hifadhi kubwa. Kwa hiyo ninashauri Dodoma ipewe hifadhi, ianzishwe hifadhi kubwa inayoendana na heshima ya Mkoa huu lakini heshima ya Jiji hili. Pamoja na hayo tufikirie kuanzisha eneo kubwa la msitu (park) ambayo Miji mingine mikubwa wanayo, Berlin wana park kubwa sana ya Tiergarten. Sasa imefika mahali Dodoma pia tuwe na park kubwa sana ili Mji huu na eneo hili lilingane na hali na hadhi ya Mji. Tunaomba hifadhi kubwa ianzishwe katika Mji wa Dodoma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia kuchangia eneo jingine na hili ni kuhusu utalii.

MHE. ALLY J. MAKOA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

TAARIFA

MWENYEKITI: Mheshimiwa taarifa.

MHE. ALLY J. MAKOA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nilikuwa nampa taarifa Mheshimiwa Mbunge anayechangia kwamba Kondoa tayari tuna hifadhi mbili. Tuna Hifadhi ya Mkungunero ambayo ina wanyama wote na tunayo Hifadhi ya Swagaswaga nayo pia ina wanyama wote na pia pale Kondoa tuna eneo ambalo tumelitenga ni kubwa kwa ajili ya hichi anachokiongelea Mheshimiwa Mbunge Wizara inaweza ikachukua ikatengeneza hiyo park kubwa na Dodoma ikawa ina eneo kubwa ambalo litakuwa ni kivutio kwa Waheshimiwa Wabunge na Taifa kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Profesa Palamagamba unaipokea hiyo taarifa?

MHE. PROF. PALAMAGAMBA J. A. M. KABUDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea taarifa hiyo lakini naiboresha huko ni Mkoa wa Dodoma lakini Dodoma ni kubwa ni pamoja na Jiji la Dodoma. Kwa hiyo, naipokea hiyo taarifa lakini naongezea Jiji la Dodoma na lilikuwa maarufu sana kwa tembo na ndiyo maana inaitwa Dodoma, Idodomia maana yake hapa tembo walikuwa wanazama na njia yao ndiyo leo University hii ya UDOM ndiyo maana mara nyingi hurudi kuja kusalimia maeneo waliyoishi miaka na miaka ya nyuma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jingine ambalo ningependa kulichangia ni kwenye utalii na hapa nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa Royal Tour na tunasubiri kwa hamu sana hii film nyingine ya The Hidden Tanzania na ninaamini katika film ya The Hidden Tanzania hifadhi ya Kitulo itakuwemo. Ni hifadhi ya aina yake kabisa duniani na inastahili kutangazwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo jingine katika utalii ni upekee wa Tanzania katika utalii duniani na eneo la upekee wa Tanzania katika utalii duniani ni eneo la utalii wa vivutio vitokanavyo na hali ya jiolojia ya nchi (geo - tourism). Huu ni wakati sasa wa kusukuma geo – tourism, geo – conservation na kuanzisha geo – park nyingi iwezekanavyo. Hapa nataka nitoe maeneo 11 ambayo tukiyafanyia kazi hiyo, mengine tayari yametambuliwa na kuhifadhiwa, mengine bado. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ni Kilimanjaro. Sasa tuutangaze Mlima Kilimanjaro kuwa ndiyo mlima mrefu kuliko yote duniani wa aina ya volcano. Ndiyo mlima mrefu kuliko yote duniani wa aina ya volcano na Mlima Kilimanjaro hauna vilele viwili, una vilele vitatu kijiolojia navyo ni Shira ambayo ni extinct, Mawenzi ambayo ni extinct na Kibo ambayo ni dormant. Taarifa hizo zimo kwenye kitabu kinaitwa, “Kilimanjaro Mountain Memory and Modernity” kimechapwa na Mkuki na Nyota mwaka 2006, kina kurasa 321. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili muhimu sana ni Mautia Hill – Kongwa. Hiki ni kilima pekee duniani chenye madini ya aina ya Yoderite na jambo la kusikitisha, nakuomba Mheshimiwa Waziri chukua hatua za haraka hata ikiwezekana leo kwenda kukinusuru kilima hiki. Saa hizi ukipita pale karibu na Kongwa Ranch utaona wanachimba limestone. Kilima hiki kikipotea tumepoteza kilima pekee duniani chenye madini ya aina ya Yoderite. Kitangazwe kuwa ni kimehifadhiwa kiwe geo–park na wewe Wizara ya Maliasili na Utalii, Ofisi ya Makamu wa Rais na Wizara ya Madini tukinusuru kilima hiki. Wanakuja watalii na wanasayansi toka Marekani, Ujerumani, Austria kwenda pale Mautia Hill – Kongwa na sasa ukona pana mchirizi kuna mtu anachimba limestone. Tukinusuru kilima hiki ambacho ni utajiri duniani wa pekee. Hakuna mahali pengine duniani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu ni Ngorongoro. Tulitangaze sasa Bonde la Ngorongoro kuwa ndiyo bonde kubwa duniani la aina ya volcano (the largest caldera in the world, the largest caldera in the world). Sehemu ya nne ni Empakai. Hili ni moja ya bonde la volcano lenye kina kirefu duniani (one of the deepest calderas in the world). (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sehemu ya tano ni Yalumba kule Ludi -Kibakwe na Ikora kule Katavi. Hapo una miamba ya zamani kuliko yote duniani ya mfumo wa aina ya eclogites hupati sehemu nyingine duniani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la sita ni Oldonyo Lengai. Huu ni mlima pekee duniani wenye volcano ya aina ya cobaltite na saba ni Kimondo cha Mbozi (iron meteorites) na nane ni Mwadui. Mwadui ni moja ya Kimberlite kubwa duniani inayozalisha almasi kwa faida. Tisa ni Igwiti – Tabora, hiki ndiyo kilima chenye volcano ya aina ya kimberlite kule Igwiti – Tabora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumi ni Tendaguru. Tendaguru ambayo najua iko kwenye Jimbo la Mchinga la Mama Salma Rashid Kikwete. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tendaguru ndiyo kwenye masalia ya viumbe wakubwa duniani hawa dinosaurs, ambao walichimbuliwa na sasa wako katika Jumba la Makumbusho Berlin. Kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi tumezungumzia kujenga kituo kule. Kituo hicho kijengwe kiboreshwe na wenzetu Wajerumani sasa nyaraka na taarifa zote zipo na wametoa kitabu katika mambo yote ya Tendaguru kinaitwa, “Dinozauria Fragmente Zur Geschichte dea Tendaguru Efbideschion Undiire Objecte Nohis Hundadet Enzeks Bisdoiz Zauthousand Axzen” yaani kwa Kiswahili ni “Vipande vya Dinosauria, historia na masalia ya msafara wa kipaleontolojia kwenda Tendaguru Tanzania mwaka 1906 – 2018” na Mheshimiwa Waziri miaka yote tisa niliyokaa Berlin kila walipokuja wageni niliwapeleka kwenye museum Naturkunde ambayo iko kwenye Chuo Kikuu cha Humboldt Universitat zu Berlin ambako kwa bahati Mke wangu Dkt. Amina alifanya PhD yake pale, na ninazo picha ambazo nitazileta za watu wote walioshiriki kuchimba ile masalia. Tutengeneze Tendaguru iwe ni moja ya vivutio vikubwa vya utalii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, 11 ni Olduvai Gorge. Hii ndiyo bonde la kwanza duniani kukaliwa ni viumbe vya kwanza vyenye umbile la binadamu. Ndiyo chimbuko la kwanza la binadamu, ndiyo the first home of Zinjathropus Australopithecus Boisei. Hapa tufikirie upya zile nyayo. Wataalamu wa sayansi watusaidie ziendelee kufukiwa au sasa zifukuliwe ili watu wazione na katika kundi hili sehemu ya 12 ni Mapango ya Amboni. Haya ni mapango yanayotokana na limestone na yalitokea miaka milioni 150 iliyopita na katika kipindi cha Jurassic na kwa miaka milioni 20 yalifunikwa na maji. Najua yako mapango 10 ni moja tu ambalo linatumika. Tuone hayo tisa kama tunaweza tukaongeza mengine ili eneo nalo hilo liwe hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namuomba sana Mheshimiwa Mchengerwa na Wizara tuyahifadhi maeneo haya, tuyatambue maeneo haya, tuyatangaze maeneo haya na tuwe ndiyo watu wa kuonyesha dunia tunavyo vitu vya pekee ambavyo sehemu nyingine duniani havipo isipokuwa Tanzania tu na hii ni hali ya jiolojia ya nchi yetu ambayo Mwenyezi Mungu ametusaidia kuiumba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo jingine ambalo ningependa kushukuru ni kwenye upande wa malikale na kumbukumbu za Taifa. Nashukuru sana Mheshimiwa Waziri katika hotuba yako ukurasa wa 93 umetangaza kwamba Pango la Magubike katika Jimbo la Kilosa ni moja ya maeneo sita ya malikale ambayo mmebaini yanakidhi vigezo vya kuwa Urithi wa Taifa. Nawakaribisha sana mje tufanye, tutunze hilo pango la Magubike. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nakushukuru sana kuwa njia ya kati ya biashara ya utumwa na vipusa kutoka Ujiji hadi Bagamoyo pia vijiji viwili vya Jimbo la Kilosa vimo, Mamboya alikozaliwa Babu yangu na Rubeho. Nawakaribisha sana kufika katika maeneo hayo ili tuhifadhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Kilimatinde ambako anatoka Baba yangu na hapa Kilimatinde Mheshimiwa Naibu Waziri ameshafika. Ile nyumba waliyokaa Askari wa Kijerumani iliyokuwa officers mess leo ndiyo nyumba ya Kasisi pale inaanza kubomoka. Lile boma la mawe linaanza kubomoka. Yale makaburi matatu ya Maafisa wa Kijerumani waliofia Kilimatinde yameanza kuharibiwa. Yale makaburi saba ya Wajerumani Askari yameanza kuharibiwa. Naomba na kile kisima ambacho watumwa walikunywa maji kabla ya kushuka kwenye bonde la ufa pale Kilimatinde na ninaamini ndiyo iliyozaa Kilimatinde ya Pemba na ndiyo iliyozaa Kilimatinde ya Oman na ndiyo iliyozaa Kilimatinde Liverpool, ningeomba maeneo hayo pia yahifadhiwe ili yawe urithi wa Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa Kilosa naomba Stesheni ya zamani ya Kondoa, jengo ambalo halitumiki kati ya Kimamba na Kilosa lije litengenezwe ili ibaki kuwa ni kumbukumbu ya aina ya stesheni ambazo Wajerumani walizijenga lakini ile stesheni ina umuhimu mkubwa sana. Hiyo ndiyo ilikuwa njia ya watumwa na inaelekea watumwa hao kutoka Kondoa walipitia njia ya kutoka Kondoa kuja Mamboya wakashuka kuja mpaka pale, na tufahamu kwamba sehemu kubwa ya reli ya kati kutoka Morogoro mpaka Dodoma zamani ndiyo ilikuwa njia ya utumwa na njia ya biashara ya vipusa. Kwa hiyo nitashukuru sana lile jengo mkishirikiana na Shirika la Reli Tanzania kulitengeneza kulihifadhi kati ya Kimamba na Kilosa limepandwa miti linahitaji utaalamu ili nalo liwe sehemu ya vivutio vya utalii katika Kilosa ambayo sasa tuna tunnel zile tano za SGR lakini pia tunaomba kufungua sasa geti jipya kutoka Mji wa Kilosa kuingia katika Mbuga ya Mikumi ili watalii wakifika Kilosa na SGR waweze kwenda Mikumi na ninaamini kabisa katika hilo mtatusaidia kufungua haraka sana geti la Kilosa Mjini ili watalii hawa waweze kuingilia Mikumi lakini pia waweze kuingilia Kilosa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kutoa hayo yote nakushukuru sana kwa kuchangia na ninaunga mkono hoja asilimia 100 na ninaomba fidia ya kifuta jasho kwa ajili ya tembo kule Kilosa. (Makofi)