Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati

Hon. Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Spika, nachukua nafasi hii kuungana na Watanzania wenzangu wote kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kutujalia baraka zake katika nyanja mbalimbali za ustawi kwa Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, nachukua nafasi hii kuungana na wananchi wa Jimbo langu la Mbulu Mjini kumpongeza sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali nzima ya Awamu ya Sita kwa jinsi wanavyoliongoza Taifa letu na kutatua changamoto nyingi sana zinazowakabili wananchi hususan utekelezaji wa Ilani ya CCM yam waka 2020 - 2025 kwa kila sekta. Hivyo basi tuendelee kuliombea Taifa letu kwenye nguzo kuu ya amani, upendo, uchumi, baraka, utulivu, diplomasia ya kisiasa, na mshikamano kwa Mwenyezi Mungu.

Mheshimiwa Spika, naomba nikupongeze wewe, Naibu Spika na Wenyeviti wetu wote kwa kuliongoza Bunge letu katika kuzigatia Kanuni za Bunge kikamilifu na kwa busara ya hali ya juu hongereni sana.

Mheshimiwa Spika, aidha, sisi Wabunge wako tunaungana wote kukuombea mafanikio mema katika nafasi unayogombea, Mwenyezi Mungu awe kiongozi katika kufungua mapito yako upate kuchaguliwa kwa maslahi makubwa ya Taifa letu.

Aidha, nachukua nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa January Makamba, Waziri wa Nishati Naibu Waziri na watendaji wakuu wa taasisi zilizo chini ya Wizara hii.

Mheshimiwa Spika, sasa naomba kutoa mchango wangu kupitia mapendekezo na maoni ya Kamati yetu ya Kudumu ya Bunge na kupitia maoni ya Mheshimiwa Dunstan Kitandula, Mwenyekiti wa Kamati yetu na hotuba ya Mheshimiwa January Makamba Waziri wetu wa Nishati.

Mheshimiwa Spika, sasa naomba kuelezea hali halisi ya jiografia ya Jimbo la Mbulu Mjini; eneo la Mbulu Mjini tuna kata 17 kati ya hizo kata 11 ni maeneo ya vijiji na kata sita ni eneo la mitaa 58 ya miji. Hapa naomba kutoa maelezo ya hali ya uunganishaji wa umeme katika vijiji, mitaa na vitongoji. Ninaishukuru sana Serikali, tayari tumeweza kuunganisha laini kubwa kwenye makao makuu ya kila kata, kwa upande wa vijiji bado hatujaweza kuwasha umeme kwenye vijiji 11 hali inayowafanya wananchi kutopata huduma hii muhimu ya kuwaunganishia umeme. Mbaya zaidi katika maeneo mengi ya mitaa ya mji pembezoni kuna wateja wengi sana waliofanya kuunganisha waya kwenye majengo yao kwa lengo la kulipia shilingi 27,000 lakini wameshindwa kwa kuwa hawana uwezo huo wa kulipia gharama ya shilingi 320,000. Kwa hiyo, Serikali iangalie namna ya kuwaunganishia huduma ya umeme.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu kwa Serikali; Serikali yetu iangalie kwa kina suala la kuunganisha umeme kwa shilingi 27,000 katika maeneo ya mitaa ya miji yenye sura ya vijiji ili kuwezesha wananchi hao wenye uhitaji mkubwa kupata huduma hiyo muhimu. Serikali iangalie upelekaji wa umeme kwenye vitongoji kwa kuangalia vipaumbele maeneo ya taasisi za Serikali, binafsi, migodi ya madini na makazi mengi ya wananchi ili kutumia fedha kidogo kunufaisha watumiaji wengi zaidi. Kwa kuwa maeneo ya vijijini majengo mengi yako mbali mbali Serikali iangalie kutafuta kile chombo cha Umeme Tayari (UMETA) ili kuwapatia wananchi hao ambao hatutaweza kuwaunganishia kwa muda wa miaka mitano ijayo kutokana na umbali kati ya makazi na makazi mengine.

Aidha, Serikali ijitahidi sana kutoa fedha za bajeti ya Wizara hii kama ilivyoomba kwenye bajeti hii ili kufanikisha utekelezaji wa vipaumbele vyote vilivyoainishwa kwenye mapendekezo ya Wizara na maoni ya Kamati yetu ya Kudumu ya Bunge ili kujibu kiu ya wananchi.

Mheshimiwa Spika, katika muhtasari wa utambulisho wako wa wakuu wa taasisi zilizo chini ya wizara hii kuna nafasi nyingi za watendaji wakuu zinazokaimiwa, hivyo basi tunaiomba Serikali nafasi hizo zijazwe na watendaji wenye sifa stahiki ili kuleta ufanisi wenye tija kwa manufaa mapana ya Taifa letu.

Mwisho, naomba nitoe shukrani zangu kwa Mheshimiwa Waziri na watendaji wakuu wa Wizara yake kwa kutupatia mitungi 100 ya gesi ambayo itafanikisha kampeni ya kupunguza matumizi ya nishati ya kuni na kupunguza athari ya mabadiliko ya tabianchi, hongera Mheshimiwa Waziri ubarikiwe.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja na naomba kuwasilisha.