Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, napenda kuwashukuru na kuwapongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Dkt. Philip Isdor Mpango, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mawaziri na viongozi wote wa Wizara ya Nishati, kwa uongozi wao na utendaji uliotukuka.

Mheshimiwa Spika, napenda pia kutumia fursa hii kukupongeza wewe binafsi, Naibu Spika na uongozi wote wa Bunge kwa uongozi wenu mahiri na wenye ubunifu wa hali ya juu katika kuongoza mhimili wa Bunge.

Mheshimiwa Spika, napenda kumpongeza Waziri wa Nishati kwa hotuba nzuri iliyojaa ubunifu mkubwa na imedhihirisha utayari wa Serikali katika utekelezaji wa ustawi wa jamii na maendelo endelevu, na hii ni mojawapo ya nguzo kuu katika utayari wetu wa Ushindani wa Kimataifa (National Competitiveness). Bajeti hii inaenda sambamba na Dhima ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2021/2022 – 2025 /2026 ambayo ni “Kujenga Uchumi Shindani na Viwanda kwa Maendeleo ya Watu.”

Mheshimiwa Spika, naipongeza Serikali kupitia Wizara ya Nishati kwa kuendelea kutekeleza kwa ufanisi mkubwa miradi ya umeme ikiwemo Miradi ya Kusambaza Umeme Vijijini (REA) na ujenzi mkubwa wa Bwawa la Julius Nyerere (JNHPP) litakalozalisha umeme wa megawati 2,115. Miradi hii ya Kusambaza Umeme Vijijini umeiweka Tanzania katika nafasi ya juu Afrika na umeweza kuchochea kasi ya ukuaji wa viwanda na uchumi.

Mheshimiwa Spika, kutokana na changamoto za vita ya Ukraine na Urusi na kupelekea kupanda kwa bei ya mafuta ya petroli, napongeza Serikali kushirikisha Wizara ya Nishati, Wizara ya Fedha, EWURA na wadau wengine kuweka mkakati wa kuanzisha Mfuko wa Kudhibiti Mabadiliko ya Bei za Mafuta (Fuel Price Stabilization Fund) ili kukabiliana na kupanda kwa bei za mafuta. Pia Serikali ichukue hatua stahiki za kuanzisha Hifadhi ya Taifa ya Kimkakati ya Mafuta (Strategic Petroleum Reserve-SPR) ili kukabiliana na dharura na kuimarisha usalama na uhakika wa mafuta kwa Taifa.

Mheshimiwa Spika, kutokana na changamoto za upatikanaji wa dola za Kimarekani (USD) kwa kipindi kirefu sasa, makampuni yanayoagiza mafuta yanapata changamoto za kulipia mafuta kwa wakati na kulazimika kulipa faini kwa Shirika la PBPA. Kutokana na ukame wa USD kwenye soko la fedha za kigeni, makampuni yamelazimika kukopa kwenye mabenki kwa namna tofauti (post import loans, swaps, forward contracts etc). Kutokana na changamoto za upatikanaji wa dola, makampuni yameshindwa kuagiza mafuta ya kutosha na hali hii ni hatarishi kwa uchumi wa Tanzania.

Mheshimiwa Spika, pamoja na makampuni kulazimika kununua USD kwa gharama kubwa zaidi ya bei elekezi ya Benki Kuu, makampuni yameshindwa kulipia na kupelekea kushindwa kupokea mafuta.

Mheshimiwa Spika, nashauri Serikali kuchukua hatua za haraka kuchochea upatikanaji wa USD hasa kutoka vyanzo vya madini na kilimo na ikiwezekana kuanzisha utaratibu wa biashara ya Serikali kwa Serikali na nchi rafiki zinazozalisha mafuta kwa makubaliano kulipa baada ya makusanyo ya mauzo ya madini na kilimo. Serikali inaweza kuratibu mfumo mzuri wa kununua dhahabu yote toka kwa wachimbaji wadogo kwa shilingi na kulipa bei nzuri zaidi kuliko hata ya soko na ikifanya hivyo kwa mazao ambayo yamekuwa yanatoroshwa kinyemela nje ya nchi. Dhahabu na mazao yaliyonunuliwa kwa shilingi yapate soko zuri kwa wanunuzi kwa dola za Kimarekani kusaidia uagizwaji wa mafuta. Kwa taarifa za makampuni yanayoagiza mafuta yanahitaji zaidi ya USD bilioni moja ili kulipia mzigo uliofika nchini ila haujapokelewa na kila mwezi inatakiwa kutenga USD milioni 250 kwa ajili ya kuagiza mafuta ya ndani ya nchi.

Mheshimiwa Spika, mfumo wa kununua mafuta kwa pamoja (BPS) umeonesha mafanikio makubwa na napendekeza uendelee ikiwa ni pamoja na kuvutia kutumika kwa mahitaji ya mafuta kwa nchi jirani. Mfumo huu uboreshwe hasa katika kuweka vinasaba kwa kutumia mashine (automation) na pia kuwepo na ulinganifu wa taarifa ya kila siku kati ya kiasi cha vinasaba vilivyotumika na kiasi cha mafuta yaliyopakiliwa. Na pia magari ya kubeba vinasaba yafungwe kamera kwa ajili ya udhibiti mafuta yanayoenda nchi za nje pasipo kutorudi kinyemela kutumika nchini.

Mheshimiwa Spika, kutokana na changamoto za kupakua mafuta bandarini, napendekeza kupanua na kuboresha miundombinu ya kupakulia na kupokelea mafuta ikiwemo kupakua mafuta kwa saa 24. Napendekeza pia kujenga miundombinu ya kuhifadhi mafuta kwa matumizi ya ndani na pia kwa nchi jirani, na usafirishaji uwe wenye tija kubwa ikiwemo kusafirisha kwa treni. Pia Serikali iangalie uwezekano wa kujenga bomba la mafuta kwenye MKUZA wa TAZAMA na kujenga miundombinu ya kuhifadhi mafuta kwenye bandari kavu eneo la Inyala, Mbeya kwa matumizi ya mikoa ya Nyanda za Juu Kusini na nchi jirani za DRC, Zambia, Malawi na hata Zimbabwe.

Mheshimiwa Spika, pamoja na REA kutekeleza miradi ya kupeleka umeme kwenye makao makuu ya karibu vijiji vyote vya jimbo la Mbeya Vijijini, bado kuna uhitaji mkubwa wa umeme kufika kwenye vitongoji vyote. Napendekeza kuendelea kwa kasi utekelezaji wa Awamu ya Pili ya Mradi wa REA III (REA III, Round II) na kufikisha umeme katika vijiji vyote vilivyobakia na pia kuendelea na utekelezaji wa Mradi wa Ujazilizi (Densification). Napendekeza utekelezaji utoe kipaumbele kwa Kata za Itawa na Shizuvi na pia kwenye vitongoji vinavyolizunguka Jiji la Mbeya, ikiwemo Mina na Lusungo Kata ya Iwindi, Kijiji cha Shongo, Kijiji cha Wambishe, kwenye shule zote ikiwemo Shule ya Sekondari Iwiji.

Mheshimiwa Spika, katika vijiji vilivyopatiwa umeme kwa kiasi kikubwa imechochea ukuaji wa viwanda hasa vya kuongeza thamani ya mazao ya kilimo. Nashauri TANESCO iongeze speed ya kuunganisha umeme na pia kushughulikia maombi ya wateja wengi wanaosubiria umeme ikichukuliwa hii ni fursa pia kwa TANESCO kuongeza mapato ya shirika.

Mheshimiwa Spika, pamoja na vyanzo vya sasa, napendekeza Serikali itekeleze miradi ya vyanzo vingine kama vile vyanzo vya Jotoardhi, Umeme wa Jua, Upepo na Mkaa wa Mawe ili nchi yetu iendane na mahitaji makubwa ya umeme kwa hapa Tanzania na hata kuuza kwa nchi zingine za Afrika. Ni muda mrefu sasa, TANESCO kupitia Kampuni Tanzu ya Uendelezaji wa Jotoardhi nchini (TGDC) inaendelea na tafiti katika maeneo mbalimbali nchini kama vile eneo la Ziwa Ngozi lililoko Mkoani Mbeya ambapo ndipo yalipo makutano ya Bonde la Ufa la upande wa Mashariki na lile la Magharibi.

Napendekeza Serikali iharakishe utekelezaji wa miradi huu wa Jotoardhi na ule wa Mkaa wa Mawe wa Mchuchuma na Kiwira ili tuweza kuzalisha umeme zaidi kwa mahitaji ya ndani na nchi za nje.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.