Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati

Hon. Prof. Palamagamba John Aidan Mwaluko Kabudi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilosa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati

MHE. PROF. PALAMAGAMBA J. A. M. KABUDI: Mheshimiwa Spika, namshukuru Mwenyezi Mungu Rahim kwa ruzuku ya uhai na afya. Nichukue pia fursa hii kukushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika bajeti ya Wizara ya Nishati. Nami niungane na wale wote wanaokutakia kila lakheri katika azma yako ya kugombea nafasi ya Rais wa IPU. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninajua una hakika miongoni mwa watu ambao wanafuraha kubwa ya wewe kupanda katika nafasi hiyo ni mimi. Fahari ya Mwalimu yoyote yule ni kumuona mwanafunzi wake aliyemsomesha, aliyemlea anapanda na kupanda na kupanda zaidi. Kwa hiyo mimi ambaye nilipata bahati ya kuwa Mwalimu wako katika ngazi mbalimbali nakuombea kila la kheri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuipa kipaumbele na kuiwezesha sekta hii ya nishati kwa hali ya juu. Ila nimpongeze Mheshimiwa January Makamba, Waziri wa Nishati pamoja na Stephen Byabato, Naibu Waziri, Katibu Mkuu Eng. Mramba, Naibu Katibu Mkuu, Mbutuka kwa kazi nzuri mnayoifanya.

Mheshimiwa Spika, mchango wangu utakuwa katika maeneo matatu nikipata fursa. Kwanza ni Wilaya ya Kilosa, pili Mradi wa Julius Nyerere na tatu Umeme wa Joto Ardhi. Mradi wa REA ni muhimu sana kwa maendeleo ya nchi yetu na watu wake, na ndio mradi ambao unabadili hali ya maisha ya watu wetu vijijini. Na mimi nichukue nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais na Wizara ya Nishati kwa kutoa fedha zote kwenye Jimbo la Kilosa lenye kata 25 na vijiji 37 ambavyo havina umeme. Nishukuru sana kwa hilo.

Mheshimiwa Spika, tatizo kubwa tumepata mkandarasi ambaye utendaji wake wa kazi hauridhishi kabisa. Lakini katika hilo nikushukuru sana wewe mwenyewe Mheshimiwa Waziri, niwashukuru sana Mtendaji Mkuu wa REA Eng. Hassan Said, Meneja wa Mkoa wa Morogoro Mhandisi Fadhili Chilombe, Mameneja wa Kilosa, Meneja wa Mvomero na wale waratibu vijana wawili ambao sasa wamechukua hatua za kuhakikisha kwamba jambo hili sasa linashughulikiwa.

Mheshimiwa Spika, Mkandarasi amepewa deadline ya tarehe 30 Juni awe amepeleka umeme katika vijiji 20 asipofanya hivyo achukuliwe hatua. Mheshimiwa Waziri naomba msukumo wako mkandarasi huyu atekeleze mkataba. Amepewa fedha zote na kwa hiyo hana sababu ya kuendelea kusuasua; na kama hatafanya hivyo ifikapo tarehe 30 Juni basi hatua zichukuliwe. Hatuwezi kuendelea kuwa na mkandarasi ambaye ana fedha na hafanyi kazi.

Mheshimiwa Spika, baada ya hilo ya REA na ugoigoi wa mkandarasi nimeletewa simu leo kutoka Kijiji cha Matongolo – Dumila kwamba inaelekea transformer imezidiwa. Mimi naamini kabisa Meneja wa Mvomero ambaye ndiye anayesimamia huko atalichukulia hatua ili liweze kurekebishwa.

Mheshimiwa Spika, baada ya hayo nije kwenye Bwawa la Mradi wa Mwalimu Julius Nyerere. Huu ni mradi ambao Watanzania wote hatuna budi kuwa na fahari nao na kuuenzi sana. Ni mradi ambao aliuasisi Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere. Na mnapokuwa na mradi huo ambao umeanzishwa na muasisi wa Taifa lenu na akashindwa kuutekeleza ninyi ambao mnapata heshima ya kuukamilisha mnapata baraka nyingi sana za Mwenyezi Mungu. Kwa hiyo mimi ninahakika kabisa Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, wewe Waziri, watendaji wa TANESCO na wote waliohusika katika mradi huu Mwenyezi Mungu atawapa baraka kwa sababu mmetekeleza mradi ambao ulikuwa ndani ya moyo wa muasisi wa Taifa letu Mwalimu Julius Kambarage Nyerere. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kutekeleza mradi huu nchi yetu, TANESCO, wahandisi na wataalamu ewote wa Tanzania tumepata uzoefu na utaalamu wa kujenga kwa ufanisi zaidi miradi ijayo ya umeme wa maji kama vile Rumakali na Ruhuchi. Tajiriba hii tuliyoipata, tajiriba kwa kiingereza ni experience, tajiriba hii tuliyoipata kama nchi itatusaidia sana huko tuendako kuwa na muala katika kutekeleza miradi hii ya maendeleo na muhala maana yake ni coherence.

Mheshimiwa Spika, mradi huu una upekee wa aina yake na ni lazima tuuenzi kwa kadri tunavyoweza. Ukubwa wa bwawa hili kwa kweli ni ziwa, kwa sababu ni bwawa ambalo lina ukubwa wa kilomita za mraba 1,194.4 ni kubwa zaidi ya Ziwa Eyasi lenye kilomita za mraba 1,050 ni kubwa zaidi ya Ziwa Natroni lenye ukubwa wa kilomita za mraba 1,040 na ni kubwa zaidi Ziwa Manyara lenye kilomita za mraba 470. Kwa hiyo bwawa hili kwa kweli linatupa heshima ya Ziwa na Bwawa hili ni muhimu sana kama ambavyo alilifikiria Baba wa Taifa. Moja ni kuzalisha umeme lakini moja ilikuwa ni kudhibiti mafuriko ya Mto Rufiji. Na mimi naamini kabisa sasa tatizo la mafuriko ya Mto Rufiji yamekwisha, lakini pia bwawa hili litatusaidia katika kilimo, katika Utalii.

Mheshimiwa Spika, katika utalii nimeambiwa kwamba bwabwa hili baada ya kuwa limejaa katika ujazo wake litakuwa na visiwa visivyopungua sita litakuwa ni bwawa la aina yake Duniani lenye utalii pia wa visiwa ndani ya bwawa hilo. Nishukuru sana kwa juhudi kubwa zinazochukuliwa mpaka sasa katika mikoa yote kumi na wilaya 26 zenye mito inayopeleka maji katika bwawa hili. Ni vizuri kabisa tujue hilo hiyo mikoa 10 na wilaya 29 zenye mito inayopeleka maji katika bwawa hili zinawajibu mkubwa sana wa kutunza mito hiyo, vyanzo hivyo vya maji ili kuhakikisha maji yanaendelea kutiririka. Watu waendelee kuelimishwa katika maeneo hayo na wajue maji yanatoka sehemu nyingi. Maji yanayokwenda kwenye hili bwawa yanatoka Chunya, Sikonge, y Manyoni, Tunduru, Kilombero, Chamwino, Chemba, Songwe, Mbeya na Makete; na zaidi kabisa ni kutunza Wetland ya Kilombero bila Wetland ya Kilombero kutunzwa bwawa hili itapata shida.

Mheshimiwa Spika, mimi niombe kwa dhati kabisa Mheshimiwa Waziri January Makamba kwa kushirikiana na wenzako katika Ofisi ya Rais, Makamu wa Rais Mazingira, Wizara ya Maji, Wizara ya Maliasili na Utalii na Wizara ya TAMISEMI kuhamasisha watu wote katika mikoa hii kumi na Wilaya hizi 24 kujua wajibu mkubwa walio nao wa kutunza mito na vyanzo vya maji ili bwawa hili liendelee kwa manufaa yetu. Na tutakapoata hizi megawatt 2115 tutakuwa tumepata umeme mwingi wa kutuwezesha kuleta maendeleo makubwa.

Mheshimiwa Spika, bila umeme huwezi kuwa na viwanda, miundombinu na huwezi kufanya chochote. Ndiyo maana Mwasisi wa Soviet Union Vladimir Lenin alipochukua uongozi alipochukua uongozi wa Soviet Union kazi yake ya kwanza ilikuwa ni kupeleka umeme. Kazi ya kwanza aliyoifanya Kwame Nkrumah Ghana baada ya Ghana kupata uhuru ilikuwa ni kujenga Bwawa la Umeme la Akasombo ili aweze kuleta maendelo kwa Ghana. Kwa hiyo suala la bwawa hili ni suala muhimu sana. Kwa hiyo ningeomba Wizara zote na wadau wote na sisi Wabunge tuone fahari na bwawa hili lakini sasa tuongeze juhudi katika kutunza mazingira ili mradi yaweze kwenda katika bwawa.

Mheshimiwa Spika, hatua tuliyofika kwa Mheshimiwa January Makamba sasa ni sawasawa na pilot ambaye ametangaza ndege kutua. Tunaitakia ndege hiyo itue salama na kama kutakuwa na landing turbulences basi pilot ashike usukani ndege itue salama.

Mheshimiwa Spika, jambo jingine ambalo ningependa kulichangia ni hili la umeme wa joto ardhi. Katika maonesho haya nimepata elimu kubwa sana kuhusu joto ardhi. Na mimi naomba Wizara, Mheshimiwa January Makamba, jambo hili ambalo mmelianza sasa na mtakalolianzia kule Ngozi na yale maeneo mengine manne mliongeze juhudi kubwa sana. Kama tu pale Ngozi kwa awamu ya kwanza tutapata megawatt 70. Megawatt 70 si umeme mchache tunaamini katika maeneo mengine 52 tutafanikiwa kupata umeme mwingi zaidi.

Mheshimiwa Spika, Kenya sasa wanazalisha megawatt 1000 kutokana na joto ardhi, sisi kwa vyanzo vyote tulivyonavyo tutapata umeme mwingi sana naomba kuunga mkono hoja na kwa asilimia zote.

Mheshimiwa Spika, kila lakheri katika mbio zako za unakoelekea. (Makofi)