Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati

Hon. Timotheo Paul Mnzava

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Korogwe Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili nami nitoe mchango kwenye bajeti hii ya Wizara ya Nishati. Nianze kwa kuungana na wenzangu waliotangulia kusema kukutakie kila la heri katika jambo hili kubwa na zuri ambalo liko mbele yako. Tuko pamoja na wewe na tunakuombea heri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, watendaji wa Wizara hii na taasisi zao zote. Sisi sote ni mashahidi wa kazi kubwa na nzuri wanayoifanya. Miaka kadhaa nyuma iliyopita tulikuwa tukikutana kwenye Bunge hili kujadili Bajeti ya Wizara ya Nishati tulikuwa tunatumia muda mwingi kwenye eneo la REA, lakini leo kuanzia kwenye hotuba ya Waziri, taarifa ya Kamati lakini hata Michango ya Wabunge inatambua kazi kubwa na nzuri inayofanywa kwenye uzalishaji wa umeme kwenye maeneo mengine na kwenye vyanzo vingine. Leo tutazungumzia gesi, umeme wa upepo, umeme wa jua na vyanzo vingine mbalimbali. Niwapongeze Wizara kwa maono hayo ni jambo zuri tunaliunga mkono endeleeni nalo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nina mchango kwenye maeneo mawili. Eneo la kwanza ni eneo la usambazaji wa umeme vijijini lakini eneo la pili nitazungumza kidogo kuhusu gesi.

Mheshimiwa Spika, kama kuna miradi ambayo imesaidia kuipa heshima Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwenye nchi hii ni pamoja na mradi wa kusambaza umeme vijijini. Wananchi wamefurahi ni mradi unaogusa maisha yao moja kwa moja, ni mradi unaokwenda kubnadilisha maisha ya watu wetu kule vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa kwenye eneo hili mimi nilitaka nizungumze tu kuhusu Jimbo la Korogwe Vijijini. Sisi Korogwe vijijini tuna vijiji 118, vijiji 54 havijapata umeme kabisa. Tulikubaliana kwamba vijiji hivi vitapata umeme kupitia mradi wa REA awamu ya tatu mzunguko wa pili. Kwa bahati mbaya sana baada ya zoezi kufanyika na kutafuta wakandarasi kuna lots tano ambazo zilikosa wakandarasi ikiwemo lot moja ambayo ilikuwa ina Wilaya za Korogwe, Mkinga pamoja na Pangani. Tukachelewa kwa muda mrefu lakini baadae wizara, Serikali na REA wakatusaidia tukapata mkandarasi na tukaamini kwamba kazi ya kupeleka umeme kwenye vijiji inakwenda kuanza kwa kasi na wananchi wetu wapate umeme.

Mheshimiwa Spika, kwa bahati mbaya sana tukapata mkandarasi ambaye kwa kweli uwezo wake ulikuwa si wa kurudhisha na hivyo hajaifanya kazi hii Vizuri. Kipekee nishukuru sana Kamati yetu ya Bunge ya Nishati na Madini kwa kutembelea eneo la Korogwe kama eneo la kujifunza. Walipofika Korogwe waliona kazi aliyoifanya mkandarasi yule. Katika vijiji 54 mpaka Kamati inakwenda ilikwenda kuwasha umeme kwenye vijiji viwili na vijiji vilivyokuwa vinakaribia kuwa tayari na maeneo mengine yote kulikuwa hakuna kazi iliyofanyika. Jambo hili lilitusikitisha sana na limewaumiza sana watu wa Koropgwe na limewachelewesha watu wa Korogwe kupata huduma ya umeme

Mheshimiwa Spika, lakini nimshukuru Mheshimiwa Waziri, baada ya Kamati kutoka tumekaa vikao kwa maelekezo yake Mheshimiwa Waziri na kwa usimamizi wake kwa kweli tumeanza kuona ile speed ya yule mkandarasi imeanza kubadilika. Katika vijiji 54, vijiji sita tayari tumekwishawasha umeme, vijiji viwili wanasubiri ratiba ya Mbunge tukawashe umeme kwa wananchi na kuna vijiji 21 tayari nguzo zimekwisha simikwa na kazi inaendelea. Pia yako makubaliano ambayo tumekubaliana na mkandarasi huyo chini ya REA na ninyi wenzetu wa Wizara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninachoomba niwashauri kwenye eneo hili la REA katika maeneo matatu.

Mheshimiwa Spika, ushauri wa kwanza, makubaliano tuliyokubaliana kwenye vikao vyetu na yule mkandarasi ayatimize, na ayatimize kwa kasi; na tukiona hayaendi kama tulivyokubaliana tunaomba msisite kuchukua hatua nyingine za kisheria ili kazi zikamilike na wananchi wa Korogwe waweze kupata umeme.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, tumesema kuhusu vitongoji. Mimi Korogwe tuna vitongoji 610. Kwenye hotuba yako Mheshimiwa Waziri kwenye ukurasa wa 36 umesema vizuri kwamba tunahitaji shilingi trilioni 6.7 ili kukamilisha kazi ya kupeleka umeme kwenye vitongoji vyote ambavyo havina umeme. Fedha hii ni nyingi sana, na wewe mwenyewe umesema tukienda kwa utaratibu wa kawaida tunaweza kuchukua miaka 20. Hata hivyo, kwenye kitabu chako umetuahidi kwamba mnakamilisha mpango wa kupeleka umeme kwenye vitongoji hivi angalau ndani ya miaka mitano kazi iwe imekamilika.

Mheshimiwa Spika, ninamwomba Mheshimiwa Waziri kazi hiyo waifanye kwa kasi. Kuna vijiji ambavyo vina vitongoji vikubwa na vina hadhi hata ya kuwa vijiji havijapata umeme. Kama shida ni fedha kaeni Serikalini huko wekeni utaratibu na ifanyeni hii kama mradi kama ilivyo miradi mingine. Kama tulivyo na mradi wa kupeleka vijijini tuwe pia na mradi wa kupeleka umeme kwenye vitongoji vipate umeme tuwe tumemalizana na jambo la umeme kwenye vijiji na kwenye upande wa vitongoji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la tatu ambalo nilitaka nimshauri Mheshimiwa Waziri na wizara na hili kwa kiasi mmeanza kulifanyia kazi ni hii namna ya kupata wakandarasi. Utaratibu uliozoeleka na ambao umekuwa ukitumika mkandarasi anapatikana kwa njia ya ushindani. Mnazingatia vigezo vya kifedha na vigezo vya kitaalamu kwa maana ya vigezo vya kiufundi. Huo ndio utaratibu ambao umekuwa ukitumika muda mrefu na kiukweli ndio ambao umehusika kutuchelewesha kufika hapa tulipofika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimpongeze Mheshimiwa Waziri, tumeona maelekezo yako kwa REA kwamba vigezo hivi viwili visiwe vigezo pekee vya mkandarasi kupata kazi ya kupeleka umeme vijijini. Pamoja na kuangalia uwezo wa kifedha, uwezo wa kitaaluma na uwezo wa kiufundi umewambia REA waangalie historia ya Mkandarasi, utendaji kazi wake kwenye miradi mingine ambayo tayari alishaifanya huko nyima au ambayo anaendelea kuifanya. Ninashukuru nimesikia angalau REA wamesema kwa saa ili mkandarasi apewe kazi nyingine au mpya afike angalau asilimia 60 au 80. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninachoomba jambo hili lisiwe maneno likasimamiwe vizuri ili litusaidie kuendelea kupata wakandarasi wazuri ambao watafanya kazi vizuri ya kupeleka umeme kwenye maeneo ya vijiji vyetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la pili ambalo nilitaka kulichangia kidogo ni eneo la gesi. kipekee tumshukuru na kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kukubali na kufufua tena ndoto za watanzania kufanya kazi ya utafutaji na uza.ishaji wa gesi ndani ya nchi yetu. Manufaa ya gesi ni makubwa, tangu Mheshimiwa Rais alipoamua mwaka 2022, nchi yetu sasa imeanza kukaribia kuingia kwenye ramani na kwenye nchi za uchumi wa gesi na mafuta. Tunampongeza sana Mhe shimiwa Rais kwa jambo hili kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi niseme, jambo hili limesemwa vizuri na hata kwenye hotuba Mheshimiwa Waziri amelieleza vizuri. Halikufikia maamuzi haya kwa bahati mbaya jambo hili ni la muhimu sana na lina sababu. Sababu ya kwanza ni Mheshimiwa Rais mwenyewe kutengeneza mazingira wezeshi na mazingira rafiki ya uwekezaji kwenye nchi hii hasa kwenye eneo la gesi, tunampongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini jambo la pili, jambo la gesi halikwepeki. Duniani sasa hivi gesi ni sekta inayokua kwa kasi. Sekta ya gesi inakuwa kwa zaidi ya asilimia 7.5 kwa mwaka sio jambo la kudharau. Vile vile, mahitaji ya gesi yamekuwa ni makubwa sana. Hata hivyo, kwa tafiti na taarifa tulizonazo tuna gesi za kutosha lakini pia tuna faida ya jiografia yetu. hapa tulipo ni rahisi kutoa gesi hapa kwa urahisi zaidi na kuipeleka maeneo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninachoomba nishauri mambo mawili kwenye eno hili la gesi. kwanza, Mheshimiwa Waziri umesema kwenye hotuba yako ukurasa wa 50 kwamba mnaelekea kukamilisha kazi kudurusu mkataba kifani. Niwaombe sana jambo hili lifanyike kwa haraka ni jambo muhimu. Mkataba huu utatusaidia kutuwekea uwazi wa sisi tunafaidika nini? Nini wanafaidika wenzetu lakini pia itatuondolea uwezekano wa yeyote anayekuja kwenye Serikali au kwenye nafasi za Serikali kuamua anachokitaka kwa sababu tayari mkataba huu unao mwongozo wa kunufaika na mapato haya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini jambo la pili nataka nishauri. Ukisikiliza michango humu ndani, ukamsikiliza Mheshimiwa Waziri, ukawasikiliza watendaji wa Wizara kuhusu jambo la gesi linasemwa kwa matarajio makubwa na faida kubwa na watu wana matumaini makubwa. Vile vile, gesi hii kuna hatua. Niwaombe jambo moja tu la muhimu sana, jiandaeni kama Serikali kufanya expectation management. Watu huko wanajua matrilioni, mabilioni yanakuja lazima wajue kuna hatua za kwenda, kuna hatua za kufuatwa mpaka uchimbaji unaanza na kunufaika moja kwa moja kunaonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo nakushukuru sana na naunga mkono hoja.