Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati

Hon. Nicodemas Henry Maganga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia kwenye hii sekta ya nishati.

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu Muumba wa Mbingu na Nchi kwa kupata nafasi hii adhimu ya kuweza kuzungumza na watanzania wote kupitia Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Spika, nimshukuru Mama yetu, Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Sita kwa kazi anazoendelea kuzifanya hapa nchini ikiwemo kupambana na miradi hii mikubwa iliyoachwa na mtangulizi wake. Kweli shukrani za dhati, wananchi wangu wamenituma nije ni mshukuru. Walifurahia sana walipomwona anazindua Ikulu maana ilikuwa kama vile ndoto, kwamba Ikulu ya Dodoma imekamilika tena kwa kiwango cha juu kushinda hata ile ya zamani. Kwa kweli Mheshimiwa Rais ubarikiwe sana. Pili nikushukuru wewe Mheshimiwa Spika kwa jinsi unavyotuendesha kwenye Bunge hili Tukufu. Na sisi maombi yetu tu, kwa niaba ya Machifu wa Kisukuma tunakuombea kwa Mwenyezi Mungu ili kusudi uweze kukamilisha dhima yako uliyokusudia. Na kwa niaba ya Watumishi wa Mwenyezi Mungu, kwa maana ya Makanisa yote Wakristo na Waislamu wamenituma kukwambia usome Zaburi 23:1 nakuendelea. Maneno haya yakutie ngunvu katika safari yako ya mapambano. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa nije kwenye hii sekta ya nishati na nianze na hii miradi ya REA. kwanza, nikiri wazi kwamba mimi ni mjumbe wa Kamati, na nikuombe Mheshimiwa Waziri, ushauri tuliokupa kama Kamati uuzingatie na uufanyie kazi sana maana umesomwa vizuri na Mwenyekiti wetu Mheshimiwa Kitandula pamoja na wajumbe ambao huwa tunakuwa wa wewe kwa pamoja, huwa tunakupa ushauri mzuri sana na ukiufuata utakuwa ni Waziri wa kiwango ambae utaacha historia kubwa hapa Tanzania kwenye hiyo sekta. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri, hii sekta yako ina changamoto nyingi na inafahamika katika historia ndio sekta ambayo huwa ni ngumu katika Wizara zote hapa nchini. Hata hivyo, nianze kwa kukushurukuru jinsi unavyonipa support kwenye Jimbo langu maana toka niingie madarakani nilikuwa nina vijiji 34 na kwa sasa bado vijiji 18 ambavyo bado havijapata umeme; naomba nivitaje. Kuna Kijiji cha Nyashinge, Kagongo, Isungabula hiki ni Kijiji kimoja kikubwa sana na huwa kinanipa shida sana ninapoenda pale. Mheshimiwa Waziri, kwa hiyo nikuombe wewe kwa vile mkandarasi yuko chini yako utoe msukumo, pale utakapofanya majumuisho mkandarasi huyu wa Geita afanye faster hapo Isungabula ili wawahi kulala peupe. Pia, kuna kijiji cha Bwendaseko, Kiseke, Nyashinge, Mgerere, Igalura, Burongo, Bushetu, Bukwimba, hiki ni kitongoji kikubwa, kimeamua kupewa Kijiji, na ndipo nilipozaliwa hapo. Pia, kuna Baguta, Kabanga, Buruhe, Ruhala, Mwagimagi, Mponda, Nhungwiza pale niliposoma Shule ya Msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri, napenda nikwambie akupendaye lazima atakushauri kwenye Bunge kama hili. Mimi nakupenda sana kwa kweli Mheshimiwa Waziri; lakini kama nilivyotangulia kusema mwanzoni, sekta hii ni kubwa, unaongoza watu wenye akili, maprofesa, lakini hivyo wengine nia zao sio nzuri sana. Ninakuombea sana kwa Mwenyezi Mungu akupe ujasiri wa kutokusita kuchukua maamuzi pale unapoona mambo hayaendi vizuri. Nimeiona bajeti hii ina trilioni 3.48, kwa hali ya kawaida unaweza ukasema ni pesa nyingi lakini ni chache. Kwa kuwa mimi ni mjumbe wa Kamati na changamoto za sekta hii nazijua vizuri, bajeti hii ilitakiwa iende hata trilioni tano kwa jinsi mahitaji yalivyo hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu tukiangalia kwenye upande tu wa mafuta umetenga bajeti ili kusudi kuwasaidia vijana wanaojishughulisha na uuzaji wa mafuta holela mitaani. Kwanza, nipende kuwapa pole sana wenzangu kwa sababu na mimi ni zao ambalo linalotokana na kuuza mafuta huko mitaani. Niwape pole sana watu wangu wa Masumbwe ambapo tarehe 29 nyumba iliwaka kufuatia kuweka mafuta ya petrol ndani. Mheshimiwa DC wangu alishughulika vizuri sana, pamoja na Jeshi la Poliisi japokuwa hatukuwa hata na kizima moto, mchanga ulitusaidia na Mungu alismama na sisi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niwape pole pia wale waliounguliwa na vitanda vyao kwenye Mtaa huu wa Masumbwe Shinyanga B Mungu awasaidie. Kwa sababu hasara hii imetokea, na hata huyu mfanyabiashara yeye hakupanga kwamba nyumba hiyo iungue. Kwa hiyo, Mungu awasaidie muweze kupata mitaji mingine maisha yaendelee. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia nimpe pole mfanyabiashara mmoja tarehe 23 aliunguza nyumba yake kwa shoti ya umeme. Mheshimiwa Waziri hii nayo ni changamoto nikuombe wasiliana na Waziri mwenzako wa Mambo ya ndani ikiwezekana kila mnakopeleka umeme huko mtaani kuwepo na vifaa vya kuweza kuzima shoti za umeme pale zinapotokea. Ni kweli huduma hii ni nzuri lakini pale inapotokea shoti inakuwa ni majuto kwamba ni kwanini niliunganishiwa umeme huu. Mimi nimeyaona kwa macho nyumba za watu zinavyotekekea kwa shoti za umeme. Kwa hiyo, Serikali ilifikirie. Na kwa kuwa hapa nazungumza na Serikali yote mpo, mlifikirie hasa pale mnapowaunganishia umeme wananchi wa vijijini mkumbuke je, ikitokea shoti watazima na nini katika nyumba zao?

Mheshimiwa Spika, kwa mfano mji wa Masumbwe ni mkubwa na hatuna gari la zima moto japokuwa hoja hii nilitakiwa niiwasilishe Mambo ya ndani. Hata hivyo, kwa kuwa wewe Mheshimiwa Waziri uko makini unaweza ukaongea na ndugu yetu ili aweze kutusaidia ili nyimba hizi zinapopigwa shoti ya umeme ziweze kuzimwa kwa haraka.

Mheshimiwa Spika, naomba nitoke jimboni nishauri jambo lingine la kitaifa. Hapa nchini tuna changamoto ya upandaji wa mafuta, na hili mimi nakuomba Mheshimiwa Waziri kwa vile una uwezo mkubwa ukae na wataalamu wako uangalie ni jinsi gani mnamsaidia Mheshimiwa Rais. Kwa sababu sio kawaida Watanzania kununua bei za 3000/3000. Kwa sababu tusiseme maisha tumeyaweza sana, kero zilizoko mtaani nikubwa.

Mheshimiwa Spika, tuna bandari yetu, jinsi gani tunakwenda kuwasaidia wanyonge ili kusudi bei za mafuta na nauli zishuke bei; kwa sababu mafuta yakishuka bei ina maana na vitu vyote vitashuka bei, mabati yatashuka bei na kila kitu kitashuka bei. Kwa uwezo wako uliopewa na Mwenyezi Mungu kaa na wataalamu wako muangalie. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mfano nchi ya Kenya tumesikia sasa hivi wao wanaagiza mafuta kwa fedha zao za Kenya. Kama Kenya inawezekana kwa nini sisi Tanzania ishindikane kuagiza mafuta kwa fedha zetu? Vile vile, uagizaji wa mafuta zile Sheria zilizopo ni ngumu. Tuachieni Machinga tufuate mafuta wenyewe nje ya nchi ili kusudi muone bei zitakavyoporomoka ili Watanzania waweze kuishi maisha wanayoyataka.

Mheshimiwa Spika, Watanzania wana imani kubwa na Chama cha Mapinduzi lakini pale maisha yanapoonekana kuwa magumu halafu tukawa kama vile hatuwajali inaonekana kama tumewasahau. Mkumbuke Sera yetu ni kuwasaidia wanyonge. Sasa wanyonge hawa bei za nauli zinapopanda wanashindwa kuelewa kwamba Serikali hii ilitutangazia kutusaidia ama kutukomoa? Kwa hiyo, nikuombe Kaka yangu January kaa na wataalamu wako pamoja na bodi inayohusika kupanga wale waingizaji wa mafuta Sheria hizo zifutwe na watu tuingize mafuta kwa uwezo wetu ili kusudi tuweze kuilinda nchi yetu na kuweza kuileta manufaa mazuri ili watu waishi kwenye maisha mazuri ya kupendeza.

Mheshimiwa Spika, suala lingine, Mheshimiwa Waziri nizidi kukushukuru tu, lakini pale Masumbwe zile transformer zilishazidiwa. Transformer zilizopo Wilaya ya Mbongwe zilikwisha zidiwa, maana kipindi umeme unapita nyumba zilizokuwa zinaunganishawa zilikuwa chache. Hivi sasa kuna viwanda vya mchele kwa hiyo, pale wanapowasha mashine hizi za kukoboa mchele umeme unazima. Utufikirie kutuongezea transformer nyingine kupitia bajeti yako hii ya Trilioni 3.4. kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri nikuombe sana na ukipata nafasi utembelee kwenye jimbo langu ili kusudi uje u–solve matatizo yangu. Kwa sababu wewe ni rafiki yangu na urafiki mzuri ni ule wa kujaliana wakati wa shida sio kusubiriana tu huku kwenye raha. Kwa hiyo, nakukariobisha sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda nimshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa vile na yeye ni Mbunge mwenzangu kila mara huwa anapita. Naibu Waziri, nikuombe mji wa Masumbwe usipopita kwenye chocho ni lazima wewe uukanyage ili ufike Bukoba. Siku moja utenge nafasi uweze kuzungumza na wafanyakazi wa TANESCO, hawana magari, hawana vitendea kazi vijana hawa wanasumbuka sana kufanya kazi...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana kengele ya pili imeshagonga.

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana ahsante. Nitaleta mchango wangu wa maandishi kwa yale niliyoacha.