Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati

Hon. Innocent Edward Kalogeris

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati

MHE. INNOCENT E. KALOGERIS: Mheshimiwa Spika, ahsante sana na mimi kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja ambayo iko mbele yetu.

Mheshimiwa Spika, na mimi nitumie nafasi hii vilevile kwanza kukupongeza kwa uthubutu kwa jambo ambalo liko ndani ya moyo wako na uhitaji wako. Kubwa zaidi, sisi kama Wabunge wenzako tuko nyuma yako na tunaendelea kukuombea Mungu katika dini mbalimbali Mwenyezi Mungu aweze kukamilisha hiyo azma na Taifa liendelee kung’ara kupitia wewe.

Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mama yetu Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kutoa fedha katika maeneo mbalimbali. Sisi Wabunge ni mashuhuda, tangu tumeanza kupitisha bajeti hapa za Wizara mbalimbali, kila Wizara iliyopitishwa kuna mambo makubwa yamefanyika.

Mheshimiwa Spika, na katika hili, hata katika Wizara ya Nishati kuna mambo makubwa; trilioni tatu na pointi si jambo dogo, ni jambo kubwa ambalo linahitaji uthubutu mkubwa, na Mheshimiwa Rais amefanya. Sasa hivi kazi kuwa iko kwa ndugu yangu tu, Mheshimiwa January, kuhakikisha kwamba fedha hii inayokuja ikafanye yale matokeo ambayo yanatakiwa kwa Watanzania.

Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii vilevile kukupongeza Mheshimiwa Waziri, Niabu Waziri, management ya Wizara na watendaji kupitia taasisi zote; REA, TANESCO, EWURA na kwingineko, kwa kazi kubwa ambayo mnaifanya, lakini kwa bajeti ambayo imekuja mbele ya Bunge hili.

Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii vilevile kutoa pongezi kwa Meneja wangu wa TANESCO Mkoa wa Morogoo, Eng. Fadhili pamoja na Meneja wa TANESCO wa Wilaya ya Morogoro, kwa kazi kubwa wanayoifanya.

Mheshimiwa Spika, vilevile pongezi hizi ziende kwa Mkandarasi makini Stagic International Services ambaye ndiye amefanya kazi kubwa ya kupeleka umeme wa REA katika Halmashauri ya Morogoro. Alipewa vijiji 84, tunavyozungumza sasa hivi vijiji vyote 84 vinawaka; tuna kila sababu ya kupongeza katika hili.

Mheshimiwa Spika, kubwa zaidi, nimwombe Mheshimiwa Waziri, bado kuna vijiji vitano ambavyo havikuwepo katika ule mkataba, mkandarasi ameongezewa, tayari ameshakwenda site, anachosubiri nadhani ni kuanza kazi. Niombe, katika zile kilometa mbili mbili ambazo tumeongezewa, nikuombe mfanye kwa haraka – mkandarasi huyu yuko idle – apewe hiyo kazi afanye ili tumalize, kama vile ilani ilivyosema; mpaka kufikia 2023 tukamilishie vijiji vyote nchini. Kwetu sisi Morogoro tunaamini tutakuwa tumekamilisha; nikupongeze sana.

Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii vilevile kukuomba, katika suala la kwenda kwenye vitongoji. Bado tuna changamoto kubwa, vitongoji ni vingi. Tunakushukuru kwa hivyo 15 lakini nikuombe, angalia uwezekano mwingine wa kuhakikisha kwamba umeme unawafikia Watanzania.

Mheshimiwa Spika, Watanzania wana hamu kubwa ya umeme, na umeme ni nishati kubwa sana yenye uhitaji mkubwa kwa Tanzania. Nikuombe tu Mheshimiwa Waziri, angalia namna gani – tunakushukuru kwa hivyo 15 kwa sababu tuna kila sababu ya kuanza kushukuru kwa kile tulichopata – lakini tunahitaji vingine utusaidie.

Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii kumwomba Mheshimiwa Waziri, Mkoa wa Morogoro ni mkoa wa kimkakati. Kuna uhitaji mkubwa katika TANESCO wa magari na watumishi. Naomba wasaidieni watumishi wa TANESCO Mkoa wa Morogoro wapate magari mapya ili waweze kufanya kazi.

Mheshimiwa Spika, kuna vyanzo vikubwa vitatu vya Kihansi, Kidatu lakini tunakwenda kwenye Bwawa la Mwalimu Nyerere. Lakini mkoa ni mkubwa, wana uhitaji mkubwa wa watumishi pamoja na vitendea kazi. Nikuombe unapokuja ku-wind up uone jinsi gani ya kuwasaidia.

Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii vilevile kumwomba ndugu yangu, Mheshimiwa January, kwenye hili suala la vinasaba, hebu tuliache lilipotulia, tusianze mambo mengine mapya. Ninachojua nyuma kulikuwa na changamoto nyingi, lakini tulipoingia kwenye TBS changamoto zilizokuwepo tunahitaji Serikali kuisaidia TBS. TBS ni kampuni ya Serikali, ina utaalamu mkubwa, inafanya mambo makubwa katika nchi. Kwa hiyo nikuombe libakie hapohapo, hatutaki kwenda kwingine. Kwa sababu tukienda kwingine tunaanza kwenda kufukua makaburi ambayo hayana sababu.

Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii kupongeza jitihada za dhati za Mheshimiwa Rais anazozifanya katika kuendeleza Bwawa la Mwalimu Nyerere. Bwawa hili Mheshimiwa Rais alipolichukua lilikuwa kwenye wastani wa asilimia 30/32. Lakini leo tunapozungumza mpaka kufikia Aprili tumefikia almost asilimia 88; tuna kila sababu ya kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa hii anayoifanya.

Mheshimiwa Spika, ombi langu kwa Wizara, na hasa kwako ndugu yangu, Mheshimiwa January; ndani ya mradi ule kuna kitu kinaitwa CSR ambayo tangu mradi umeanza mpaka unafikia asilimia hiyo, hakuna fedha yoyote iliyokwenda katika Halmashauri ya Morogoro Vijijini au Halmashauri ya Rufiji. Nikuombe, katika Bunge lililopita ambalo tulikuwa tunapitisha mpango wa bajeti kulikuwa kunasemekana fedha ile inatakiwa ipelekwe Tanga, fedha ile inatakiwa ipelekwe Dodoma, Kigoma na Lindi. Nikuombe, fedha ile ni ya watu wa Morogoro, ni haki ya watu wa Morogoro, tunaitaka watu wa Morogoro, tuna shida nyingi Wanamorogoro ambazo kupitia fedha hii tunaamini tutaweza kuzitatua au kusaidia Serikali kufikia katika yale maendeleo tunayoyataka.

Mheshimiwa Spika, sasa kama suala ni kujenga chuo hicho cha TEHAMA ambacho mnadhani wataalamu mnakihitaji kijengwe Morogoro au kijengwe Pwani kwa sababu tuna maeneo makubwa ya kuweza kufanya jambo hilo. Lakini vilevile Morogoro juzi tuliambiwa kupitia TAMISEMI kwamba tupeleke mahitaji yetu kwenye suala la afya; tumefanya. Na hapo TAMISEMI, tunaomba yaheshimiwe.

Mheshimiwa Spika, lakini bado kuna suala la elimu, kwa sababu katika mradi huu fedha ya CSR zinakwenda kwenye elimu, zinakwenda kwenye afya. Morogoro kama Morogoro kiwilaya ina halmashauri mbili, wenzetu mjini wana VETA, sisi Halmashauri ya Morogoro Vijijini hatuna VETA; tunahitaji VETA. Tunahitaji High School, tunahitaji mabweni kutokana na jiografia ambayo tunaishi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nikuombe, Waziri anapokuja ku-wind up aje na jambo la kutueleza Wana-Morogoro na Wanapwani. Najua jambo hili Mheshimiwa Mchengerwa hawezi kulisema, yuko kwenye Cabinet; je, tufanye nini kupata haki zetu sisi ambazo ni haki ya Kikatiba na ya kimkataba?

Mheshimiwa Spika, mara ya kwanza mlipeleka Dodoma kujenga uwanja, mkabdarasi kakataa kwa sababu anajua CSR ile ni ya Morogoro na Pwani. Sasa hivi kama mtapeleka huko maana yake tunazidi kuchelewesha fedha ile, mnazidi kuchelewesha maendeleo kwa Morogoro na kwa Pwani.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nikuombe sana, najua wewe ni kijana makini, na bahati nzuri umekulia Morogoro, unaijua Morogoro, unajua shida za Wana-Morogoro, nakuomba simama kuhakikisha kwamba haki ya Wana-Morogoro na Pwani ya CSR inabaki katika maeneo husika.

Mheshimiwa Spika, sitaki kusema maneno mengi, najua Mheshimiwa January ni mchapakazi, anajua kazi. Sasa nakuomba tu utakapokuja, sitaki kushika shilingi yako lakini nataka tu unipe majibu hayo na jioni baadaye mimi ni profesa unajua, nataka tukutane baadaye ili nikupe furaha na wewe ukafurahi baada ya bajeti.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru; naunga mkono hoja. (Makofi)