Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati

Hon. Maimuna Salum Mtanda

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Newala Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati

MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipatia fursa hii. Awali ya yote namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipatia afya. Kipekee nimshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa ambayo ameendelea kuifanya. Na katika Wizara hii amefanya mengi sana makubwa ambayo mengine yanaendelea kukamilika na mengine yanaanza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii kipekee kukutakia heri sana wewe binafsi kwa ule mchakato ambao uko mbele yako, na Insha Allah Mwenyezi Mungu ataleta heri, kwa sababu Waswahili wanasema iliyonona inaanzia miguuni; huku Tanzania umenona, hongera. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimpongeze Waziri mwenye dhamana aliyewasilisha hotuba yake pamoja na viongozi wake wote wanaomsaidia kazi; hongereni sana, hotuba ni nzuri.

Mheshimiwa Spika, nina mchango katika maeneo machache. Mchango wangu wa kwanza unakwenda kwenye suala la kukatika katika kwa umeme katika maeneo mbalimbali ya nchi yetu. Niishauri Wizara kutafuta namna nzuri ambayo tatizo hili la kukatika katika kwa umeme litakwenda kukomeshwa kwa sababu linaathiri kwa kiasi kikubwa sana uchumi wa nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, katika hilo, hata kwenye Mkoa wa Mtwara suala la kukatika katika kwa umeme limekuwa sasa kama ni la kawaida. Lakini kipekee niendelee kumpongeza Mheshimiwa Waziri, amekuwa msikivu, juzi tulikaa naye kikao yeye pamoja na wataalamu wake wote kwa saa zaidi ya mbili kwenye jando – maana lile tunaliita jando, na mambo ya jandoni hayasemwi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimwombe Mheshimiwa Waziri pamoja na timu yake, yale ambayo tumejadiliana yanayowenda kutekelezwa kwenye Mkoa wa Mtwara ili ku-rescue hali ya kukatika katika kwa umeme basi mkayasimamie. Na nishukuru kwamba zoezi lile nimesikia wameshaanza na kuna wengine wameniambia wanaondoka kesho wanakwenda kukaa huko wiki nzima. Kwa hiyo Mheshimiwa Waziri kilichobakia ni usimamizi wa yale ambayo tumekubaliana ili suala la kukatika katika kwa umeme na kuunguza vifaa vya watu liende likapotee. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hapa ninapoongea ukienda Mkoa wa Mtwara sasa kumedorora kwa sababu wafanyabiashara wengi vifaa vyao vimeharibika kutokana na tatizo hilo la kukatika katika kwa umeme, uwekezaji hakuna na watu wana hofu hiyo. Kwa hiyo yale ambayo mnakwenda kuyatenda, ikiwemo pia na kupeleka grid ya Taifa kwenye Mkoa wa Mtwara ikitokea Tunduru – Masasi kwenda Mahumbika, ni jambo ambalo litakwenda kuleta urahisi wa upatikanaji wa umeme katika Mkoa wa Mtwara ili sasa uwekezaji na uchangamfu wa mkoa, kwa maana ya kiuchumi, uende ukatekelezwe. Kwa hiyo nawatakia kila la heri katika usimamizi wa hilo ili Taifa liendelee na wananchi wapate uchumi wao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo nataka kuliongelea ni suala la REA. Niwaombe Wizara, wenzetu wa afya wana model, ukienda kwenye hospitali zao kubwa wametenga, wale wagonjwa mahututi wana namna yao ya kuwatibu na wagonjwa wengine wa kawaida wana namna ya kuwatibu. Sisi Mtwara kwa suala la REA tuko mahututi. Kwa hiyo niombee treatment ya Mtwara kwenye suala la REA ichukuliwe kama special case, ikasimamiwe. Tukiwasimamia wakandarasi hali ya upatikanaji wa umeme nadhani itakwenda kuwa nzuri.

Mheshimiwa Spika, nitolee mfano tu wa Jimbo la Newala Vijijini. Kwenye huu Mradi wa REA III Round Two, kulikuwa na vijiji 76. Kati ya vijiji 107 vya Newala Vijijini, vijiji 76 ndivyo vimlivyoingia kwenye mkataba na mkandarasi ambaye yuko site. Na mkataba ule ulikuwa ni wa August, 2021. Mpaka sasa status ilivyo vijiji 17 tu ndivyo ambavyo vimepata umeme, vijiji 17 viko kwenye process, vijiji 42 bado hawajafikiwa; na deadline ya mradi huu ni December mwaka huu. Sasa naona kama mzigo uliobakia ni mkubwa sana. Tusipowasimamia hawa watu watatuangusha, vijiji vile hawatapata umeme, tutapinduka 2024 bila ya kuwa na umeme. Niombe sana Wizara ikawasimamie.

Mheshimiwa Spika, sasa hivi wana suala wanasema wanaomba LC kutoka Serikalini, wapeni LC isije ikawa ndiyo kisingizio chao. Wapeni na wasimamieni kwa sababu nilicho-study kwa muda mrefu wa mkandarasi wetu ni kwamba anakosa usimamizi ule wa karibu. Kwenye mchezo wa mpira tunasema man to man – twende tukafanye man to man kwenye huu Mradi wa REA kule Newala Vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, athari ya kutokuwa na umeme ni kubwa sana. ukienda leo tunazo shule za sekondari kwenye Jimbo la Newala Vijijini, lakini wanajifunzaje TEHAMA kama hawana umeme? Kwa hiyo wale watoto watamaliza bila ya kuwa na knowledge ya TEHAMA kwa sababu tu ya ukosefu wa umeme, lakini huku tumeshawapatayari miradi wakandarasi. Kwa hiyo ili tuokoe kizazi hiki cha watoto ambacho ni cha kidijitali, lazima umeme ukafike shuleni. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili, Wizara ya Elimu imetenga fedha na imeendelea kuboresha miundombinu ya VETA Kitangali. Tumetangaza kwenye Ilani ya Chama Cha Mapinduzi kwamba tutaoa ajira zaidi ya 8,000 ifikapo 2025. Ajira hizi zinatoka kwenye sekta iliyo rasmi na isiyo rasmi. Mategemeo yetu ni wale wanaotoka VETA wakajiajiri kwenye sekta zisizokuwa rasmi. Watoto wale wanajifunza useremala, uchomeleaji na mapishi mbalimbali; vyote hivyo vinategemea umeme. Leo hii wanamaliza hawana kwa kwenda ku-practice kile ambacho wamejifunza kutoka kwenye chuo cha VETA. Maana yake ni kwamba tunawekeza fedha nyingi kuwafundisha watoto hawa lakini tija yake haionekani kwa sababu wanakwenda kwenye maeneo ambayo umeme hakuna, kwa hiyo application ya knowledge waliyoipata inakuwa haionekani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, tunamshukuru Rais sisi Wananewala, Tandahimba na Nanyamba, ametuletea fedha shilingi bilioni 84.7 kwa ajili ya mradii mkubwa wa maji ambao sasa hivi umeanza kutekelezwa. Karibuni, ikifika 2024, Juni huko mradi unakwenda kukamilika; tutasukumaje maji yawafikie wananchi kama hatuna umeme wa uhakika? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo mimi niiombe sana Wizara, tunashukuru kwa yale ambayo mmekuwa mnayabuni kila siku, lakini tukasimamie suala la ufikaji wa umeme katika vijiji vyetu. Tumeona kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri kuna kipengele cha kupeleka kwenye vitongoji 15 kila jimbo kufikisha umeme. Newala Vijijini naogopa, kwa sababu kama vijiji mpaka leo havijafikiwa, hivyo vitongoji vitafikiwa kesho? Kwa hiyo Mheshimiwa Waziri na timu yako, mna kazi ya kufanya Newala Vijijini. Bahati nzuri tumeshakueleza kwa kina na wewe unatambua pamoja na management yako, ni kusimamia sasa tuone utekelezaji wa yale makubaliano, yaende yakatekelezwe kwa vitendo ili uchumi wa wananchi wa Newala Vijijini pamoja na Mtwara kwa ujumla, kupitia sekta ya umeme, ukaweze kupatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo ninataka kuliongea kidogo; tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa suala lile la LNG pale Lindi. Uwepo wa mradi ule mkubwa utachechemua kwa kiasi kikubwa sana uchumi wa watu wa Kusini. Kwa sababu kama mradi utaanza kutekelezwa, akina mama wanaolima mbogamboga watakwenda kuuza, na mambo mengi sana ambayo yanategemea upatikanaji wa nishati ile kwa ajili ya uzalishaji wa uchumi kwa wananchi wa Mtwara na Lindi, kwa kweli yatakwenda kufanikiwa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo niombe tu Wizara, kwamba tusimamie utekelezaji ili miradi hii ikaweze kuleta maendeleo ya kiuchumi kwa mwananchi mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Kengele ya pili ilishagonga Mheshimiwa Mtanda.

MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi; naunga mkono hoja. (Makofi)