Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati

Hon. Dr. John Danielson Pallangyo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Arumeru-Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati

MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia kwenye Wizara hii ya Nishati ambayo ndiyo hasa inatupeleka kwenye maendeleo nchi hii. Pamoja na shukrani hizo nichukue nafasi hii pia kuungana na wenzangu kukuombea uso wa Mungu upatane nawe katika hiyo safari ambayo unaiendea. Tunaamini kabisa kwamba unaweza. Kwa namna ambavyo unaendesha hili Bunge kwa umahiri mkubwa, huko unakokwenda ni shaihi kabisa. Tunakuombea Mungu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nianze kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa jinsi ambavyo anatufanyia kazi Watanzania. Pamoja na fedha nyingi sana ambazo ameweza kupeleka majimboni mabilioni kwa mabilioni, lakini pia ameendelea kutekeleza miradi mkakati mikubwa na mfano mzuri kabisa ni hili Bwawa la Nyerere ambalo linakuja kutuongezea umeme mwingi sana kwenye grid ya Taifa, megawati 2,115. Kazi inayofanyika ni nzuri na sasa hivi kazi imefikia asilimia 86.89; kwa kweli tunamshukuru na kumpongeza.

Mheshimiwa Spika, lakini kipekee nimpongeze Waziri Januari Makamba na Naibu wake Stephen Byabato lakini pia Katibu Mkuu Eng. Mramba na Naibu wake Bwana Butuka na watendaji wote pale Wizarani, kazi ni nzuri inaonekana. Waliobahatika kufika kwenye mabanda ya maonesho ya wiki ya nishati, wanaweza kukubaliana na mimi kwamba Wizara inafanya kazi nzuri na mmejipanga vizuri. Kwa hiyo ninachoweza kusema ni kwamba muendelee vivyo hivyo; ari hiyo hiyo, nguvu hiyohiyo, msirudi nyuma kwa sababu hii kazi ya kusambaza nishati kwa Watanzania ndiyo maendeleo yenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na sifa na pongezi hizo kwa Wizara nizungumzie kidogo kuhusu REA. Tunashukuru kwamba REA wanafanya kazi vizuri lakini kuna mapungufu. Waheshimiwa Wabunge wamesema, kwamba bado vijiji vingi havijapata umeme, vitongoji ndivyo vingi zaidi; lakini pia hat akule kwangu kule Arumeru Mashariki hali sio shwari sana. Kuna kata, vijiji na vitongoji ambavyo bado havijapata umeme. Hivi ni kama vile Kata za Uwiro, Marurango, King’ori na Majengo, kuna vijiji na vitongoji ambavyo havijapata umeme wa REA. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na niseme kwamba, tatizo kubwa sana ni kwamba, hawa wakandarasi ambao wanapewa hii kazi wanapokuja majimboni wanakwenda moja kwa moja site bila kuwasiliana na mamlaka. Wanapaswa wakifika waripoti kwa DC, waripoti Halmashauri, lakini pia na Ofisi ya Mbunge kwa sababu Mbunge ndiye anayefuatilia hizi fedha. wanapokuja halafu wanakwenda moja kwa moja site kunakuwa kuna maswali mengi kwamba, kazi inaendeleaje, lakini kama wakipitia kwenye hizi ofisi nilizosema tukakaa chini wakatueleza mpango kazi inakuwa ni rahisi kuwafuatilia na kujua kwamba, kazi inaendeleaje. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la kule Korogwe ambalo limezungumzwa na Mwenyekiti wa Kamati ya Nishati ni mfano halisi, kwamba kuna mapungufu. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri aliangalie hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia, niseme kwamba bei ya kuunganisha umeme bado haiko clear. Nadhani ni wakati umefika Serikali iwe wazi iseme sasa kwamba, utaratibu uko hivi, shilingi 27,000/= zitatumika maeneo fulani na kulipia nguzo itakuwa maeneo fulani, ili tuache kuuliza maswali ambayo tunakutana nayo kwa wananchi na hatimaye na sisi tuwe na amani.

Mheshimiwa Spika, nilisema kwamba, kazi ni nzuri inayofanyika na Wabunge wote wamepongeza. Na niseme kwamba, Mheshimiwa Waziri endeleeni kufanya kazi vizuri, msimamie hapohapo, Watanzania wanawaona na wanawaelewa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya hayo machache nakushukuru sana kwa nafasi hii. Naunga mkono hoja. (Makofi)