Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati

Hon. John Michael Sallu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Handeni Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati

MHE. JOHN M. SALLU: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kupata nafasi hii. Kwanza nikushukuru sana kwa jinsi unavyotuongoza na unavyotulea, na jambo lako ni jambo letu na Insha Allah Mwenyezi Mungu ataliwekea mkono litakwenda kwa kheri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nipende kumshukuru sana Mama yetu Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutupa fedha nyingi ambazo zimeendesha miradi mingi katika majimbo yetu hususan Jimbo langu la Handeni Vijijini. Kwa kweli tunamshukuru sana kwenye Jimbo letu la Handeni Vijijini ameleta fedha ambazo zimeendesha miradi mingi sana ya maendeleo kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nipende kumshukuru ndugu yangu January Makamba, Naibu wake Byabato, Katibu Mkuu Ndugu yangu Mramba na timu yote ya Wizara kwa kazi kubwa wanayoifanya katika kuhakikisha umeme na mambo yote ya mafuta ambayo yapo chini ya Wizara yao yanakwenda vizuri kabisa na nchi yetu inaimarika; kwa kweli hongereni hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kutokana na speed inavyokwenda sasa hivi ya umeme vijijini kwenye Jimbo letu la Handeni Vijijini mpaka ikifika mwezi Desemba vijiji vyote 91 vitakuwa vimeshapata umeme. Kwa kweli tunashukuru, tunashukuru sana kwa sababu heka heka na speed ya mkandarasi inaenda vizuri kwa hiyo tuna imani ikifika mwezi Desemba hali ya vijiji vyetu kupata umeme itakuwa imefika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini nitoe ombi kwenye vitongoji. Jimbo letu la Handeni Vijijini lina vitongoji 770, kwa hiyo naomba tuangalie kwa jicho la huruma kwa sababu vitongoji ni vingi sana na shida ya umeme vitongojini ni kubwa na tayari vitongoji vile vina idadi kubwa ya watu kwa sasa hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nipende kumshukuru sana Mama yetu, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa mara ya pili kwa kuridhia kutoa fedha ambazo zinaleta mwarobaini ambao ulikuwa unasababishwa na tatizo la kukatika umeme zaidi ya mara 20 kwa siku kwenye Jimbo langu la Handeni Vijijini. Sasa ameridhia kutoa fedha bilioni 77.5 kwa ajili ya kujenga sub station kubwa ya MVA 120 pale Mkata, na line ya double circuit itatoka Mkata kuelekea upande wa Kwa Msisi, Mkalamo mpaka Pangani kwenye migodi ya graphite na chuma, na line nyingine itatoka pale Mkata itaelekea Kabuku Mzundu mpaka kwa Bojo kwenye migodi ya dolomite, calcite pamoja na chuma. Line nyingine itakwenda upande wa Manga – Madebe – Sua mpaka Kang’ata kwenye migodi ya dhahabu. Kwa kweli umeme huo utatukomboa sana hata kiuchumi kwenye eneo letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kama haitoshi Mama huyu vile vile ameridhia kutoa fedha kwa ajili ya line nyingine kubwa itakayotokea pale Mkata kuelekea Handeni Mji mpaka kwa ndugu zetu wa kule Kilindi. Kwa kweli tunashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niipongeze Wizara kwa kuzama zaidi kwenye vyanzo vya nishati jadidifu. Hivi karibuni tumeshuhudia wakisaini umeme wa umemejua. Na mimi napenda kusisitiza hapo kwenye nishati jadidifu kwa sababu kwanza ni nishati salama lakini vile vile itatuongezea nguvu kwenye Gridi yetu ya Taifa. Kwenye masterplan inatakiwa ikifika mwaka 2030 masterplan ya umeme tunatakiwa tuwe na megawatt zisizopungua 10,000. Sasa nilikuwa nashauri tuzame zaidi kwenye Umeme wa Jotoardhi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Umeme wa Jotoardhi Tanzania tuna viashiria 50 vya umeme wa joto ardhi ambavyo tukivitumia vizuri tutaweza kupata megawatt zisizopungua 5,000 ambazo zitakuwa ni mchango mkubwa sana kwenye Gridi yetu ya Taifa. Lakini kwa kuanzia kuna maeneo matano ambayo tayari yamekaa vizuri, na ninaishukuru Wizara imeweza kununua ridge kwa ajili ya kuchimba ili tupate mvuke ule wa kuendesha zile turbines.

Mheshimiwa Spika, katika hayo maeneo matano ambayo yanatarajiwa kutota megawatt 200 naomba Wizara ipeleke fedha kuhakikisha jambo hili linatokea. Lakini vile vile niombe Serikali kwa ujumla kukamilisha Sheria ya Umeme wa Jotoardhi kwa sababu bila sheria hatutakwenda vizuri kwenye eneo hilo; kwa sababu kwenye jotoardhi inatakiwa kuwe na sheria madhubuti itakayowawezesha hata wawekezaji kuweza kuvutiwa kuja kuwekeza kwenye umeme wa jotoardhi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na ndugu zangu hii joto ardhi huwa pamoja na kuzalisha umeme lakini lina vitu vingi unaweza kuvuna ndani yake. Kwa mfano mvuke ule ukishatumika kutengeneza umeme utaweza kutusaidia kukausha mazao, kukausha mbegu zetu, kwa yale maeneo yanayolimwa mbegu za kuzalisha mbegu. Pia itatusaidia kukausha vitu kama samaki, lakini vile vile inazalisha vitu kama hydrogen na sulphur ambazo zitatumika hospitalini, vile vile tunaweza tukapata Carbon dioxide ambayo huwa inatumika kwenye vinywaji baridi bia na soda. Kwa hiyo jotoardhi hili lina faida kubwa sana, kwa hiyo nilikuwa naomba tuwekee mkazo zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa haya machache nashukuru sana naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)