Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati

Hon. Samweli Xaday Hhayuma

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati

MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, ahsnate sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia bajeti ya Wizara hii ya Nishati.

Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kumpongzea sana Mheshimiwa Waziri wazo lake la kufanya wiki ya nishati hapa Dodoma imetusaidia sana sisi Wabunge. Badala ya kutafuta wa wilaya, mkoa na ngazi ya Taifa wote tunawapata kwa pamoja, kweli wameturahisishia huduma na suluhu zingine tumekuwa tukizipata hapa hapa. nimpongeze sana kwa ubunifu huo, ni vitu vya kuigwa na kuendelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kazi kubwa inafanyika kwenye sekta ya nishati, na naamini kwamba miradi hii ikikamilika kwa wakati, na Mheshimiwa Waziri amechambua vizuri, kwamba tutaongeza upatikanaji wa umeme mpaka kufikia megawatt 5,213.22 na tutakuwa tunaanza kuuza umeme mpaka nje ya nchi. Ninaomba, kwa sababu lengo hili limewekwa mwishoni mwa mwaka wa fedha 2023/2024, naomba kasi hii iongezeke ili tupate umeme wa uhakika kwani umeme ndio unaowezesha viwanda kuendelea na Tanzania viwanda haviwezekani bila kuwa na umeme wa uhakika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kipindi kirefu tumekuwa na changamoto mmesikia wenzangu wakisema umeme unakatika. Jimbo la Hanang’ changamoto hiyo ipo, umeme unakatika na haijulikani wakati gani kuna umeme na shughuli zinalala. Sisi ni wakulima, sisi ni wafugaji; kuchakata mazao hayo ya mifugo, mazao yanayotoka mashambani inakuwa ni changamoto kubwa kwa sababu umeme unakatika sana. Tulikuwa tumesahau kipindi cha hapo katikati masuala ya kuhangaika na generator lakini sasa hivi wimbo umekuwa ni huo. Naomba uchukue hatua. Na pale ulitupa kituo cha kupooza umeme ili angalau kupunguza ile line kwa sababu line ikiwa ndefu nayo inachangia umeme kukatika. Pale Mogitu watu wako wamekwisha tembeatembea naomba zoezi lile la kujenga kituo cha kupooza umeme liharakishe.

Mheshimiwa Spika, wakati Dkt. Samia Suluhu Hassan, anashika nchi vijiji vyangu vyenye umeme vilikuwa 54 tu, kwa sasa viko 73. Nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa ambayo inafanyika ya kuwapatia wananchi umeme. Hata hivyo, bado tuna vijiji 23 naomba mkandarasi ambae yuko site msukume aongeze kasi mradi ule uweze kukamilika na wananchi wapate umeme. Lakini kuna maneo mengine ambapo umeme umegusa tu kama Kijiji cha Getasam nyumba tatu tu ndizo zina umeme. Watu wako waangalie eneo hilo ili utusaidie watu wapate umeme wa kutosha.

Mheshimiwa Spika, vilevile kuna maeneo ambayo yamepata umeme tangu miaka ya 90, watu wameongezeka sana kwenye maeneo hayo. Kata kama ya Gitting maeneo yake mengi yalipata umeme zamani. Sasa hivi tunapeleka umeme kwenye vijiji vipya ambavyo havina umeme lakini wale wa zamani kasi ya TANESCO ni ndogo sana.

Mheshimiwa Spika, ukienda Nangwa maeneo mengi watu wengi wengi hawana umeme, ukienda Gendabi maeneo ambayo umeme ulipatikana zamani watu wengi hawana umeme, maeneo ya Jorodom maeneo hayo yaangaliwe kwa jicho la kipekee ili watu wapate umeme.

Mheshimiwa Spika, umeme ukifika kwenye eneo unachangamsjha maendeleo na watu wanajenga zaidi. Wakijenga TANESCO waongeze kasi ya kupeleka umeme kwa wananchi. Lakini, kuna changamoto pia, sijui ni TANESCO au wakandarasi wenu ambao mmewathibitisha; wanawambia wananchi wafunge umeme. Kwa mfano Kijiji changu cha Dirma Kata ya Bassotu wananchi asilimia kubwa wamefanya wiring miaka mitatu mpaka sasa umeme umeme haujaenda. Sasa mnapohmasisha wananchi wafanye wiring iende sambamba na miradi ya upelekaji wa umeme.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema haya ya jimboni kwangu; kwenye hotuba yake Mheshimiwa Waziri ameeleza vizuri kuhusu matumizi ya gesi; ni kama matumizi ya mpito, na ikifika 50/50 kwa ule mpango wa kutumia clean energy gesi nayo itakuwa phased out. Mmefanya negotiation ya gesi asili imechukua muda mrefu sana. Ongeza kasi kwenye eneo hilo ili gesi hii ya kwetu tuweze kuitumia na tunufaike nayo. Imechukua muda mrefu mnajadiliana mjadala huo haufiki mwisho. Simamia, na tunakuamini; wewe nguvu yako ni kubwa na ubunifu tumeuona weka kasi hapo ili hatimaye tuweze kutumia gesi yetu ya asili iweze kunufaisha taifa letu isije ikawa kama makaa ya mawe, ambako dunia sasa inaacha matumizi ya makaa ya mawe na sisi hata hatujawahi kuyatumia. Hivyo, isije ikatokea kwenye gesi pia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hapa Bungeni tumejadili sana masuala ya udhibiti vinasaba kwenye mafuta. Huko nyuma kulikuwa na kelele nyingi sana, imeenda TBS sasa hivi kumetulia. Maneno yameanza kuwa mengi kwamba sasa TBS waondolewe kwenye eneo la usimamizi wa vinasaba kwa ajili ya kuhakikisha ubora wa mafuta yetu. nikushauri tu kwamba, jambo lililotulia tusiliamshe tusiingie kwenye migogoro ambayo haina tija. Mamalaka ya TBS ni msimamizi wa ubora kwa bidhaa nyingi kazi kubwa anafanya, maabara zake ni nzuri tuendelee kuwaamini.

Mheshimiwa Spika, nigusie kidogo eneo la Shirika letu la TANESCO. Mheshimiwa Waziri, tupia jicho kule kidogo. Shirika hili lina mkataba wa hali bora ya wafanyakazi na chama cha wafanyakazi; lakini kuna harakati mbalimbali zinazofanyika katika kuboresha shirika. Ni jambo jema kwa sababu ili shirika lolote liweze kuwa na ufanisi ni lazima lijitazame. Hata hivyo, majukumu yote yanayofanyika kila mmoja anataka kujua kesho yake iliyo wazi. Hata wewe Mheshimiwa Waziri unapanga mipango yako na upanga vitu ambavyo vitakutengenezea njia ya kazi. Na watumishi nao wanataka kufahamu haki yao na majukumu yao wanayoyafanya na wajibu wao wanaoutekeleza lakini haki ziwe wazi, kama kuna mabadiliko yoyote washirikishwe ili hatimaye nao wajipange kwa sababu ni watu wana mipango yao, badala ya kuwa na harakati ambazo zinafanyika ambazo haziko wazi kwa chama cha wafanyakazi.

Mheshimiwa Spika, nikuombe tu, baada ya kusema haya ambayo nimesema, Jimbo langu la Hanang’ ni kati ya majimbo makubwa; tuna vijiji 96 na vitongoji 414. Wakati unapopanga mipango yako ya kazi majimbo haya makubwa uyaangalie kwa macho ya kipekee ili hatimaye maendeleo yaweze Kwenda sambamba katika nchi yetu. Uki-concentrate, na kwa mfano suala hili upande TARURA nilishaongelea, kwamba tunagawa rasilimali kijimbo au kiwilaya maeneo mengine ni makubwa na mengine ni madogo. Maeneo haya makubwa yaangaliwe ikiwezekana twende kwa idadi ya watu au kwa hali ya jiografia ya maeneo yanayohusika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baadya ya kusema haya nakushukuru sana naunga mkono hoja.