Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Hon. Asia Abdulkarim Halamga

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi ya kuweza kuchangia kwa ufupi katika Bajeti ya Wizara ya Mambo ya Ndani kwa mwaka 2023/2024.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niungane na wote ambao wameweza kumpongeza Mheshimiwa Rais pamoja na Waziri, Naibu Waziri, Wizara nzima kwa ufanisi wao wa kazi na utendaji wao wa kazi. Nichukue nafasi hii kutoa pole sana kwa wananchi wa Endasak, Wilaya ya Hanang kwa kuunguliwa na soko usiku wa kuamkia juzi, lakini niendelee kuwapa pole kwa sababu wafanyabiashara wengi ni wa hali ya chini kabisa hususani akina mama ambao wameweza kupteza mitaji yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kumpongeza Mkuu wa Wilaya pamoja na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya lakini kubwa zaidi wananchi wa Endasak na wa Wilaya ya Hanang’ kwa kukabiliana na moto ule japo umeweza kuleta hasara lakini walihangaika usiku kucha na kufanikiwa kuuzima japo hawakuweza kufanikiwa kuokoa vitu. Adha hii ambayo imeweza kuwakuta wananchi hawa ni kwa sababu Mkoa wa Manyara kwanza kijiografia kutoka Wilaya na Wilaya, Wilaya iliyopo karibu ni kilometa 75, kwa hali ya kawaida Wilaya nyingi unatembea takribani kilometa zaidi ya 300 na hivyo kunapotokea janga na kwa sababu hatuna gari la zimamoto madhara yanakuwa ni makubwa zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo ninamuomba Mheshimiwa Waziri uzingatie jiografia ya Mkoa wa Manyara ukubwa wake na uzingatie sasa tuweze kupata gari kwa sababu hatuna gari la zimamoto, gari lililopo lipo Babati Mjini na hatuna visima maalum kwa ajili ya maji, pia hatuna mabomba maalum kwa ajili ya uzimaji wa moto. Kwa hiyo, tunakuomba sana unapokuja kuhitimisha hoja yako basi uhakikishe kwamba Mkoa wa Manyara tupate usafiri huo ili kuweza kukabiliana na majanga yanapotokea ndani ya Mkoa wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo nakushukuru kwa kunipa nafasi. (Makofi)