Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Hon. Sylivia Francis Sigula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

MHE. SYLVIA F. SIGULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia. Kwanza kabisa nianze kwa kumshukuru Mungu Mwingi wa Rehema kwa kuniwezesha kusimama katika Bunge lako hili tukufu. Nitumie nafasi hii pia kumpongeza Mheshimiwa Waziri kaka yangu Masauni na Naibu Waziri, kwa kweli wanafanya kazi nzuri sana na tunawapongeza sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii pia kuipongeza Serikali. Sasa hivi askari wetu wanapokuwa kwenye mafunzo haya ya refresher course mambo ni mazuri. Serikali imechukua suala lile la chakula na sasa hivi inaligharamia Serikali. Tunaipongeza sana Serikali na waendelee kufanya hivyo ili askari wetu wafanye kazi zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la ulinzi wa raia na mali zao tumewapa jukumu hili Jeshi la Polisi. Ni ukweli usiofichika Jeshi la Polisi wanafanya kazi kubwa sana, lakini mazingira yao ni magumu mno. Leo ukienda Mkoa wa Kigoma, ukienda Wilaya ya Kibondo ukaambiwa hizi ndizo nyumba za askari, utatoa machozi, lakini utaungana na mimi Wabunge hapa wanasimama kila mmoja anaelezea makazi ya askari, makazi ya askari. Mimi naomba nikuombe Mheshimiwa Waziri, utakapokuja kumalizia hapa hebu tupe mkakati wa Serikali ni namna gani tunaenda kukabiliana na hili jambo la nyumba za askari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ningependa kuchangia kuhusu hii inaitwa Police General Order (PGO). Kama kuna changamoto ambayo polisi wanakutana nayo basi ni hii PGO. PGO hii imeanzishwa zaidi ya miaka kumi iliyopita, na huenda lengo lake lilikuwa zuri, kuwapa motisha askari, lakini jambo hili kulingana na mazingira ya sasa limekuwa tena halina uhalisia na hivyo ni wakati mwafaka sasa wa kufanya mapitio yahii PGO. PGO hii ni sheria zinazoongeza Jeshi la Polisi, na zimekuwa zimeeleza mambo mengi sana. PGO hii ina kurasa zaidi ya 900 lakini mimi nitaomba nijielekeze kwenye PGO namba 132. PGO hii namba 132 inazungumzia posho za askari. PGO hii imeeleza posho nyingi ambazo askari anastahili kupewa. Kuna posho ya pango, kuna posho ya mavazi, kuna posho ya upelelezi, kuna posho ya utaalam lakini kuna posho nyingine nyingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini masikitiko yangu ni kwamba posho hizi haziendani na uhalisia wa sasa kwa mfano, ukizungumzia posho ya pango inasema askari atapewa asilimia kumi ya mshahara. Huenda kwa kipindi hicho ilikuwa ina maana sana. Leo kwa askari anayepata mshahara wa laki tano asilimia kumi ni shilingi elfu 50, sasa uniambie ni nyumba gani askari atapata kwa shilingi 50,000? Hii haiwezi kukubalika. Lakini PGO hii haijaeleza ni namna gani hii posho wanapewa. Sasa ninashauri Serikali tufanya mapitio, tupitie hii ili tutoe utaratibu rasmi ni namna gani askari wanapata posho hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tunazungumza hapa, unapozungumzia suala la posho ya mavazi, maisha yamebadilika kila mmoja anafahamu. Miaka kumi iliyopita leo uhalisia ni tofauti…

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE.SYLVIA F. SIGULA: …leo unampa posho ya mavazi askari, unasema posho ya mavazi apewe shilingi 30,000, kwa mavazi gani atakayo nunua?

Mheshimwia Mwenyekiti, kwa hiyo mimi niombe, ni wakati sasa Mheshimiwa Waziri wa kufanya mapitio ya hii PGO kwa sababu ina mambo mengi mengi sana ambayo yanahitaji kufanyiwa marekebisho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo ningependa kulizungumzia ni suala la rushwa kwa askari polisi. Mimi nilikaa nikatafakari sana, lakini nikaona kuna uhusiano wa moja kwa moja kati ya rushwa kwa askari na uhaba au ufinyu wa mishahara yao. Haiwezekani leo upate mshahara ambao hauwezi kukidhi mahitaji yako. Kitakachofanyika ni nini? Kwa hiyo mimi niombe Mheshimiwa Waziri, ni wakati sasa wa kuboresha maslahi, ni wakati sasa wa kuboresha mishahara ya askari ili nao waweze kufanya vizuri. Tusikae kuwalaumu rushwa, rushwa, rushwa wakati maslahi yao ni madogo. Mwaka jana ilitembea video hapa ya askari amechukua elfu kumi kama rushwa …

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa malizia.

MHE. SYLVIA F. SIGULA: Mheshimiwa Mwenyekiti,lakini askari yule ile video ilinitoa machozi. Askari yule elfu kumi ile alipewa adhabu kali, alifukuzwa kazi lakini leo ukisoma ripoti ya CAG kuna wezi wa mabilioni bado wako ofisini. Hili jambo haliwezekani. Kwa hiyo mimi niombe Mheshimiwa Waziri, askari wanafanya kazi kubwa sana na wanafanya kazi ngumu sana hebu ifikie hatua tuwape thamani yao. Ikitokea kesho askari wakagoma ndio utaelewa kwa nini askari ni muhimu katika nchi hii.

MWENYEKITI: Mheshimiwa ahsante, malizia.

MHE. SYLVIA F. SIGULA: Tuna amani sasa kwa sababu askari wanafanya kazi yao vizuri. Naunga mkono hoja ahsante. (Makofi)