Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Hon. Simai Hassan Sadiki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nungwi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

MHE. SIMAI HASSAN SADIKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana nami kunipa nafasi ya kuwa mchangiaji siku hii ya leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nitumie fursa hii kumpongeza sana Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama Samia Suluhu Hassan kwa uzalendo wake mkubwa aliouonesha jana, licha ya kwamba Dar-es-Salaam Young Africans walipoteza mchezo, lakini hakurudi nyuma aliweza kuweka mzigo mezani kama alivyoahidi. Pia nitumie fursa hii kumpongeza sana Rais wa Zanzibar Dkt. Hussein Ali Hassan Mwinyi kwa kudumisha misingi ya haki na utawala bora katika uongozi wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Taifa lolote raia ili ajulikane kwamba yeye ndiye mwananchi wa Taifa hilo hakuna kinachomtambulisha zaidi ya kitambulisho. Kitu kinachoshangaza katika Taifa letu hili mambo ni tofauti. Kumekuwa na ukakasi mkubwa katika upatikanaji wa vitambulisho vya uraia, vitambulisho vya Mtanzania. Mheshimiwa Waziri ningependa sana Kaka yangu utakapokuja hapa kuhitimisha ni lazima utueleze mkakati wa Serikali mlionao juu ya upatikanaji wa vitambulisho vya Mtanzania. Kama siyo hivyo, mimi sitaondoka na shilingi, lakini nitaondoka na mshahara wote na mamilioni yako. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna jambo ambalo linaendelea sasa hivi, kule Zanzibar tunapozungumzia suala la upatikanaji wa leseni za udereva ni tofauti sana na huku. Zanzibar ili upate leseni ya udereva wanaohusika na masuala ya leseni ya udereva ni mawasiliano. Maana inawezekana mawasiliano wakaidanganya Wizara ya Mambo ya Ndani, lakini Tanzania Bara ili upate leseni ya udereva ni lazima upite kwa Jeshi la Polisi. Jeshi la Polisi wao ndiyo wanaotoa leseni za udereva. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi karibuni kumekuwa na zoezi la unyang’anyaji wa leseni za udereva kwa madereva hata kama wameendesha miaka 20. Unajua napata suala kitu kimoja, leseni walizokuwanazo zinathibitisha wazi kwamba wao walikuwa na leseni, lakini kwa nini wanyang’anywe leseni? Sifa gani waliyoikosa? Kama kumrejesha darasani kwa nini msimrejeshe wakati ule ambapo alikuja kuomba leseni, mumrejeshe sasa hivi kakosa sifa gani? Je, kapunguza uwezo wa kuona au kigezo kipi mnachotumia? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa nimkumbushe Kaka yangu Mheshimiwa Masauni na Mheshimiwa Jumanne kwamba, mwaka jana niliuliza swali hapa Bungeni kuhusiana na ujenzi wa nyumba za Askari kule Nungwi na upanuzi wa kituo cha Polisi. Majibu niliyojibiwa ni kwamba, mnawaruhusu wananchi waliozunguka maeneo yale waweze kukodisha nyumba zao ili Askari wale wapate sehemu ya kukaa. Kusema kweli, nilikaa nikatafakari mara sita, hivi kweli askari tunamtakia mema? Turuhusu raia aende akamkodishe tena maeneo ya Nungwi ambayo ni maeneo ya uwekezaji? Chumba kimoja unaweza kukodi kwa laki, je, leo Askari ana familia nyumba moja atakodi kwa shilingi ngapi? Kwa mshahara gani anaoupata atakaoweza kujikimu kama siyo kumtengenezea misingi ya rushwa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kibaya zaidi, ulikataa kupanua nyumba za Askari, ulikataa kupanua eneo la Kituo cha Polisi, kinachonisikitisha na kinachonihuzunisha, umeenda kuchukua kituo changu cha afya Nungwi na kuweka Askari Utalii, hili jambo halikubaliki. Hili jambo halikubaliki! Kituo cha afya kile wananchi walikuwa wanakitegemea sana, kuweka Askari wako katika maeneo yale kumesababisha usumbufu mkubwa. Kama ulishindwa kujenga vituo vya polisi basi ilikuwa huna haja ya kwenda kung’ang’ania kituo cha afya, mlitumia njia moja mkatuchezea mchezo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri tuliuliza kwa nini kituo chetu kimefungwa? Hoja mkasema kwamba, kituo kile mashimo yake ya choo yamejaa, ninachotaka niulize wale Askari wako wanajisaidia wapi? (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, sababu ya pili ukaniambia kwamba, pindi ikinyesha mvua katika maeneo yale maji yanaingia mpaka ndani yanaweza kusababisha maradhi juu ya wagonjwa, hivi Askari wao wana kinga juu ya maradhi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuelewe ya kwamba, kabla ya kuanzishwa Polisi Utalii, Nungwi sisi tulikuwa na Polisi Shirikishi, Polisi Jamii. Polisi Jamii walikuwa wanafanya kazi kubwa mno kwa sababu, ulinzi wa kwanza wa raia na mali zao unategemea zaidi wananchi wanaozunguka maeneo yale. Leo hii mmetuletea Askari Utalii, sipingani nao, Rais alianzisha kile kikundi kwa lengo mahsusi na lengo madhubuti kabisa, lakini leo hii kimebadilika kikundi kile, kimekuwa ni kikundi cha manyanyaso, kimekuwa kikundi cha wala rushwa, kimekuwa ni kikundi ambacho kinasababisha shaghalabaghala, zogo, kafara, sijui hata kitu gani kwa wananchi wangu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mambo mengine lazima tukae tutafakari sisi kama Taifa, hivi tuseme Askari Jamii wakiwezeshwa hivi wanaweza kushindwa kweli kulinda fukwe zao? Hivi Askari Jamii tukiwapatia vifaa kuna haja gani ya maeneo yale yanayozunguka fukwe kuleta Askari Utalii kulinda beach?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jeshi la Uhifadhi lilikuwa na dhamira nzuri kuanzishwa, kama nilivyotangulia kusema, lakini sasa hivi Mheshimiwa Waziri, wanalichafua Jeshi letu la Polisi. Misingi na utaratibu wa uchukuaji wa rushwa na kunyang’anya kwa kutumia nguvu imekuwa mtihani katika maeneo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme kitu kimoja, wakati mlipokuja kujenga kituo Nungwi, wananchi waliamini kwamba mtawalinda raia na mali zetu, lakini kumbe mmekuja kutuwinda raia na vitu vyetu. Mmekuja kuwawinda raia na wasio kitu, kwa sababu vituo vya Polisi vimekuwa vina-base zaidi kuwaweka ndani wale watu masikini. Masikini wananyanyasika. Kile Kituo cha Polisi pale Nungwi kimekuwa kikitumika na watu kuonesha mamlaka waliyokuwa nayo. Watu wanaweza kuwekwa ndani kituoni, lakini sababu za msingi hazijulikani. Tunaongoza kwa kuwa na unreported case. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kibaya zaidi kinachonisikitisha, unaleta kesi za watu wanaohusika na dawa za kulevya; wananchi wetu wanajitolea kuwaonesha maaskari nani na nani anayehusika na dawa za kulevya, kumbe tunawatafutia kula! tunaleta ripoti leo, kesho mtu huyo katoka. Halafu anakuja kukutajia, sasa nimeambiwa na afande moja, mbili, tatu. Kusema kweli tunalikosesha uaminifu Jeshi letu la Polisi na tunaliondolea ushirikiano baina ya raia wema na Jeshi hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati walala hoi, waendesha bodaboda na wavuvi wananyanyasika; wakati hawa wanalia; cha kushangaza, wauza unga, wavuta bangi na wanaokwepa kodi za Serikali, wao wanalindwa pamoja na kuhifadhiwa. Tunaelekea wapi? Mara ngapi Kituoni kwetu Nungwi tunapeleka watu ambao wanahusika na tuhuma mbaya lakini mnawaachia? Mheshimiwa Waziri mimi nimekuwa nikikutumia messages mara nyingi juu ya mwenendo mzima wa Kituo cha Polisi, Nungwi, lakini hakuna moja linalotekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitazuia mshahara wa Mheshimiwa Waziri kama hajanipigia msasa kituoni kwangu.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Simai. Malizia sekunde 30.

MHE. SIMAI HASSAN SADIKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. (Makofi)