Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Hon. Hamida Mohamedi Abdallah

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Lindi Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia. Kwanza nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri na timu yake kwa maandalizi ya bajeti ya 2023/2024. Bajeti ambayo inatupa afueni wa kwenda kupunguza changamoto mbalimbali. Sina mashaka na bajeti hiyo na naunga mkono kwa asilimia mia moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze Kamati kwa taarifa yao, lakini kwa ushauri wao mzuri walioutoa na naomba Wizara kuzingatia ushauri wa Kamati ili waweze kuufanyia kazi na hatimaye ikiwezekana bajeti inayokuja, basi tuone mabadiliko ya changamoto mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze vilevile Koplo Hamisi Masana kwa kukataa kupokea rushwa wakati anatekeleza kazi zake. Amekuwa ni mfano mzuri, lakini sio rahisi kwa watu wengine. Huyu ameonesha mfano mzuri na ni mzalendo wa kweli. Tuhakikishe basi wenzetu wengine wanafuata nyayo za Koplo Hamisi kwa kutopokea rushwa wakati wakiwa kazini ili tuweze kupunguza changamoto mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la Polisi. Ninamshukuru sana Mheshimiwa Waziri wetu kwa sababu nilikwenda kupeleka kilio cha Polisi. Lindi Manispaa tulikuwa hatuna Kituo cha Polisi, tulikuwa na Kituo cha Polisi lakini walikuwa wanatumia nyumba za kupanga. Ninamshukuru Waziri Masauni kwa wema wake wa kutupatia shilingi milioni 900 na tumeweza sasa kuendeleza ujenzi wa Kituo cha Polisi Daraja A, kituo hiki kitakuwa cha mfano Kanda nzima ya Kusini. Kwa hiyo, nikushukuru sana Mheshimiwa Waziri wetu kwa wema wako na kwa huruma ambayo umeionesha kwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikizungumzia suala la Wilaya ya Lindi, Lindi ina Majimbo matatu na jiografia yake Mheshimiwa Waziri anaifahamu vizuri kwa sababu ameshawahi kuja na anajua mazingira yaliyopo. Changamoto tunayoipata ni vitendea kazi, ukiangalia ukubwa wa eneo tuna Jimbo la Mtama, Jimbo la Lindi Mjini na Jimbo la Mchinga, ukiangalia hayo maeneo hatuna magari ya kutosha. Panapotokea dharura yoyote Polisi wanashindwa namna ya kwenda kushughulikia changamoto ambazo zinajitokeza. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri nikuombe sana katika eneo hili ambalo umeagiza magari yaliyoingia nchini na magari ambayo tunategemea yatakuja, uitazame Lindi kwa jicho la huruma kuhakikisha kwamba, tunapata gari na Polisi waweze kufanya kazi yao vizuri kwa sababu kuna doria nyingine za usiku wanashindwa kufanyakazi kwa sababu ya kukosa vitendea kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ofisi ile ya Polisi haina viti, haina fenicha, mazingira ya kazi ni magumu. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri nikuombe sana tutakapokamilisha ofisi mpya basi tupate vitendea kazi kuendana na hali ya ofisi na mazingira ya ofisi yatakavyokuwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na changamoto hiyo, niiombe Kamati ije kutembelea Lindi kuona mazingira ya nyumba za Polisi wanazoishi. Nyumba zile ni chakavu, nyumba zimepitwa na wakati, vijumba vidogo utafikiri mabanda ya kufugia Wanyama, ni huruma sana. Ninakuomba sana Mheshimiwa Waziri pamoja na kwamba, ziko fedha ambazo zimetengwa katika kujenga nyumba za Polisi, hebu rudi tazama Lindi, mazingira yaliyopo kuhakikisha kwamba, Polisi Lindi wanapata nyumba. Japokuwa tusiwezeshe nyumba za kukamilisha wafanyakazi wote, lakini kila mwaka tukipata kiasi cha kujenga nyumba za Polisi basi tuweze kupata nyumba za Polisiā€¦

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Hamida kuna Taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Esther Matiko.

TAARIFA

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Nilikuwa nataka nimpe Taarifa Mheshimiwa Hamida kwamba, uhaba wa nyumba kwa Askari Polisi na Magereza ni Tanzania nzima. Pale Tarime mvua ikinyesha Askari Magereza anafanya kuhamisha godoro kutoka sehemu moja kupeleka nyingine na ni vijumba ambavyo vimejengwa toka enzi za mkoloni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nilikuwa nampa taarifa hiyo ili Serikali ione ni kwa namna gani itenge bajeti ya kutosha kuboresha makazi ya Askari Polisi kwa maana ya Magereza na wengine wote. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante. Mheshimiwa Hamida taarifa unaipokea?

MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Taarifa ninaipokea kwa sababu changamoto hiyo ni kubwa na ipo katika maeneo mbalimbali kama Mheshimiwa Mbunge alivyotolea taarifa, katika maeneo yote nchini Tanzania utakuta miundombinu mbalimbali imekuwa ni mibovu kwa hiyo, tunaomba Serikali kuhakikisha kwamba, kila mwaka wa fedha tunaendelea kupunguza changamoto ili hali ya ndugu zetu Jeshi la Polisi na Jeshi la Ulinzi na Usalama waweze kufanya kazi katika mazingira mazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la uhamiaji. Ninajua kwamba, Serikali imeendelea kujenga majengo ya ofisi za Uhamiaji katika kuhakikisha kwamba, tunatoa huduma mbalimbali katika Mikoa mbalimbali, lakini nimshukuru pia Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya muungano wa Tanzania kwa kutupatia fedha na kuweza kujenga Ofisi ya Uhamiaji ya Mkoa wa Lindi. Nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa kusimamia hilo, lakini changamoto iliyopo, bado vitendeakazi ni kizungumkuti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado tuna changamoto kubwa ya kutokuwepo magari. Hawa ndugu zetu wa Uhamiaji wana doria za mchana na usiku, ukisema Ofisi ya Mkoa maana yake wanatembea Wilaya mbalimbali kuhakikisha kwamba, wanaangalia mambo yanavyokwenda, kuona wavamizi ambao siyo raia wa Tanzania wanaendelea kuingia bila kuwa na passport. Kwa hiyo, ni suala sasa la Serikali kuona namna gani wanasaidia, kama tumeboresha ofisi zetu, basi sasa vitendea kazi viboreshwe katika Ofisi ya Uhamiaji Mkoa wa Lindi, tupatiwe magari ili waweze kufanya kazi usiku na mchana, lakini waweze kuhudumia wananchi ipasavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaipongeza Serikali kwa huduma ya utoaji wa Passport, imekuwa ni suala zuri sana. Changamoto nyingi zimepungua, hakuna usumbufu kama ambavyo miaka ya nyuma ilikuwa inatokea, tuongezee kuwapa vitendea kazi vya kisasa, kutumia mifumo ya TEHAMA na kuharakisha huduma. Siyo Afisa Uhamiaji anakusanya hapa makaratasi ya maombi anapeleka Dar-es-Salaam, badala yake angeweza kutia kwenye computer na yakaweza kufika Dar-es-Salaam wananchi wakashughulikiwa na wakatapa passport kwa wakati. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Hamida. Muda wako umeisha.

MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante naunga mkono hoja. (Makofi)