Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

Hon. Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nominated

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nikushukuru kwa kunipatia nafasi. Nianze na mimi kwanza kwa kuanza kuunga mkono hoja hii ya Bajeti ya Wizara yetu ya Ardhi na nimpe pongezi nyingi sana Waziri wa Ardhi pamoja na Naibu Waziri wa Ardhi na uongozi mzima wa Wizara hii kwa kuja na bajeti hii. Naamini itakuwa ni bajeti ya kihistoria, bajeti ambayo itaweza kutusaidia na kuweza kutoka, lakini zaidi kutatua migogoro mbalimbali na kuweza kuhakikisha kwamba tunakuwa na ardhi ambayo imepangwa, imepimwa lakini vile vile imeweza kumilikishwa vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nipongeze mpango walionao katika suala zima la usimamizi wa ardhi nikiamini katika fedha zile za mikopo, zitaweza kusaidia pia wanawake wengi zaidi kuweza kuwa na milki ya ardhi ambayo pia itaweza kuwasaidia wanawake wetu na vijana katika suala zima la uwezeshaji pia wananchi kiuchumi, hongereni sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza nitajikita zaidi katika suala zima la utatuzi wa migogoro. Tumeweza kuwasikia Waheshimiwa Wabunge na mna hoja ambazo ni za msingi tumezipokea. Hakuna hoja hata moja ambayo hatutaitilia maanani, tutaendelea kulifanyia kazi suala hili na kuhakikisha kwamba tunaendelea kushirikiana na wananchi lakini pia nanyi kama viongozi wao na wawakilishi katika suala zima la utatuzi wa migogoro hii yetu ya ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili tutaendelea pia kusimamia suala zima la utatuzi wa migogoro ya mipaka katika vijiji na vijiji, kata na kata, wilaya na wilaya lakini pia na mikoa, mmoja na mwingine kuhakikisha kwamba kila mmoja anajua mipaka yake sahihi na wananchi wetu wanajua pia wanaangukia katika eneo gani la mipaka, lakini kubwa zaidi kuweza kutatua migogoro ambayo kimsingi siyo ya lazima na ninaamini hili linawezekana kama ambavyo tumekuwa tukiendelea kufanya hivyo kwa kushirikiana na wenzetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tutaendelea pia kuweka mkazo katika suala zima la mipango ya matumizi bora ya ardhi kwa kushirikiana na Tume yetu ya Mipango ya Matumizi Bora ya Ardhi tumeendelea kufanya hivyo. Ukiangalia mfano katika Wilaya ya Ifakara tumeweza pia kupima muda siyo mrefu. Mwaka jana tu vijiji zaidi ya 30 lakini vilevile kwa upande wa Serengeti zaidi ya vijiji 33 na tunaendelea pia kutenga fedha na hata Ikungi muda siyo mrefu pia tumeendelea kushirikiana na halmashauri na wadau mbalimbali ikiwemo UN Women katika kuhakikisha kwamba tunaandaa mpango wa matumizi bora ya ardhi, lakini kubwa tunaendelea kutenga fedha na tumezielekeza halmashauri zetu ziweze kutenga fedha katika suala zima la Mpango wa Matumizi Bora ya Ardhi ili kuwa na matumizi sahihi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nipende tu kujikita pia katika eneo la Kamati za Mipango Miji; tunaendelea kusimamia Kamati zetu za Mipango Miji kuhakikisha kwamba kwanza zinafanya kazi kwa uadilifu, lakini vilevile kwa weledi unaokusudiwa kuhakikisha kwamba tunaenenda kwa mujibu wa sheria, kanuni, taratibu na miongozo mbalimbali ambayo ipo na kwa kamati zile ambazo zitaonekana pia hazitimizi wajibu wao ipasavyo hatutaendelea kusita kuzivunja na kuweza kuunda zingine. Lengo tu ni kuhakikisha kwamba kunakuwa na kamati ambazo kweli zina weledi, zina uadilifu lakini pia zinafanya kazi kwa ufanisi kuhakikisha kwamba hatuleti migongano na migogoro ambayo haina msingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee pia tu kulihakikishia Bunge lako tukufu, tunaweka mkazo katika suala zima la kupanga, kupima na kumilikisha kama mamlaka za upangaji kupitia halmashauri zetu na tushukuru sana Serikali yetu. Tumeweza kupata zaidi ya shilingi bilioni 42.3 ambazo tumeshazikopesha kwa halmashauri takribani 54 na mwelekeo ni kuhakikisha kwamba fedha hizi tunaweza kuzikopesha, lakini pia zimetengewa mfuko maalum, hazichanganyiki na fedha zingine za halmashauri ili ziweze kuwa na mzunguko na kuweza kupanga miji yetu vizuri zaidi, kuweza kumilikisha, lakini pia wananchi wetu waweze kupata hati au kupata milki ambazo zitakuwa salama na ambazo zimeweza kupimwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini mwisho kabisa niwahakikishie tu Waheshimiwa Wabunge kwamba kwa kushirikiana na Wizara yetu ya Ardhi tutaendelea kusimamia suala zima la usimamizi wa sekta yetu hii sekta ambayo ni muhimu sana katika uchumi, lakini vilevile katika suala zima la maendeleo ya jamii, lakini pia maendeleo ya kiusalama na mambo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nipende kusema naunga mkono hoja na ninashukuru kwa kupata nafasi hii. (Makofi)