Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge Kuhusu Mapendekezo ya Kurejea Katiba ya Tume ya Usafiri wa Anga ya Afrika ya Mwaka 2009

Hon. Innocent Edward Kalogeris

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Azimio la Bunge Kuhusu Mapendekezo ya Kurejea Katiba ya Tume ya Usafiri wa Anga ya Afrika ya Mwaka 2009

MHE. INNOCENT E. KALOGERIS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja iliyoko mbele yetu ya kuridhia Tume ya Katiba ya Usafiri wa Anga Afrika ya 2009.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie nafasi hii kuipongeza Serikali kwa kuleta Azimio hili ndani ya Bunge lako tukufu. Kubwa zaidi niseme neno moja tu kwamba naunga mkono azimio hilo lakini naunga mkono maazimio na ushauri uliotolewa na Kamati ya Miundombinu kwa Bunge lako tukufu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama walivyotangulia kusema wachangiaji waliotangulia, kwa kweli tumechelewa na katika kuchelewa kwetu naamini kabisa yako mambo mengine mazuri ambayo tumeyakosa sisi kama nchi kwa kuchelewa kujiunga na Tume hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie faida. Mojawapo ya faida kubwa ni kwamba, kama nchi tutakuwa katika mawasiliano ya uhakika ya usafiri wa anga na usalama wa anga letu kwa kujiunga na Tume hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile kama nchi tutakuwa tunapata faida kwa kupata teknolojia mpya za ulinzi na usalama wa anga letu kwa kujiunga na Tume hiyo kwa sababu moja. Kama Nchi Wanachama kuna fursa nyingi za mafunzo zitakuwa zinatolewa kwa ajili ya ulinzi wa anga letu. Kwa hiyo, sisi kama nchi tunaamini kabisa tutakuwa tumepata msaada huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama alivyosema ndugu yangu Mheshimiwa Mlaghila kwamba, kama nchi kupitia Tume hiyo tutakwenda kukuza Kiswahili chetu. Vijana wetu wataweza kupata ajira katika nchi hizo ambazo ni wanachama wa Tume hiyo na tutakuwa tumekuza lugha yetu ya Kiswahili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile, hapa tumeelezwa kwamba CAG ndiye Mkaguzi Mkuu wa Tume hiyo ya usafiri wa anga wa Afrika. Kwa hiyo, kwa namna moja au nyingine kama nchi tumepata heshima kubwa sana ya kwamba CAG wetu ameweza kutambulika katika Afrika na kwenda kukagua Tume kubwa ya Anga. Tuna kila sababu ya kukubaliana na hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika faida hizo pia nizungumzie hasara. Ni kweli kwamba tunazungumza kwamba tunapofungua anga Shirika letu la Ndege linaweza likamezwa, lakini naamini kwamba kadri tunavyokuwa tunakwenda, tutakuwa tunazidi kujipanua vizuri na tutalisaidia shirika letu, kwa sababu shirika letu pia linatakiwa litoke nje ya nchi na likafanye kazi katika nchi nyingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kutokujisajili wenzangu Wanayanga waliokwenda kule Algeria, walipata matatizo makubwa...

NAIBU SPIKA: Hivi hakuna mifano mingine mpaka huo tu? (Kicheko)

MHE, INNOCENT E. KALOGERIS: Mheshimiwa Naibu Spika, unajua Simba wasingepata shida hiyo kwa ajili ya uzoefu wa mechi za Kimataifa, lakini Wanayanga walipata shida kubwa sana, almost three hours walibaki pale uwanjani nchini Algeria wakifuatilia taratibu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niombe tu kwamba tusije tukaingia katika shida nyingine za hapa na pale na nyingine kama hizo. Turidhie na niwaombe na niwashawishi Waheshimiwa Wabunge wenzangu kwamba jambo hili ni jepesi wala halina mashaka yoyote. Faida ni kubwa kuliko hasara ambazo tunajaribu kuzionesha. Niwaombe na nishauri Bunge lako turidhie na tuingie katika Mkataba huu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)