Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari

Hon. Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Naibu Spika, nachukua nafasi hii kuungana na Watanzania wenzangu wote kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kutujalia baraka zake katika nyanja mbalimbali za ustawi wa kijamii, kiuchumi, kisiasa, kidiplomasia pamoja na mambo mengi sana katika Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nachukua nafasi hii kuungana na wananchi wa jimbo langu la Mbulu Mjini kumpongeza sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Philip Mpango, Makamu wa Rais, Mheshimiwa Waziri Mkuu na Serikali nzima ya Awamu ya Sita kwa jinsi anavyoliongoza Taifa letu na kutupatia fedha nyingi sana za miradi ya maendeleo kwani miradi inayotekelezwa hivi sasa ni mikubwa sana ambayo ni utekelezaji wa Ilani ya CCM 2020-2025.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimpongeze sana Mheshimiwa Dkt. Tulia Ackson, Spika wetu, wewe mwenyewe Mheshimiwa Naibu Spika, Wenyeviti wa Bunge letu kwa jinsi mnavyoliongoza Bunge hili toka tulivyoanza, hongereni sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa namna ya pekee nampongeza Mheshimiwa Nape Nnauye – Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mheshimiwa Engineer Mathew Kundo - Naibu Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari na watendaji wa Wizara na taasisi zilizoko chini ya Wizara hii muhimu kuendana na utendaji wao wa kila siku, hongereni sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba kutoa mchango wangu kuishauri Serikali kupitia mapendekezo ya bajeti ya Wizara hii muhimu sana kupitia hotuba ya Waziri na maoni na mapendekezo ya Kamati yetu ya Kudumu ya Bunge.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza Serikali iangalie utaratibu wa kuboresha minara yetu ya TTCL kwani tuna minara mingi ya TTCL ina uwezo wa chini kupokea usikivu wa mawasiliano hali ambayo inawafanya wananchi wengi kutokutumia mitandao yetu ya TTCL kuliko mitandao mingine ya simu. Hivyo basi ushauri wangu timu ya wataalam wetu wa Wizara wafanye tathimini ya minara yote ya TTCL kwa lengo la kufanya maboresho ya usikivu na kuleta ushindani na minara ya mitandao mingine kwa ajili ya kujibu kiu ya watumiaji wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa kuwezesha masomo ya TEHAMA katika shule zetu za sekondari nchini hasa zile za A-level tunaiomba Wizara hii kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) kuzipatia shule hizi computers ili kuwezesha wanafunzi wetu wa shule za sekondari za kata waweze kijifunza TEHAMA na kushindana na wanafunzi wenzao wa shule binafsi na kuwajengea uwezo wa kufahamu kikamilifu matumizi ya TEHAMA kabla ya kuhitimu masomo ya sekondari.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Serikali yetu idhibiti sms za utapeli zinaotumwa kupitia line za simu zetu za TTCL na matapeli kuomba hela kwa wananchi kwa kuwa hapo awali line za simu mitandao mingine zilikuwa zinatumika, ni dhahiri kuwa walifanya maboresho katika kukomesha tatizo hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja na naomba kuwasilisha.