Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari

Hon. Joseph Zacharius Kamonga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ludewa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari

MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia mjadala wa bajeti hii. Nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais. Nampongeza sana kwa kuwa kazi anayoifanya kwenye eneo hili ni kubwa sana ni lazima tuweze kumpongeza. Vilevile nampongeza sana Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Nape Nnauye, Mheshimiwa Naibu Waziri wake, Mheshimiwa Kundo na taasisi zao zote. Kuna TCRA, kuna UCSAF, kuna yule dada yangu Justina, kwa kweli anafanya kazi nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninachomshukuru Mheshimiwa Nape, kwa sababu anapafahamu pale Lupingu kuna mwaka alienda akiwa Mwenezi wa Chama Taifa, na nilipoenda kumwomba mnara wa simu, alimtuma Naibu wake tukaenda mpaka pale wakapanda boti mpaka sehemu inaitwa Igha. Aliwaahidi wananchi wale kwamba atawasha mnara mapema. Nitumie nafasi hii kuishukuru sana Serikali, sasa hivi Kata yote la Lupingu, wananchi hata wakiwa kwenye maji wanavua Samaki, wanaweza kuwasiliana. Likitokea tatizo lolote, ajali yoyote, mawasiliano yanakuwa ya mapema kwa sababu kuna mnara pale ambao unaweza kusaidia kutoa taarifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii ni ishara kwamba wizara hii inatambua kwamba mawasiliano ya simu siyo anasa, ni hitaji la muhimu kwa dunia ya leo, wananchi wanatumia kwa manufaa mbaliambali kuweza kupeana habari kwa ajili ya biashara mbalimbali, fursa mbalimbali kupitia mitandao ya simu. Vilevile kwenye shule zetu za msingi, walimu wanasajili wanafunzi wa Darasa la Saba kwa kutumia mitandao ya simu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda kule, zahanati zetu hii mitandao inatumika kwa ajili ya matumizi ya shughuli za kila siku. Kwa hiyo, na kule Ludewa maeneo mengi ambayo yako pembezoni tuna zahanati nyingi ambazo zinahitaji mawasiliano ya simu. Tuna shule za msingi zaidi ya 100 ambao walimu walikuwa wakitembea umbali mrefu sana kwenda kusajili wanafunzi wale wa Darasa la Saba. Nafurahi kwamba tokea nimekuwa Mbunge Serikali hii ya awamu ya sita imeweza kunisaidia kupata minara 15.

Mheshimiwa Naibu Spika, tulipata mnara pale Madope, tayari unafanya kazi; tulipata mnara Kijiji cha Ilawa Kata ya Madilu, unafanya kazi; Tulipata mnara Mkongobaki, Ibumi, Lupanga na Galawale pale Kata ya Ludewa ambao unahudumia hadi Nindi kule; Kuna mnara Mkumbili, kuna mnara Mkomangā€™ombe, Mapogoro ambao unaenda kujengwa sasa mnara wa Tigo; kuna mnara Shaurimoyo na Mdiligili ambao unakwenda kujengwa sasa wa Vodacom; kuna mnara Kitowele; na Lupande ambao unakwenda kujengwa sasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri, hapa Lupande alikwenda, alifanya mkutano na aliwaahidi wananchi kwamba atakwenda kujenga mnara, Serikali itapeleka mnara pale. Kwa hiyo, nafurahi sana siku ya utiaji saini mikataba ile 758 mimi nilikwenda pale kwa niaba ya wananchi wa Ludewa na niliona hawa wananchi wa Kitewele na Lupande sasa watakwenda kupata mnara kama ambavyo Mheshimiwa Waziri aliweza kuahidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo tunapata mnara ni Mapogoro, mnara wa Tigo, kuna eneo la Ludende mnara wa Vodacom, kuna Iwela tumepata mnara wa TTCL na Igalu. Kwa hiyo, nitumie nafasi hii kwa niaba ya wananchi wa Ludewa kuishukuru sana sana Serikali. Hata mimi Mbunge mmenipa heshima sana, nikipita kwa wananchi naonekana Mbunge wa maana kwa sababu ya Mheshimiwa Nape Nnauye na Serikali ya Awamu ya Sita. Kwa sababu kule kwetu minara ilikuwa changamoto kubwa sana ila sasa hivi kwa mwendo huu, naamini tutafika mbali zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie fursa hii kuiomba Serikali iendelee kuangalia ile Kata ya Ibumi, eneo lile lina utajiri mkubwa wa madini, kuna migodi mikubwa inaenda kuanza pale. Kwa hiyo, mawasiliano yatakuwa muhimu sana hasa Kijiji kile cha Masimavalafu, kuna reserve kubwa sana za copper na makaa ya mawe, kwa hiyo, kuna wawekezaji kule. Naishukuru Serikali mwaka huu kupitia TAMISEMI, wataenda kutujengea daraja pale ambalo linaunganisha Kata ya Ibumi na Kata ya Itumbandyosi ambayo iko kule kwa Mheshimiwa Benaya. Kwa hiyo, maeneo haya, mawasiliano yatakuwa muhimu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba sana Kijiji kile cha Masimavalafu kiweze kupata mawasiliano ya simu. Tunao mnara pale wa TTCL na umewashwa kipindi nikiwa Mbunge, kwa hiyo, naishukuru sana Serikali, lakini coverage yake bado ni ndogo. Siku ile niliongea na Mkurugenzi yule wa TTCL akaniahidi atatuma wataalam. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri naomba sana msaada wako, hawa watu wa TTCL waweze kwenda pale kuongeza uwezo wa ule mnara ili uhudimie kile Kitongoji kile cha Nyamalamba na maeneo jirani.

Mheshimiwa Naibu Spika, halikadhalika, Tarafa ya Mwambao Kijiji cha Lumbila Kata yote ya Lumbila, Kata ya Makonde na Kata ya Kilondo, wana mnara ule wa Halotel ambao nao kama ambavyo Waheshimiwa Wabunge wameeleza, unategemea teknolojia ya umeme wa jua (solar). Sasa kukiwa na hali ya hewa kidogo ya mawingu mawingu, wananchi wanakosa mawasiliano. Kabla ya Mheshimiwa Naibu Waziri wataalam walishaenda na vipimo wakaweza kutambua maeneo yote. Kwa hiyo naomba tu utekekelezaji ufanyike. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hayo machache, nashukuru sana. Naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)