Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari

Hon. Francis Kumba Ndulane

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari

MHE. FRACIS K. NDULANE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia katika Wizara hii ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari. Kwa ujumla ninapenda kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu Dokta Samia Suluhu Hassan kwa jinsi ambavyo anashughulikia ipasavyo utatuzi wa kero mbalimbali na changamoto mbalimbali za wananchi wetu wa Tanzania katika tasnia hii ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia napenda nimpongeze sana sana sana Ndugu yangu Nape Moses Nnauye ambaye leo ningependa kumtunukia mimi binafsi cheo cha ujemadari. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Jimbo langu la Kilwa Kaskazini miaka 118 iliyopita ililshuhudia majemadari 30 wakiongoza Vita vya Majimaji kwa ajili ya kutokomeza ukoloni wa Wajerumani. Leo nimeamua kumtunukia ujemadari Nape Moses Nnauye siyo kwa ajili ya kutupa mikuki dhidi ya wakoloni, bali ni kwa ajili ya kupambana na adui ujinga, umaskini na maradhi kupitia tasnia ambayo anaiongoza ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari. Bila tasnia hii kusimamiwa vizuri, adui ujinga, maradhi na umasikini hawezi kuondoka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeshuhudia wiki moja iliyopita Serikali yetu imesaini mikataba kwa ajili ya ujenzi wa minara 758 katika Kata 713 hapa nchini. Hili ni tukio kubwa la kimapinduzi ambalo linakwenda kuipeleka nchi yetu katika mstari wa mbele kabisa wa maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilipoingia madarakani kwa nafasi ya Ubunge, Jimbo langu la Kilwa Kaskazini lilikuwa na vijiji 22 ambavyo vilikuwa havina mawasiliano ya simu lakini ndani ya mwaka mmoja ilipofika mwaka 2021 Serikali iliweza kutujengea minara minne katika Vijiji vya Pungutini, Nandete, Chapita na Mwengei. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeshuhudia juzi Serikali imeingia mkataba na kampuni mbalimbali kwa ajili ya ujenzi wa minara ya simu. Napenda nikutaarifu, sisi Wilaya ya Kilwa tumepata minara 15 ambayo itajengwa katika vijiji 21 vya Wilaya ya Kilwa, na jimbo langu litapata minara minane ambayo itaweza kutoa mawasiliano katika vijiji vipatavyo 10. Kwa hiyo, ukichukua ile takwimu ya vijiji 22, ukitoa vile vinne vya mwaka 2021, ukitoa hivi 10 ambavyo vinaenda kupata huduma ndani ya miezi tisa ijayo, tayari tutakuwa na vijiji vipatavyo vinane, ndiyo vitabaki kuwa havina mawasiliano ya simu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli naipongeza Serikali kwa kuweza kufanya kazi kubwa ndani ya kipindi kifupi. Ndiyo maana nimempa huu wadhifa wa ujemedari ndugu yangu Mheshimiwa Nape Moses Nnauye. Hongera sana Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba maeneo yafuatayo yazingatiwe katika utekelezaji wa hii miradi ya ujenzi wa minara 15. Katika jimbo langu kuna Kijiji kinaitwa Zinga Kibaoni kimeainishwa kwamba nacho kitapelekewa mnara. Hiki kijiji ni kipana sana. Uki-calculate ile dimension ya kijiji toka kona moja mpaka nyingine, ni zaidi ya kilometa 40. Sasa tayari pale katikati ya kijiji kuna mawasiliano ya Halotel. Kuna kitongoji ambacho kina watu wengi zaidi kinaitwa Nambunju, naomba mnara huu upelekwe Nambunju. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna Kijiji inaitwa Namatewa, kinajengewa minara miwili, lakini wakati huo Makao Makuu ya Kata hakuna mnara hata mmoja uliojengwa pale Kandawale. Kwa hiyo, naomba mnara mmoja ambao ulikuwa ujengwe Kandawale na Airtel upelekwe Kandawale ili pale Namatewa ubaki mnara mmoja. Naomba hilo lizingatiwe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna changamoto katika ile minara minne ambayo ilijengwa mwaka 2021 katika Vijiji vya Pungutini, Nandete, Mwengehi, pamoja, Chapita, pamoja na Kijiji cha Mtopera. Ile minara inatumia teknolojia ya solar kwa ajili ya kuipa nguvu iweze kufanya mawasiliano. Hili limesababisha changamoto kwa ile minara kuweza kufanya kazi kwa masaa yasiyozidi 10 kwa siku, na matokeo yake kumekuwa na malalamiko mengi. Kwa sababu mwingine anaweka bundle litatumika masaa 24, lakini mwisho wa siku ndani ya masaa 14 ya saa hizo 24 mawasiliano yanakuwa hayapo na wakati bado bundle lake lilikuwepo kwenye simu. Matokeo yake anashindwa kupata haki yake ya kutumia lile bundle mpaka liweze kwisha. Kwa hiyo, naomba Serikali iunganishe hii minara yote na mtandao wa umeme wa REA ambao upo katika hatua za mwisho za kukamilisha katika hivyo vijiji vyote nilivyovitaja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nivitaje vijiji vinane ambavyo vimebaki ambavyo havitakuwa na mawasiliano ya simu baada ya mradi huu wa maeneo 15 kukamilika. Vijiji hivyo ni vya Hanga, Kinywanyu, Ingirito, Kongwe, Marendego pamoja na Namanungutungu na pia kipo Kijiji cha Nandombo pamoja na Kijiji Nambondo. Naiomba sana Serikali katika awamu ijayo ya ujenzi wa minara hivyo vijiji vinane vifikiriwe ili tuweze kupata mawasiliano mwanana jimbo zima na wilaya nzima ya Kilwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho kabisa naipongeza TBC kwa kazi kubwa wanayoifanya, na nimeona jana pale nilipokuwa napita kwenye banda lao, wamelenga kujenga kituo kikuu cha mawasiliano ya TBC katika Wilaya ya Kilwa pale Nangurukuru. Naomba kazi hiyo iendelee ifanyike kwa haraka kwa sababu kuna changamoto kubwa ya Mawasiliano ya TBC.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Kengele ya pili hiyo Mheshimiwa.

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. Ahsante sana. (Makofi)