Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

Hon. Francis Kumba Ndulane

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nitangulie kukushukuru wewe kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia bajeti ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, jioni ya leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili ninapenda kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu kwa namna ambavyo kwa haraka sana ameleta mabadiliko katika kuisimamia Wizara hii ambayo leo tunaijadili bajeti yake. Pia nampongeza Mheshimiwa Waziri Dada yangu, Mheshimiwa Angeline Mabula kwa kazi nzuri anayoifanya kwa kushirikiana na Naibu Waziri wake pamoja na watendaji katika Wizara yake pamoja na watendaji katika taasisi mbalimbali zilizo chini yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuanza na takwimu. Katika sensa ya nchi yetu mwaka 2012 tulikuwa na watu milioni 44.9. Miaka kumi baadaye, yaani mwaka 2022 wananchi wetu waliongezeka hadi kufikia milioni 61.9 na kwa mujibu wa projection iliyopo, tunatarajia ifikapo 2025 wananchi wetu watakuwa milioni 67.9 na mwaka 2050 tunatarajia idadi ya watu katika nchi yetu ya Tanzania itakuwa milioni 151.2. Katika watu hao milioni 151.2 inatarajiwa asilimia 48 watakuwa wanaishi katika miji mbalimbali hapa nchini, kutokana na watu wengi wanaohamia katika miji lakini wanaozaliwa pia katika miji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia katika Jiji letu la Dar es Salaam ndilo jiji ambalo linaongoza kwa sasa kwa kuwa na idadi kubwa ya watu, ikiwa na watu milioni 5.4 kwa mujibu wa sensa ya mwaka 2022 na inachukua asilimia 8.7 ya wananchi wote wa nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kwa kusema, kwa mujibu wa taarifa za kiuchunguzi za UN zinaonesha kwamba Jiji letu la Dar es Salaam ni la tatu kwa kuwa na ongezeko kubwa la wananchi kwa mujibu wa Sensa ya Mwaka 2022. Pia kwa mujibu wa taarifa hizo hizo za UN, inaonesha kwamba nchi yetu ya Tanzania inakadiriwa ifikapo mwaka 2100 itakuwa ni nchi ya tisa yenye watu wengi hapa duniani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimetoa takwimu hizi makusudi ili mwone kwa namna gani tunatakiwa kujipanga katika kuhakikisha wananchi wetu tunawapatia makazi muhimu na Madhubuti. Ni lazima tuwe na mpango madhubuti wa makazi kwa wananchi wetu hasa wananchi wa hali ya chini wakiwemo watumishi pamoja na wale ambao wanafanya shughuli nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwezi uliopita Kamati yetu ya PIC (Kamati ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma) ilitembelea miradi inayosimamiwa na Taasisi yetu ya NHC. Kwa kweli tuliona mambo mazuri. Mheshimiwa Rais wetu amefanya mambo mazuri, amepeleka fedha nyingi kwa ajili ya uendelezaji wa ujenzi wa mradi wa nyumba pale Morocco Square na pia pale Kawe Seven Eleven, miradi ambayo ilisimama kwa muda mrefu. Nampongeza Mheshimiwa Rais, naipongeza Wizara kwa kazi nzuri inayoendelea katika ile miradi miwili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna mradi mpya wa Samia Housing Scheme ambao unasimamiwa pia na watu wa National Housing, lakini ukiiangalia ile miradi na matarajio ya pesa zitakapouzwa zile apartments, kwa kweli ni fedha nyingi sana watahitaji kulipa wale watu ambao watanunua zile nyumba. Kwa hiyo, sioni nafasi ambayo Serikali imetoa kwa ajili ya uwekezaji kwenye nyumba za watu wa kawaida au watu wa hali ya chini kama watumishi wenye vipato vidogo vidogo, wakulima wadogo wadogo, wafanyabiashara wadogo wadogo na watu wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, miaka ya mwanzoni kabisa mwa Uhuru tulishuhudia viongozi wetu, waasisi wa Taifa letu akiwemo Mzee wetu Abeid Amani Karume pamoja na Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere wakiwekeza kwa kiasi kikubwa kwa wananchi wa vipato vya chini. Kwa hiyo, naiomba Serikali, turudi katika ule mwanzo mzuri ambao walituanzishia waasisi wetu. Pale Magomeni kulikuwa na sehemu ile ambayo sasa inaitwa Magomeni Mapipa, nyumba zilikuwa zikiezekwa kwa mapipa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda pale Magomeni Quarters kulikuwa na nyumba zilikuwa zimeezekwa kwa makuti, lakini Hayati Baba wa Taifa akasema Hapana, ni lazima twende na mkakati wa kuanzisha nyumba ambazo wananchi watakodishwa au kukopeshwa kwa masharti nafuu. Watakuwa katika utumishi wao na mwisho wa utumishi wao watakuwa tayari wanajimilikia zile nyumba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo kuna hali inayojitokeza ambayo wananchi wetu hasa watumishi wa hali ya chini wamejikuta wakijenga nyumba baada ya kupata kipato chao cha kustaafu, wengine wanajikuta sasa wanatumia ile hela yote na kikokotoo kimebadilika sasa hivi, kwa hiyo, unajikuta wanatumia hela yote kujenga nyumba na hawamalizi, kwa hiyo mwisho wa siku wanabaki na stress, wanakufa mapema na mwisho siku ni lazima sasa tuone namna ambavyo tutatengeneza hii skimu mpya ambayo itawasaidia watu wa kipato cha chini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata kule Zanzibar kulikuwa na magorofa ya Michenzani yalijengwa na Hayati Abeid Karume kwa ajili ya kuwasaidia wananchi wa kipato cha chini. Kwa hiyo, rai yangu kwa Wizara yetu, twende tukabuni revolving fund ambayo itapelekwa kwenye taasisi zetu ambazo zimehusika na ujenzi kama NHC, TBA pamoja na Mwananchi Housing ili waweze kujenga nyumba za aina hiyo, wananchi waweze kukopeshwa kwa bei nafuu wakiwa ndani ya utumishi wao, wakiwa na nguvu zao ili wanapofika umri fulani, basi wanamilikishwa zile nyumba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaweza tukatumia kwa mfano vifaa vya ujenzi tukaweka mle charge kidogo. Kwa mfano, kwenye cement kila mfuko wa cement tukiweka kwa mfano Shilingi mia moja, mia moja, mifuko mingapi ya cement inazalishwa hapa nchini kwenye viwanda vyetu? Tutajikuta tuna hela nyingi ya kuweza kuhudumia hao wananchi, na hiyo population ambayo tunatarajia ikue mpaka kufikia 2100.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nilifikiri kwamba kuna sheria nyingine za umilikaji wa ardhi zimepitwa na wakati pamoja na mali. Kwa mfano, sasa hivi mwananchi ambaye sio raia wa Tanzania haruhusiwi kumiliki ardhi katika nchi ya Tanzania. Sikusudii hapa kuzungumzia suala ya uraia pacha (duo citizenship), ninachoweza kuzungumza hapa ni kwamba, kama mtu anauwezo wa kuja kujenga apartments katika nchi yetu ambazo zitawasaidia wananchi wetu, zile nyumba hawezi kuondoka nazo, hata kama yeye sio raia wa nchi hii. Tuliona kule Dubai, ona leo Zanzibar, mambo haya yanaendelea, yanafanyika vizuri kabisa. Watu wanaruhusiwa kuwekeza, wanajenga majumba, na watu wanakodi, wengine wananunua, maisha yanaendelea, yanazidi kuboreka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili tuweze kuihudumia ile population ya mwaka 2001 ni lazima twende na hii mikakati…

MHE. ALI JUMA MOHAMED: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Ndulane, kuna taarifa.

TAARIFA

MHE. ALI JUMA MOHAMED: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpe taarifa mchangiaji. Kwa Hayati Mzee Karume, alizijenga nyumba hizi ambazo amezizungumza mchangiaji, mijini na vijijini zote zikiwa na hadhi moja. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Ndulane, taarifa unaipokea?

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Namshukuru ndugu yangu hapa, Mheshimiwa Ali, kwa kweli naipokea taarifa yake kwa asilimia 100. Kwa hiyo, naomba tuliangalie hili jambo katika Wizara yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu ambalo napenda kulizungumzia ni kuhusu matumizi bora ya ardhi katika Wilaya yangu ya Kilwa, maana yake usije ukasemea Taifa halafu mwisho wa siku ukajikuta wewe kwako hujisemei.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mpango wa matumizi bora ardhi, mwaka uliopita tulipitisha bajeti ya Shilingi bilioni 205, ilisomwa hapa, lakini baadaye ilirekebishwa, ikaongezwa hadi kufikia Shilingi bilioni 300. Kwa kweli Serikali ilifanya jambo zuri, lakini nasikitika kusema, katika vijiji kumi na moja ambavyo Wilaya yetu ya Kilwa ilitakiwa kuvipima katika mpango huu wa matumizi bora ya ardhi kupitia fedha zile ambazo niliomba hapa kwa kilio, bahati mbaya sisi wengine hatuna uwezo wa kuruka sarakasi, wala kupiga magoti, wala kulia ndani ya Bunge, ni wavumilivu sana, lakini zile pesa hazijafika hadi kufikia wakati huu. Naiomba Wizara, katika huu mwezi mmoja uliobaki ituletee fedha, tuendelee na upimaji na kuboresha mpango wa matumizi bora ya ardhi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, kulikuwa na mgogoro katika Kijiji cha Mtepela na katika utatuzi wa huo mgogoro tulijitahidi mimi pamoja na Mheshimiwa Diwani wangu wa Kata ya Miguruwe kusuluhisha. Pia Kamati ya Mawaziri nane ilifika, lakini kikubwa walichosisitiza pale wale Mawaziri, ni suala la ulinzi wa maji katika chanzo cha Mto Matandu. Mambo mengine hayakuzungumzwa, lakini juzi tumeona, wafugaji wanaambiwa ifikapo mwakani wawe wameondoka, wakulima ifikapo mwezi ujao, Julai tarehe 30 wawe wameondoka. Naomba, kabla ya utekelezaji wa kuwaondoa wale wananchi wa Kijiji cha Mtepela pale, basi uwepo mpango madhubuti wa kulipa fidia pamoja na kuzingatia mambo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha. Naunga mkono hoja. (Makofi)