Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

Hon. Joseph Zacharius Kamonga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ludewa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia bajeti hii ya Wizara ya Ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote niungane na Wabunge wenzangu wote waliompongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kutoa kipaumbele kwenye sekta hii ya ardhi. Hali kadhalika nimpongeze sana Mheshimiwa Angeline Mabula, Waziri wa Ardhi na mlezi wangu, nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri na wataalamu wote wa sekta hii ya ardhi. Nitakuwa pia mchoyo wa fadhila nisipo mpongeza Mthamini Mkuu, mthamini amesimamia zoezi la uthamini wa fidia vizuri kule Ludewa; aliitwa kwenda kuhakiki akaenda na wataalamu wake, na hivi sasa ninavyozungumza wananchi wanalipwa fidia ya bilioni 15.4. Kwa hiyo niipongeze sana Wizara kwa kazi nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi niombe pia waweze kushirikiana na watu wa NDC na Wizara ya Viwanda na Biashara. Upimaji ule uliofanyika kule Liganga na Mchuchuma kulikuwa na haki mbili. Kulikuwa na mineral right yaani zile leseni za madini na kulikuwa na land right, hati za umiliki wa ardhi. Sasa, mwekezaji alimiliki eneo kubwa la ardhi lakini ulipaji wa fidia alipunguza eneo lake atakalofanya uwekezaji, na lile eneo jingine ambalo halijalipiwa fidia tulitaka tulipange tutoe hati kwa wananchi ili nao waweze kunufaika na mradi. Kwa hiyo naomba sana Mheshimiwa Waziri ili kuepusha mgongano na wananchi wataalam wawahi mapema sana, nina imani sana wanaweza wakafanya vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unajua mpira mtu anaweza akaucheza vizuri akiwa nje ya uwanja, ukiwa nje unaweza kuwa na mawazo mazuri zaidi kuliko wachezaji walioko ndani; lakini na wewe ukipewa nafasi uende kucheza utaona pale unakuwa kituko. Sekta ya ardhi ni tofauti sana na tunavyo ichukulia. Sekta hii ina sheria nyingi sana, na zote za muhimu. Lakini mpaka hati ije kutengenezwa kuna hatua nyingi za kupitia na kuna wataalamu wengi wanahusika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nashukuru nimebahatika kufanya kazi kwenye sekta hii ya ardhi kwenye Wizara ya Ardhi kwa muda usiopungua miaka kumi. Katika kipindi hicho nimesimamiwa na kufundishwa kazi na wengi na mimi nimesimamia na kufundisha kazi wengi; kwa hiyo nina ufahamu mkubwa wa sekta hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna kazi zile za kuandaa mpango kabambe (master plan) ikishaandaliwa ile waje wale watu wa mipango miji. Na master plan ile inakuwa ni shirikishi, inahusisha watu wengi zaidi. Wanakuja watu wa mipango miji, anachokifanya Afisa Mipango Miji, mpima ardhi hawezi kukifahamu na hawezi kufanya. Ni taalum mbili tofauti wote wanakaa darasani miaka miwili mitatu minne wanafundishwa, na anachokifanya Afisa Ardhi ni kazi tofauti. Ndiyo maana kuanzia ukurasa wa 30 wa hotuba ya Mheshimiwa Waziri, nilikuwa naisoma, ameainisha pale eneo la uandaaji wa mpango kabambe (master plan), uandaaji wa mipango kina, upimaji wa ardhi, umilikishaji, na mambo ya utatuzi wa migogoro. Kwa hiyo kuna vipengele vingi ambavyo ni muhimu sana ningeomba ikiwezekana wizara iweze kutoa mafunzo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kuna kitu pia nimekibaini, tunachanganya sana upimaji wa vijiji na upimaji wa mashamba ya wananchi na utoaji wa hati milki za kimila. Baadhi ya Waheshimiwa Wabunge tunachukulia kwamba upimaji wa vijiji ndio huohuo upimaji wa mashamba ya wananchi na utoaji wa hati miliki za kimila. Kwa hiyo haya maeneo ningeomba Wizara iweze kukutupa semina za kutosha ili tuweze kuwa na uelewa ili tunavyoishauri tuweze kutoa ushauri ambao uko sahihi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitatoa mfano. Kwenye upimaji wa mipaka ya vijiji hili linanyika sana wakati ule inavyokuja sensa labda ya watu na makazi au uchaguzi, wanapotaka kuzaliwa vijiji vipya; au wakati wowote Ofisi ya Rais TAMISEMI wanavyo kuwa wanaongeza vijiji. Sasa, inatakiwa wananchi wakae wakubaliane mipaka ndipo wataalamu waweze kwenda kuweka mipaka hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na eneo hili ningeiomba Wizara ipunguze kutumia mipaka ile ya asili kama mito na milima, kwa sababu mazingira ya kijiografia yanabadilika. Kuna mito inakauka, kuna mito inahama. Kwa hiyo ni vizuri wakaweka zile bicorn kubwa kama ambavyo mmeweka kwenye mipaka ile ya kule kwenye hifadhi, na kule kwenye mipaka ya nchi. Zile nguzo ni kubwa zimefyatuliwa pale, mwananchi yeyote anaweza kuona, kwa sababu tukitegemea mto kuna wakati mwingine mto unahama. Kwa hiyo ni muhimu sana tukafyatua nguzo kubwa za bicorn ili wananchi wasije wakaingia kwenye migogoro. Kila mwananchi akiona anajua kwamba hapa ni mpaka wa kijiji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye mipango ya matumizi bora ya ardhi niipongeze sana wizara imejitahidi kadri ya uwezo wake, imejitahidi sana; na Tume ya Mipango ya Matumizi Mora ya Ardhi nayo imejitahidi kufanya kazi vizuri. Niishukuru Serikali, mwaka jana wakati wa bajeti mara ya kwanza tuliweka ile bilioni 205 lakini zikaongezwa zaidi ya hizo ili angalau waweze kupima vijiji vingi zaidi. Kwa hiyo naomba sasa wataalamu wetu waweze kwenda kuandaa mipango ya matumizi bora ya ardhi kwenye vijiji ambavyo vimepangwa kutekelezewa mradi huo, wapime mashamba ya wananchi na kutoa hati miliki ya kimila.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile sijui tutatumia njia gani, bado baadhi ya maeneo hati miliki ya kimila haina uzito sana, mwananchi akienda benki kuomba mkopo wa trekta bado haitambuliki sana. Sasa sijui tutatumia njia gani kuweza kuelimisha taasisi zinazotoa mikopo kwa wananchi waweze kuitambua vyema hati ya haki miliki ya kimila.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo tunavyopima maeneo mengi zaidi kwenye nchi yetu na kutunza kumbukumbu za wamiliki vizuri tunapunguza muda wa kutatua migogoro wa ardhi. Mwananchi akija kama kumbukumbu ziko vizuri za mwananchi ni rahisi kumpa majibu. Kwa hiyo ni muhimu sana, Waheshimiwa Wabunge wanavyoshauri maeneo mengi katika nchi hii yaweze kupimwa na kutolewa hati miliki ni ushauri ambao ni mzuri sana ambao wizara haina budi kuufuata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeomba Serikali iongeze zaidi fedha na itoe kibali kwa Wizara hii kuweza kuajiri watumishi wa kutosha, kwa sababu wizara hii ina upungufu mkubwa sana wa watumishi, haijaajiri muda mrefu. Kwa hiyo ni muhimu sana Serikali Ofisi ya Rais Utumishi wa Umma wakawapa kibali waweze kuajiri; kwa sababu vyuo vipo vijana wako mtaani hawana ajira na wana uwezo na wana utayari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naangalia takwimu, inaonesha watumishi waliopo hawazidi asilimia 30, kwa hiyo upungufu ambao upo kwenye Wizara hii ni zaidi ya asilimia 70, kwa hiyo ni pengo kubwa sana, hivyo tusitarajie miujiza kwa idadi hii ya upungufu wa watumishi. Kwa hiyo naomba Serikali iweze kuajiri watumishi wa kutosha. Na kwa eneo la Dodoma nimeona Mheshimiwa Waziri amejaribu kuelezea pale kidogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nilikuwa hapa Dodoma. Dodoma inabidi ichukuliwe kwa namna nyingine tofauto, kwa sababu moja, tangu mwaka 1973 kulikuwa na Mamlaka ya Ustawishaji Makao Makuu CBA. CBA walikuwa na sheria tofauti walikuwa hawatumii Sheria ya Ardhi Namba Nne. Walikuwa hawafuari sana Sera ya Taifa ya Ardhi, walikuwa na taratibu zao ziko tofauti. Kwa hiyo baada ya kuvunjwa ndipo sasa tuka-switch, na mimi ndiye niliyekuwa Afisa Ardhi wa kwanza kuja kubadilli mfumo. Changamoto kubwa niliyokuwa nakutana nayo moja ni kutofautiana kwa sheria. Kwa hiyo tuangalie namna ya kuziba gap katika eneo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini vilevile Dodoma baada ya Makao Makuu kuja ardhi ilipanda sana thamani. Mahitaji ya ardhi yakawa mengi, na upimaji wataalam wamejitahidi wana viwanja, najua saa hivi wanakwenda kwenye milioni moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni vizuri Wizara ikaaangalia uwezekano wa kuongeza Kamishna mwingine wa ardhi hapa Dodoma. Kamishna mmoja mtamuua kabla ya siku zake, atazeeka kabla ya wakati wake. Kwa hiyo ateuliwe Kamishna mwingine wa ardhi ili aweze kusaidiana majukumu na Kamishna aliyepo namna ya kugawa majukumu Kamishna wa hapa atajua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, naunga mkono hoja.