Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

Hon. Michael Constantino Mwakamo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibaha Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru nami kupata nafasi ya kuchangia kwenye Wizara hii ya Ardhi. Kwanza kabisa, naungana na wenzangu kutoa shukrani kwa Mheshimiwa Rais, kwa namna ambavyo anaendelea kulihudumia Taifa, lakini kwa maslahi mapana ya wanajimbo la Kibaha Vijijini, namshukuru yeye kwa kutenga pesa nyingi na kuendeleza Mji wa Kwala ambalo limewekwa kongani kubwa ya viwanda ambayo inakwenda kujengwa katika eneo lile na kuufanya Mji wa Kwala kuwa mji mkubwa kabisa katika Miji ya Tanzania. Pia nampongeza Mheshimiwa Waziri kwa namna ambavyo anaendelea kupambana na changamoto mbalimbali anazokabiliananazo ambazo zinaelezwa na Wabunge mbalimbali kutoka katika kila Jimbo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nitakuwa na maeneo machache sana ya kuchangia kwenye eneo hili. Eneo langu la kwanza ambalo nitapenda kuchangia ni eneo la utawala wa ardhi. Tunafahamu sehemu ya utawala wa ardhi inahusisha mambo kadhaa ikiwemo masuala mazima ya migogoro ya ardhi, ugawaji wa ardhi, usimamizi wa masharti ya umilikishwaji pamoja na usajili wa hatimiliki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, najielekeza kwanza kwenye eneo hili la migogoro. Naomba nitumie hadhara hii kuwasilisha migogoro ambayo inapatikana jimboni Kibaha. Nimesukumwa kufanya hivi baada ya kupitia hotuba ya Mheshimiwa Waziri na kugundua kuwa alitembea Mikoa yote ya Tanzania Bara na kwetu Pwani alifika, na alipofika Pwani katika taarifa yake inaonesha kwamba alishughulika na migogoro 83. Nikapata taabu sasa hii migogoro 83 ni ndani ya hii ambayo ninayo Kibaha Vijijini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa sababu sikuwa na kinachonionesha kwamba katika migogoro hii 83 iliyoshughulikiwa Mkoa wa Pwani, ya Kibaha Vijijini ni mingapi, basi nitumie nafasi hii kuwasilisha migogoro hii kwa Mheshimiwa Waziri ili aone namna bora ya kuishughulikia. Japo ipo migogoro mingine, ninaamini kabisa ilishashughulikiwa, lakini tatizo Wizara au Serikali haijarudi kwa wananchi kutoa msimamo au kauli ya Serikali kwamba mgogoro huo umemalizwa kwa namna gani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaanza kuelezea migogoro ya mipaka ya maeneo ya kiutawala. Pale Kibaha Vijijini tuna migogoro ya kiutawala na mamlaka nyingine za halmashauri. Kwa mfano, tuna mgogoro mkubwa sana wa mpaka wa Mkoa wa Pwani na Mkoa wa Morogoro, kule kwenye kipande cha Kata yangu ya Magindu. Ni mgogoro ambao una muda mrefu. Zipo hatua ambazo zinaonekana zimechukuliwa, lakini wananchi kule bado hawana uhakika na nini kimefanyika kwa sababu hawana majibu ya jambo lililofanyika. Kwa hiyo, napenda waufahamu mgogoro huo kama sehemu ya mgogoro mmojawapo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mgogoro mwingine pale Kibaha tena mgogoro wa Kibaha DC pamoja Kisarawe. Kuna shida sana kwenye eneo la Kata ya Kikongo, kwenye upande ule kwa sababu kuna mgogoro mkubwa unaozungumzwa miaka nenda miaka rudi, lakini haupati ufumbuzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mgogoro mwingine, tena mgogoro huu unachekesha sana. Kibaha vijijini ndiyo imeizaa Kibaha Mji, lakini cha kuchekesha leo, eti kuna mgogoro wa mpaka kati ya Kibaha Mji na Kibaha Vijijini. Sasa unashangaa, wa kuulizwa ni Kibaha Vijijini, ulimkatia mwenzio mpaka wapi? Leo nashangaa mgogoro unakua tu, unaendelea tu, haupatiwi ufumbuzi wakati wa kuulizwa tupo na tungeweza kuwaambia hawa wanetu wakati wanazaliwa tuliwapa mpaka wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kuna tatizo la kwenye kutoa maamuzi ya migogoro na sijui inasababishwa na nini? Kwa sababu kama hii migogoro ya mipaka ni kazi nyepesi tu, ni Serikali kutoa tamko kwamba kuanzia hapa sasa ndiyo kutakuwa kunaitwa mpaka, sasa tuone atakayebisha. Kwa sababu kila mmoja atakuwa hahami na kila mwananchi atakuwa anakaa kwenye eneo lake, anaendelea na shughuli zake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kama wananchi hawasikii nini kimetamkwa na Serikali, utabaki ugomvi unaoonekana kati ya Wabunge na Wabunge au Wabunge na Wakuu wa Wilaya kitu ambacho hakuna sababu ya kuendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile, kuna migogoro ya wakulima na wafugaji. Kuna maeneo yametengwa kwa ajili ya wakulima na kuna maeneo yametengwa kwa ajili ya wafugaji. Sasa kuna maeneo yana migogoro ya mipaka; wafugaji na wakulima wanaambiana mimi naishia hapa na mimi naishia hapa. Kwangu pale katika Kata ya Gwata kuna Kijiji cha Kigoda na Kijiji cha Ndwati, wanagombana kitu ambacho kinahitaji majibu mepesi tu. Kwa hiyo, naiomba Wizara ingefanya hivi kwenye kutoa matamshi ilimradi kila mmoja ajue anaishia wapi na mambo mengine yaendelee.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano pia kuna ndugu yangu wa Chalinze, bahati mbaya hayuko hapa, lakini ngoja niseme kidogo. Wapo wananchi wanatokea katika Jimbo la Kibaha Vijijini, walikuwa na maeneo yao ya urithi katika maeneo ya Mbala na hili jambo nilikwenda nalo mpaka kwa Naibu Waziri, nilijaribu kumhusisha, lakini inaonekana kwamba sasa hivi pale wanasema ni Kijiji cha wafugaji. Matokeo yake wale wafugaji wanawaondoa wananchi wa asili kwamba, sisi tulishapewa hapa ni kwetu, ninyi hamstahili kufanya shughuli katika eneo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ukiangalia, yanatokea masuala ya sintofahamu, wananchi hawa waende wapi? Kama wao walizaliwa pale, wenzao wamekuja wameoneshwa sehemu ya kuishi, leo wanataka kuchukua kijiji kizima. Nafikiri ni vizuri jambo hili likazungumzwa. Nimeamua niseme hapa kwa sababu ni sehemu ya watu wanaoathirika katika Jimbo la Kibaha Vijijini pamoja na eneo la Chalinze kwenye eneo la Mbala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile, upo mgogoro kwenye Kijiji cha Mwembengozi. Wizara ya Ardhi, kupitia pia Wizara ya Mifugo na Uvuvi, pale Kwala ambapo ndiyo tumejenga bandari kavu, ambapo ndiyo imetengwa kongani ya viwanda, eneo kubwa lilikuwa linamilikiwa na Serikali, lakini kwa umuhimu wa kuwekeza bandari kavu, kwa umuhimu wa kuwekeza kongani ya viwanda, waliamua kupunguza eneo na kuliweka katika mazingira haya ambayo yanatumika kwa shughuli hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa lipo tatizo pale Mwembengozi. Sote tunafahamu kwamba Sheria ya Ardhi inaruhusu Serikali za Vijiji kwa mamlaka walizonazo kisheria kugawa ardhi na wamegawa baadhi ya ardhi kwa wawekezaji. Leo pale Mwembengozi walipokuja na hili suala la kongani ya viwanda, Serikali imekwenda pale Mwembengozi, wanawaambia wale wote waliopewa na Serikali za Vijiji hawawatambui. Hawawatambu eti kwa sababu eneo hili lilikuwa ni la kilimo. Wananchi wanashangaa, ni eneo la kilimo tangu lini? Kijiji kile kipo pale miaka mingi, na mihtasari ya kuwapa wawekezaji hawa Kijiji wameitoa kwa mujibu wa sheria, na imepitishwa kwenye maeneo mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa tumeamua kubadilisha matumizi, tunawapora mamlaka ya ugawaji wa ardhi na kuwaona kwamba hawana mamlaka ya ugawaji ardhi. Sasa jambo hili limeleta mgogoro mkubwa, kesi hizi haziishi. Mkuu wa Mkoa amekwenda pale, ameunda tume, lakini watu hawaelewani. Kwa hiyo, namwomba Waziri, kupitia viongozi wa ardhi, hasa wale makamishina wa ardhi, hebu hii migogoro midogo midogo waende wakaitolee tamko ili ionekane imekwisha na mambo haya yaende kwa utaratibu unaostahili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesema leo nitajielekeza sana kwenye migogoro, kwa sababu sina hakika kama ni hii migogoro 83 ya Mkoa wa Pwani imezungumzwa. Ukienda kwenye Kata ya Kikongo na Mheshimiwa Waziri anafahamu kwa sababu kabla hajawa Waziri jambo hili lilifikishwa kwake kwa muda mrefu sana. Pale Kikongo tulikuwa na shamba la UFC. Wananchi wanafahamu Shamba la UFC linaishia wapi, na lipo eneo ambalo lilibaki kwa ajili ya wananchi wanaendelea na maisha yao. Pia kulikuwa na maeneo ya kijiji ambayo kuna mtu anaitwa Transcontinental, anadai kwamba yeye amenunua. Vikao vyote vya ngazi ya Wilaya na Mkoa vimeenda. Transcontinental anaambiwa alete nyaraka za kuonesha amepataje maeneo hayo? Hana nyaraka. Leo anasumbua wananchi katika eneo lile, anataka wananchi wale watoke, wampishe eneo lile amiliki yeye. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kuna taabu na maswali ya kawaida wananchi kule wanajiuliza, huyu Transcontinental kama anakiri yeye alinunua, nyaraka zake za kununua kutoka kwa wananchi ziko wapi? Kama anakiri alipewa hati, nani alimfanya athibitishwe apewe hati wakati vijiji vinakataa havimtambui? Kwa hiyo, kuna migogoro mingine hii inakuzwa na namna ya watendaji wetu wanavyofanya kazi. Wanashindwa kutoa majibu ya moja kwa moja ili mambo haya yaishe na mambo mengine yaendelee. Kutofanya hivyo, wananchi hawa wanaingia kwenye mgongano mkubwa sana na sisi viongozi tuliopo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili jambo naomba niliseme hapa pasipo uwoga kwamba, jamani tuko wote hapa tumeingia kwa utaratibu wa siasa, na kila mmoja anacho chama ambacho anajua kabisa kinaweza kikatetea masilahi yake. Chama cha Mapinduzi ambacho wananchi wamekiamini kwa asilimia kubwa na wananchi wanaamini hakishindwi kumaliza migogoro hii, nimekwenda pale mpaka na Mwenyekiti wa Mkoa wa Chama cha Mapinduzi, amemwomba Kamishina wa Mkoa asaidie kumaliza tatizo hili, mpaka leo majibu hakuna. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawaomba ndugu zangu, naiomba Wizara iende ikachukue hatua pale tumalize hii migogoro ambayo ipo. Kwa sababu ya muda nitaiweka vizuri kwenye maandishi na nitaikabidhi pale Wizarani ili waone namna bora ya kuishughulikia migogoro hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili, nimesema nimempongeza Mheshimiwa Rais, kwa namna ambavyo ametutengea lile eneo la Kwala kuwa eneo la kongani ya viwanda lakini pia kuufanya kuwa mji mkubwa wa uwekezaji. Hata hivyo, nataka niende sambamba na jambo zima la kutengeneza makazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna kongani pale Kwala, tuna heka 1,000 pale Bisunyala na ndani ya eneo kubwa ambalo Serikali wamepima, lakini sina hakika kama uwekezaji huu wa viwanda unaoendelea pale, unakwenda sambamba na sisi kujenga majengo ya kuweza kuwapokea watumishi wanaokuja pale. Kwa sababu maeneo yote yale ya karibu yamepimwa kwa ajili ya viwanda. Je, wananchi watakaokuja kufanya kazi pale, wanaweza kufanya kazi wakiwa wanaishi kwenye maeneo gani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini kabisa kwamba kwa sababu tuna shirika letu la ujenzi wa majumba, ni vizuri wangeenda pale wakatengewa na wao maeneo sasa hivi. Wakati viwanda vinaendelea kujengwa, na wao wajenge maeneo hayo ili wananchi waweze kuishi kwenye maeneo hayo, na kwa kufanya hivyo mji ndiyo unaweza ukawa vizuri.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naona unanitazama kwa ajili ya muda, basi niungane na Wabunge wote ambao wameipongeza Serikali, nami naunga mkono hoja. Naomba tu Waziri aje kunisaidia kumaliza ile migogoro ambayo iko pale jimboni kwangu. (Makofi)