Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

Hon. Benaya Liuka Kapinga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi ili na mimi niweze kuchangia katika Wizara hii muhimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ningependa sana niende kwenye kipengele hiki cha migogoro. Si kizuri, lakini sasa inabidi tu tukisemee, ilipaswa tuje hapa tuchangie maeneo mengine ya kuboresha zaidi, lakini sasa inabidi turudi nyuma tusemee migogoro. Wamesema wenzangu hapa, na tayari wamesema chanzo cha migogoro ni sisi kutopima maeneo yetu kwa ukubwa wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naliongea hili jambo leo hapa kwa mara ya tatu; ni mgogoro wa mashamba ya wakulima Ndika. Wako wananchi Kijiji cha Mkuani, Makuka pamoja na sasa mgogoro unakua unaenda mpaka Kata nyingine ya Kipapa. Mkuani iko Kata ya Maguu, wananchi hawa tangu mwaka 2017 walichukuliwa mashamba yao na mradi unaoitwa Panda Miti Kibiashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na hapa mimi niombe sana Serikali msomane. Maana tunaisema Wizara ya Ardhi lakini kumbe ndani yake kuna watu wengine Wizara ya Maliasili na Utalii na wengine wako humo ndani lakinimambo yanaenda Wizara ya Ardhi tu. Niombe sana Wizara hizi zisomane na mambo haya muyapange kwa pamoja, ili tuwe na amani katika nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mradi wa Panda Miti Kibiashara sidhani kama Waziri wangu wa Ardhi anahusika nao hivyohivyo, huu uko upande wa Wizara ya Maliasili na Utalii; lakini ardhi ile imechukuliwa ni ya wananchi waliokuwa wanaimiliki kwa halali kabisa. Wananchi wale wamekaa pale tangu kupata uhuru nchi hii, lakini kwa bahati mbaya sana anakuja mtu mmoja leo anasema anataka kuanzisha hili shamba ninyi ondokeni, lakini la pili kwa sababu, sijui umepatikana wilaya nyingine, zamani tulikuwa wilaya moja, sasa ninyi ni wilaya nyingine ondokeni, mkitaka mkaombe kule. Nani anasema tukigawa mipaka hii ya kiutawala inanyima uhuru na umiliki wa ardhi wa mtu Mtanzania huyu, ni nani anasema hivyo? Si sawa kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, wananchi wale wanapata shida kuanzia mwaka 2017 mpaka leo. Wanakufa njaa ilhali wana mashamba yao pale kwa sababu tu ya mambo haya, mtu anakuja analianzisha hili jambo kirahisi tu hivi. Sasa niombe Waziri, wakati fulani Mheshimiwa Waziri Lukuvi alianza kulishughulikia hili na pakawa na amani, lakini ilifikia hatua pale maeneo yale, sisi hatujazoea, sisi Wamatengo kule mambo ya vita haya hatujazoea, lakini watu wametupiga risasi pale. Mgogoro, unapiga mtu risasi. Wanapigwa mapanga pale, kwa nini iwe hivyo? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe Waziri, tutatue huu mgogoro kwa sababu mashamba yale ni ya watu walikuwa wanaishi pale miaka yote. Kuanzisha huu mradi kama kweli wanataka hawa watu kuchukua yale mashamba, mbona sheria ziko wazi, walipe fidia. Walipe fidia ili wananchi wale waondoke pale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mimi nimshukuru sana Mheshimiwa Mkuu wa Wilaya, Mheshimiwa Aziza Mangosongo. Amefika anajitahidi kupambana na huu mgogoro, ili ufike mahali, lakini sasa kwa sababu uko na wilaya nyingine anashindwa. Sasa niwaombe, Mheshimiwa Rais wa nchi hii anafanya kazi nzuri ya kumaliza migogoro, siyo mpaka mgogoro huu wa Ndika tumsubiri Rais aje kutamka maneno pale, Waziri upo na viongozi wengine wapo, njooni mmalize huu mgogoro, tusimsubiri Mheshimiwa Rais, tunampa mzigo mkubwa, ana mambo mengine ya kutuletea fedha na maendeleo mengine ndani ya nchi hii. Hii migogoro ndiyo maana mpo nyie mtusaidie uishe, pale mahali wala si mahali pakuchukua muda mrefu; ukifika Waziri kwa sababu, maeneo ni ya watu utatamka tu neno, wananchi wale watasherehekea na ng’ombe watakupa, si rushwa, lakini ni sadaka kwa ajili ya shukrani; sisi wamatengo tunatoa shukrani. Uje ututamkie ili wananchi wa Ndika, wananchi wale kutoka Kipapa wawe na amani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna kijiji kingine kipo pale, Kijiji cha Kata ile ya Burma, Kata ile ya Mpapa. Na kwenyewe tuna kijiji muda mrefu, kiko pale, lakini wamekuja watu sasahivi eneo lile lote wamelihamisha. Tumejenga mpaka shule, mpaka sasahivi wanafunzi wanatoka maeneo mengine mbali wanakuja kusoma kwenye shule ile ambayo ilikuwepo pale na kijiji kilikuwepo. Lakini ni kama nilivyosema suala hili si lako peke yako, zungumza na Wizara hii ya Maliasili na Utalii, mipango hii wanapofanya basi waifanye vizuri, ili kwamba mwisho wa siku tusilete hii mivutano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mgogoro huu wa Ndika sasahivi wananchi wameamua kwenda kulima wenyewe. Wanasema hivi, kule kulikuwa ni kwetu, tuliondoshwa, sasa mtu kurudi kwao nani atakayemfukuza?

Mheshimiwa Mwenyekiti, wamerudi pale, lakini kilichofanyika pale ni kama wametengeneza, yaani mgogoro wenyewe sasa ndio unaenda kuwa mkubwa. Kwa sababu wananchi wamesema sisi tunarudi kwetu. Tumeisubiri Serikali itoe maamuzi haijatoa, sasa sisi tunarudi kwetu kwenye mashamba yetu. Kwa hiyo hofu yangu tunakoenda huku kutakuwa kubaya zaidi kuliko huku tulikotoka. Kwa hiyo, nikuombe sana Mheshimiwa Waziri twende tukalimalize hili suala pale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili. Nikushukuru sana kwa huu mpango wa hii fedha ya mkopo maana na mimi Mbinga ni mnufaika. Wananchi wetu katika vijiji vya Mbinga tutapata, japo ni vichache, tutapata na sisi kupimiwa viwanja vyetu. Ombi langu sasa, kama si kitu kibaya, Kamati hapa imeshauri kwa nini zile fedha nyingi zile bilioni 47 zikatumike kwa matumizi mengineyo na si kupima ardhi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kama si kuvunja sheria, basi Mheshimiwa Waziri chukua huu ushauri wa Kamati. Kwamba, zile fedha nyingi tukapime vijiji vingi. Na hesabu zimetolewa hapa na Mheshimiwa Komredi Kunambi hapa, ametoa hesabu vizuri sana. Ametoa hesabu kwamba, tukipima vizuri fedha hizi tunaweza kupima vijiji vingi zaidi, ili kuvifikia hivi vijiji na lengo likiwa kupunguza hii migogoro. Maeneo haya yakipimwa mengi maana yake migogoro itapungua sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lingine nilikuwa napendekeza; maeneo yetu haya, ardhi yetu hii kwa sababu hatujaipanga wananchi wanajichukulia hatua ya kwenda kukaa kila eneo. Kila eneo wanaenda kukaa, kila eneo wanaanzisha kijiji, kila eneo wanaanzisha mji, suala ambalo linasababisha hata Serikali kupata ugumu wa kupeleka huduma kwenye hayo maeneo. Sasa tukipanga, utoaji wa huduma na kupeleka huduma nyingine kwenye maeneo haya utakuwa ni rahisi sana, lakini pia tutaitunza ardhi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukumbuke tulipopata uhuru tulikuwa wangapi? Na mwaka huu tuko wangapi? Na miaka ijayo inayokuja tutakuwa wangapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ardhi yetu imebaki ni ileile. Kwa hiyo, tukiipanga hii, kama wananchi watakaa maeneo fulani na maeneo mengine yatakuwa kwa shughuli nyingine itakuwa ni jambo jema zaidi na ardhi yetu itakuwa nyingi na kubwa kuliko, hiataisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niliona niseme haya kwa nafasi hii. Nakushukuru sana na ninaunga mkono hoja. Asante. (Makofi)