Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Innocent Edward Kalogeris

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. INNOCENT E. KALOGERIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja ambayo iko mbele yetu ya Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi, Wizara muhimu katika uchumi wa Taifa letu. Nitumie nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa ambayo anaifanya katika kufungua uchumi wa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie pia nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Mbarawa na wasaidizi wake, Naibu wa Ujenzi na Naibu wa Uchukuzi, lakini vile vile na watendaji wote ambao wapo chini ya taasisi katika Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii nianze mchango wangu kwa TANROADS. Nimpongeze Mtendaji Mkuu wa TANROADS lakini vile vile nimpongeze Meneja wa Mkoa wa Morogoro wa TANROADS kwa kazi kubwa ambayo wanaifanya katika ujenzi wa barabara na madaraja yanayoendelea hapa nchini. Nitumie nafasi hii kumshukuru Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuweza kujenga Barabara ya Bigwa – Kisaki kilometa 78 na madaraja mawili kwa kiwango cha lami, lakini vile vile kwa kujenga Barabara ya Ubena Zomozi – Ngerengere kilometa 11 kwa kiwango cha lami, lakini pia kufanya upembuzi yakinifu kwa ili kujenga kwa kiwango cha lami barabara ya kutoka Ngerengere – Mvua hadi Matemele kwenye Bwawa la Mwalimu Nyerere. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna kila sababu ya kumpongeza Mama yetu Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa maamuzi ya kuweza kujenga barabara hii. Kiuhalisia wananchi wa Morogoro, Wilaya ya Morogoro ambayo ina majimbo matatu, Jimbo la Morogoro Mjini, Jimbo la Morogoro Kusini Mashariki na Jimbo la Morogoro Kusini. Hii ni historia toka tumepata uhuru tulikuwa tunasikia lami kwa wenzetu, lakini kwa mara ya kwanza sasa tunajenga lami. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri ametuambia mpaka kufikia mwezi Juni, mkandarasi atatia saini ya ujenzi. Ombi langu tunaomba kazi hii ya kutia saini mkandarasi na Serikali ifanyike kwenye Wilaya ya Morogoro kwenye eneo lolote katika majimbo hayo matatu ili wananchi wajue kwamba kweli Serikali iko kazini na kazi inaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii vile vile kuishauri Serikali kwenye TANROADS pamoja na kazi nzuri ya ujenzi wa barabara na madaraja lakini tunahitaji vile vile kutunza barabara. Nimwombe Mheshimiwa Waziri tuangalie jinsi gani tunaendelea kutenga fedha kwa ajili ya ukarabati wa matengenezo ya mara kwa mara kwenye madaraja yetu na barabara zetu ili hizi barabara ambazo tunazitengeneza kwa gharama kubwa ziendelee kudumu kwa muda mrefu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile kwa TANROADS watumishi bado ni wachache, vitendea kazi bado ni vichache, lakini vile vile hata vifaa vya kupima ubora wa kazi ni vichache. Nimwombe Mheshimiwa Waziri tuendelee kutenga fedha nyingi kwa TANROADS ili watumishi wapatikane, vitendea kazi viwepo, lakini vifaa vya kupima ubora wa kazi wa fedha nyingi ambayo tunatumbukiza katika ujenzi wa barabara iwe imekamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru Mheshimiwa Waziri mimi ni mkandarasi, naomba ku-declare interest. Tunatumia fedha nyingi sana kutajirisha wakandarasi wa kigeni, lakini kwa mara ya kwanza naamini ushauri wa Kamati ya Miundombinu ambayo na mimi ni Mjumbe inaoneka Mheshimiwa Waziri ameusikiliza. Nimeona katika ukurasa wa Kitabu cha Bajeti, ukurasa wa 44 kuna miradi minne ambayo imetengewa wakandarasi wazawa, lakini kuna miradi mitano ambayo imetengewa wakandarasi wazawa wa kike, hongera sana Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa inaonesha tunataka kujenga uchumi uendelee kubaki nchini kwetu, lakini kuwatengeneza wakandarasi wetu sasa na wao waweze kutoka hata nje ya nchi kama Wachina wanavyotoka wakafanye kazi kule wakalete fedha nchini na kujenga uchumi wa kwetu. Ombi langu, wakandarasi tuna tatizo moja Mheshimiwa Waziri, tuna tatizo wa kuwa na utaalam wa contract management, lakini tuna tatizo la utalaam wa fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe Mheshimiwa Waziri katika miradi hii minne ya wakandarasi wazawa, wanaume lakini hii miradi mitano ya wakandarasi wazawa wa kike, atengeneze utaratibu wa kuhakikisha kwamba kila mradi utakuwa na Mkandarasi Mshauri wa kuweza kuwasaidia wakandarasi hawa wazawa, lakini vile vile kuhakikisha kwamba fedha inapatikana wasiwe wanasuasua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua tulijaribu kwenye Daraja la Sibiti, lakini tumejaribu kwenye Barabara ya Ludewa – Kilosa, tumewapa wakandarasi lakini wakandarasi hawa wamepata wakati mgumu katika kufanya kazi hiyo kwa sababu ya ukosefu wa utaalam katika uendeshaji wa miradi, lakini fedha za kufanya kazi. Kwa hiyo, nimwombe Mheshimiwa Waziri aangalie hili alisimamie vizuri kama alivyosimamia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine, nizungumzie kwenye TPA. Wabunge wote wanaridhia, nami naridhia, hatuna sababu ya uoga katika hili la kutafuta wawekezaji katika bandari yetu. Bandari ni lango ambalo linaenda kuleta fedha nyingi katika nchi hii. Tumekwenda Dubai, wengine wamekwenda India tumeshuhudia tumeona wenzetu wanavyofanya, sasa tuna sababu gani ya kuogopa? Hatuna sababu ya kuogopa. Nimwombe Mheshimiwa Waziri atuletee sheria Bungeni, tutunge sheria ili kusudi tuingize Sekta Binafsi kwenye bandari, waweze kuleta fedha na uchumi wa nchi yetu uweze kukua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nichangie TRC, kazi kubwa imefanyika na Mama yetu Samia Suluhu Hassan. Vipande vyote vya Reli vya SGR vina wakandarasi na wako kazini. Ombi langu kwa Serikali, tukikamilisha reli hii tunatarajia kusafirisha tani 17,000 kwa mwaka. Ombi langu ni moja, tukitegemea kwamba Serikali ijenge miundombinu, inunue mabehewa, inunue vichwa vya treni, ni kwamba hatuwezi kufikia lengo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati huu tunajenga, nimwombe Mheshimiwa Waziri atuletee sheria Bungeni tena, tutengeneze utaratibu, wawekezaji binafsi nao waweze kununua vichwa vyao vya treni, wawekezaji binafsi waweze kununua mabehewa ili tutakapokuwa tumekamilisha ujenzi wa reli, kazi ianze moja kwa moja ili fedha irudi kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie kwenye suala la ATCL tuna kila sababu ya kwanza, kuishauri Serikali yangu hili shirika tunalipa wakati mgumu sana, Engineer Matindi naamini kwamba anaweza akazeeka wakati muda bado siyo wa kuzeeka kwake kwa kazi kubwa ambayo tunampa. Haiwezekani Mheshimiwa Waziri shirika linakodishwa shilingi milioni 700 kwa mwezi linalipa Serikalini, eti kwa ajili imekodisha ndege za Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile ndege hizo zikienda nje zinakamatwa kwa sababu ya madeni ya Serikali. Mimi ninaiomba Wizara hebu liangalie hili tufute deni la ATCL ambayo ni shilingi bilioni 113. Tukifuta deni hilo ndege hizi wakabidhiwe ATCL hata ikiwezekana kwa kukopeshwa badala ya kulipa hiyo shilingi milioni 700 kwa mwezi ambayo haijulikani wanalipa nini, walau wakope baada ya muda wakimaliza madeni ndege hizi ziwe za shirika na kazi naamini itaendelea, tukifanya hivyo tutakuwa tumelisaidia shirika hilo na ninaamini kabisa tutakuwa tumefanya kazi kubwa sana katika nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwangu mimi ni faraja ni furaha, sina sababu ya kuendelea kuchangia mengi, naamini kabisa Wanamorogoro tunakwenda kuona lami sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba niunge mkono hoja. (Makofi)