Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

Hon. Francis Kumba Ndulane

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kuniona na kuwa mchangiaji wa kwanza katika Bajeti ya Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi jioni ya leo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naipongeza Wizara yetu ya Ujenzi na Uchukuzi kwa namna ambavyo inachapa kazi katika kuhakikisha kwamba inaboresha miundombinu hapa nchini. Hongera sana Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Prof. Mbarawa, pamoja na Wasaidizi wako katika Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda kuanza kuchangia kwa kuizungumzia barabara inayoanzia katika Kijiji cha Nandete, inayopita katika Vijiji vya Gezaulole Mkoa wa Pwani, pamoja na Kijiji cha Tawi kwenda kutokea Nyamwage.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tarehe 16 Agosti, 2010 wakati wa maadhimisho ya kumbukizi za sherehe ya miaka 100 ya Majimaji, aliyekuwa Rais wetu wa Serikali ya Awamu ya Nne, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete, alielekeza Mamlaka ya TANROADS iweze kuifungua hii barabara kutoka Nandete kupitia Gezaulole – Tawi kwenda kutokea Nyamwage yenye urefu wa kilometa 46 ili iweze kupandishwa daraja na kuwa barabara ya Mkoa. Lakini kwa masikitiko makubwa, napenda nieleze kwamba mpaka kuifikia leo hatujawahi kuona dozer wala grader likifika pale kuweza kuitengeneza hii barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ingawa watu wa TANRODAS wa Mkoa wa Lindi – kwa sababu mimi nilikuwa jikoni pale TANROADS Lindi – nilishuhudia ofisi yetu ya TANROADS wakati ule ikitengeneza write-up ya ujenzi wa ile barabara ambao ulitarajiwa kugharimu shilingi bilioni 1.2 kwa gharama za wakati ule ili iweze kufunguliwa, kukatwa milima, ku-fill kwenye mabonde lakini mwisho wa siku kuijenga kwa kiwango cha changarawe. Kwa hiyo kwa masikitiko makubwa nasema kwa miaka 13 sasa hii barabara ambayo iliahidiwa na Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wetu wa Serikali ya Awamu ya Nne, haijaweza kushughulikiwa hata kidogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kusikitisha kidogo kwa sababu kuna barabara juzijuzi hapa, mwaka 2021, kwa mfano kuna barabara ile inayoanzia Bigwa kwenda kutokea Kisaki pale Morogoro ambayo inapita kwenye Majimbo matatu, Jimbo la Mheshimiwa Abood, Jimbo la Mheshimiwa Innocent Kalogeris pamoja na jimbo la Mheshimiwa Taletale, yenyewe yalitolewa maagizo kama haya na Mheshimiwa Rais wetu, Hayati Dkt. John Joseph Pombe Magufuli wa Serikali ya Awamu ya Tano, na leo hii tumepewa taarifa hapa kwamba mwezi Juni utasainiwa mkataba kwa sababu taratibu za manunuzi zimefanyika, ile barabara inakwenda kujengwa kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tunahitaji angalau changarawe tu kwa kuanzia zile kilometa 46 ili kuweza kuwainua kiuchumi wananchi wa Wilaya za Kilwa, Liwale pamoja na wananchi wa Wilaya ya Rufiji, Mkoa wa Pwani. Kwa hiyo ninaomba Serikali itilie uzito. Tusisubiri mpaka baadaye Kiongozi anafariki ndiyo unaanza kusema tunamuenzi kiongozi. Tumuenzi Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete akiwa hai. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho wa siku niseme tu kwamba wananchi wa Kilwa Kaskazini kupitia mikutano yao ya Mabaraza mbalimbali tayari walishaibatiza jina hiyo barabara, walishasema ikitimia ikawa kwa kiwango cha lami wataiita barabara ya Jakaya Mrisho Kikwete. Kwa hiyo, ninaomba Serikali iishughulikie. Nina hakika ikitengwa bilioni 2.5 ile barabara inaweza kufunguliwa, kuwekwa makalavati na changarawe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda niizungumzie barabara ya pili inayotoka Njia Nne kwenda Kipatimu yenye urefu wa kilometa 50. Barabara hii kwa miaka miwili na nusu iliyopita imeweza kujengwa kwa kiwango cha lami kilometa 1.9 na hivyo kuacha kilometa 48.1 zikiwa hazijajengwa kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa scenario iliyopo inaonesha kumekuwa kukijengwa wastani wa mita 700 mpaka mita 600 kwa mwaka, kiwango ambacho ni kidogo sana. Ninaomba katika eneo hili Serikali ije na mradi wa kimkakati wa angalau kilometa 20 katika ile barabara mwaka ujao wa fedha ili mwaka huo unaofwata tuweze kuimaliza ile barabara kwa sababu itabaki eneo dogo tu. Kwa hiyo, niiombe Serikali iongeze fedha katika ile barabara kupitia bajeti ya mwaka 2023/2024 ili barabara ile iweze kuendelea kujengwa kwa kiwango cha lami na iweze kuwa na urefu wa kutosha wa kiwango hicho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya tatu ninayopenda kuizungumzia ni barabara ya Nangurukuru – Liwale. Nimesoma kwenye randama ya bajeti yetu ya Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi, nimeona Serikali imekusudia kujenga umbali wa kilometa 50 kutoka Nangurukuru kwa kiwango cha lami. Lakini ile barabara ina urefu wa kilometa zaidi ya 230 toka Nangurukuru kwenda Liwale. Kwa hiyo ukiangalia kilometa 50 haifiki hata robo ya umbali ambao unatakiwa kujengwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ninaiomba Serikali iongeze angalau kilometa 50 nyingine tuanze na kilometa 100 baadaye tujenge tena 100 ili katika mwaka wa tatu basi tuweze kumaliza. Ikiwezekana mwaka 2025/2026 tuweze kumaliza ile barabara kwa kiwango cha lami kwa sababu wananchi wameteseka kwa miaka mingi katika ujenzi wa ile barabara.

MHE. ZEBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Ndulane, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Kuchauka.

TAARIFA

MHE. ZEBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kumpa taarifa mzungumzaji kuhusiana na hiyo barabara ya Nangurukuru – Liwale kwamba siyo tu kwamba imetengwa fedha kilometa 50, mimi ombi langu ni kwamba hizo kilometa 50 fedha hizo zitoke kwenye bajeti hii.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Francis Ndulane, unaipokea hiyo taarifa?

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa yake nimeipokea kwa mikono miwili kwa kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la nne ambalo ninapenda kulizungumza siku ya leo ni kuhusiana na upanuzi wa barabara kulingana na Sheria ya Barabara ya mwaka 2007 (The Roads Act, 2007). Katika mwaka 2007 upana wa barabara ulipanuliwa kwa barabara kuu kutoka mita 45 hadi mita 60 na zile barabara za mkoa zilipanuliwa upana kutoka mita 30 hadi mita 45.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuwaambia kuwa hadi kufikia leo katika lile eneo ambalo barabara ilipanuliwa kwa mujibu wa Sheria ya Barabara ya mwaka 2007, wananchi wote wa Mkoa wa Lindi hawajalipwa fidia zao. Kwa hiyo ninaomba Serikali ije na maelezo ni lini itaanza kutekeleza mkakati wa kulipa fidia katika lile eneo ambalo waliliongeza kwa mujibu wa sheria.

MHE. CHARLES M. KAJEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

TAARIFA

MHE. CHARLES M. KAJEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpe taarifa mchangiaji kwamba, siyo kwake tu ambako bado hawa wananchi hawajalipwa, hata kwangu Mwibara wananchi wengi wanateseka kwa sababu hawajalipwa fidia zao. Tunaomba Serikali iwalipe fidia zao.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Francis.

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naipokea taarifa yake rafiki yangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo hili inaonekana ni janga la Kitaifa, kwa hiyo naomba Wizara ikadirie fedha, ikiwezekana ianze kulipa kwa awamu katika hizi barabara wakianzia na barabara kuu baadaye waende kwenye barabara za Mikoa na nyinginezo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho kabisa, kuna barabara inayotoka Rangitatu kwenda mpaka Kongowe, yenye urefu kama kilometa 12 hivi. Ile barabara ilipangwa kujengwa zaidi ya miaka 10 iliyopita, lakini sijasikia leo hapa kama kuna kasma yoyote imetengwa kwa ajili ya ujenzi wa barabara ile kwa kiwango cha barabara nne. Kwa hiyo, ninaomba wakati Mheshimiwa Waziri anakuja ku-wind up atuambie ni lini ile barabara itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami njia nne kutoka Kongowe mpaka Rangitatu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha, naunga mkono hoja. (Makofi)