Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nimpongeze sana Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Adolf Mkenda na Naibu wake Mheshimiwa Omari Kipanga na wataalamu wa Wizara kwa kazi nzuri wanazofanya kwenye kutekeleza Ilani ya CCM.

Mheshimiwa Spika, mimi nitachangia kuhusu nafasi ya vyuo vikuu vya Tanzania kimataifa, na uhitaji wa kuboresha website za vyuo vyetu ili vionekane kimataifa na kukamata nafasi za juu Barani Afrika na duniani.

Mheshimiwa Spika, Tanzania yetu ni nchi inayokua kwa kasi hapa Afrika Mashariki na kwa kuwa nchi yetu ina muundo bora wa elimu, ni vyema ubora huo ukaonekana katika vyuo vyetu vikuu.

Mheshimiwa Spika, kwenye mpangilio wa vyuo vikuu 200 bora Barani Afrika, kwa kutumia mtandao wa uniRank kwa mwaka huu wa 2023, Chuo Kikuu cha Nairobi ni cha sita kwa ubora, na cha Makerere ni cha 16 kwa ubora na Kenyatta University ni cha 24.

Mheshimiwa Spika, Chuo chetu Kikuu cha Dar es Salaam kimeshika namba ya 34, Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine ni cha 67, Chuo Kikuu cha Afya cha Muhimbili ni cha 94, State University of Zanzibar ni ya 163 na University of Dodoma ni ya 184.

Mheshimiwa Spika, katika vyuo vikuu bora 200, Kenya na Uganda wametuzidi kwa mbali kwenye Ubora.

Mheshimiwa Spika, vyuo vya Afrika Kusini vimeshika nafasi za juu na nyingi Barani Afrika kwa sababu nchi yao imewekeza kikamilifu kwenye elimu ya vyuo vikuu, na vimefanikiwa kwa sababu vina mahusiano mazuri na vyuo vikuu bora duniani ambapo wamekuwa wanajifunza kutoka kwa wenzao kwa kushirikiana katika shughuli za utafiti na programu za kubadilishana uzoefu.

Mheshimiwa Spika, uniRank inatumia vigezo vya kimtandao kuorodhesha vyuo bora Afrika na duniani kwa ujumla. Ubora huo hutegemea machapisho ya kisayansi yaliyofanywa na chou; shughuli za kiutafiti za chou; uwepo wa cheti cha usajili wa chuo na kutambuliwa na Mamlaka za nchi (TCU); chuo kutoa mafunzo ya shahada ya kwanza au za juu (Masters na Ph.D); na chuo kutoa elimu kwa njia ya kawaida ya kuingia darasani na kukutana ana kwa ana na waadhiri.

Mheshimiwa Spika, kufanya vibaya kwa vyuo vikuu vya Tanzania kumesababishwa na viongozi wa vyuo vyetu kukosa ubunifu wa kuonyesha mambo mazuri yanayofanyika vyuoni kwenye mitandao. Pia changamoto ingine kubwa ni kwamba wasomi na watafiti wa Kitanzania katika vyuo vyetu wamekuwa wavivu kuchangia machapisho yao katikaa jukwaa la wasomi duniani. Vilevile website nyingi za vyuo vyetu zinakosa taarifa muhimu za chuo na matokeo ya utafiti hubakia kwenye kuta za chuo.

Mheshimiwa Spika, ubaya wa kushika nafasi za chini kwa vyuo vyetu vikuu inaondoa heshima ya chuo na wafanyakazi katika macho ya wadau, kama vile wanafunzi na wafadhili; umaarufu kidogo wa wafanyakazi wa chuo kwenye wasomi wa vyuo vingine vya ndani na nje; kuathiri ushirikiano na vyuo vingine vikubwa duniani kwenye kufundisha na utafiti. Hawatashirikiana na vilaza; na kukosekana nafasi kwa wasomi wetu katika soko la dunia.

Mheshimiwa Spika, ushauri kwa Wizara na vyuo ni kama ifuatavyo; iwe ni lazima kwa wahadhiri wote wa chuo kujisajili na google scholar (point huchakatwa kutoka huko); walimu na wanafunzi wote wahimizwe kuandika tafiti zao katika majarida ya kimataifa. Tafiti mpya tu ndio hutumika kutoa alama; iwepo sera ya kuweka machapisho yote kwenye repository ya maktaba kuu ya chuo, ni iweze kuonekana kwenye mtandao; walimu wote wahimizwe kuweka machapisho yao kwenye sehemu ya wazi (open source research repository); benki ya machapisho ya chuo kikuu iwe na mfumo wa kuonesha kwenye mtandao vitabu vya degree za Masters na Ph.D; kuwe na mfumo wa online kuonesha abstracts zote za kazi za wanafunzi za Masters na Ph.D; matukio yote muhimu ya chuo yapigwe picha na kuwekwa mtandaoni; wekeni mtandaoni nyaraka za mawasilisho yaliyofanyika katika mikutano au makongamano mbalimbali yaliyofanywa na walimu au wanafunzi katika sehemu duniani.

Mheshimiwa Spika, nihitimishe kwa kusema kwamba nafasi za chini kwa vyuo vyetu vikuu vya Tanzania siyo kitu chema kwani kinapunguza heshima ya nchi yetu kwenye macho ya wadau mbalimbali kama vile wanafunzi watarajiwa, watafiti, wasomi na wafadhili. Ni vyema Wizara ikachukua hatua mapema kukabiliana na tatizo hili.

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo yangu hapo juu, naunga mkono hoja.