Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami ninakushukuru kwa kunipa fursa na nianze kwa kumpongeza sana Waziri wetu Profesa Adolf Mkenda, Naibu wake Omari Kipanga na Katibu Mkuu Profesa Carolyne Nombo na Wakuu wote wa taasisi zilizoko chini ya Wizara ya Elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naanzia pale alipomalizia mwenzangu, nimpongeze sana Rais kwa kuboresha shughuli za elimu katika nchi yetu kwa sababu anajaribu ku-address, kutatua kero kubwa ambazo ni ujinga, umaskini na magonjwa na Wizara hii inahusika moja kwa moja kwenye kupambana na hivi vitu. Ninaanzia pale Mheshimiwa Sekiboko aliposema kwamba ubora na mimi nitaongelea ubora wa vyuo vikuu. Nataka tulinganishe vyuo vyetu vikuu vya Tanzania na vyuo vya Afrika na duniani kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa Tanzania na Afrika Mashariki, Tanzania tunakweda vizuri. Nchi yetu inakua vizuri sana na sisi kama nchi Taifa letu lina miundombinu bora sana ya elimu. Tunatoa elimu bure kuanzia darasa la kwanza mpaka kidato cha sita na tunatoa mikopo kwa vijana wetu waweze kusoma. Kwa hiyo suala la kusoma hapa nchini siyo shida. Nchi yetu inajitahidi vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nilisikiliza taarifa ya habari ya BBC, wakasema kwamba kule Afrika Kusini kati ya watoto 10, nane hawajui kusoma vizuri na kuandika, lakini nchi ya Afrika Kusini katika Bara letu la Afrika ndiyo nchi yenye vyuo bora kuliko nchi zote kwenye Bara la Afrika. Sasa hapa kwetu Tanzania kwenye ubora wa vyuo vikuu tuko vibaya sana, hatuko vizuri. Ni kwa nini, ni nini kinatokea kwamba hata wale ambao asilimia kubwa hawajui kusoma na kuandika wanatupita?

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ranking iliyofanyika kuangalia vyuo vikuu bora 200 duniani, Afrika Kusini nafasi ya kwanza mpaka ya tano ilichukuliwa na Afrika Kusini. Chuo Kikuu cha Nairobi kilikuwa cha sita, Chuo Kikuu cha Makerere Uganda kilikuwa cha 16. Chuo Kikuu cha Kenyatta kilikuwa cha 24. Chuo chetu Kikuu cha Dar es Salaam kilikuja cha 34, Chuo Kikuu cha SUA kikawa cha 67, Chuo Kikuu cha Afya Muhimbili cha 94, State University of Zanzibar cha 163 na UDOM ikawa ya 184. Tunawashukuru hivi vyuo angalau vimetupeleka juu kidogo lakini bado kuna kitu hakiko sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwa nini South Africa wanatushinda na ukiangalia kwa ujumla wake katika hii ranking, vyuo vya Kenya na Uganda vimetupita vibaya sana. Sisi tuko chini kusema ukweli kwenye hii aspect.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa wenzetu wamefanikiwa sana kwa sababu wamewekeza kikamilifu kwenye sekta ya elimu na hapa sawa tunakwenda vizuri lakini bado kuna haja ya kuendelea kuwekeza pesa za kutosha kwenye sekta ya elimu ili vyuo vyetu navyo vionekane vizuri kwenye uso wa Kimataifa. Vigezo vinavyotumika kwenye ku-rank hivi vyuo ni vitu vya kwenye mtandao tu, mambo ya kwenye mtandao na sisi kama nchi Tanzania iko vizuri sana kwenye mambo ya mtandao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza wanaangalia kwenye mtandao kama kuna machapisho ya kisayansi yaliyofanywa na wasomi wetu. Kitu cha pili wanachoangalia ni shughuli za kitafiti kwenye mitandao ya vyuo vyetu. Je, kuna shughuli zinazoendelea za kitafiti? Je, chuo kimesajiliwa na mamlaka husika kama TCU? Je, chuo kinatoa degree za kwanza, Master na Ph.D? Hiyo tunafanya. Je, vyuo vinatoa elimu kwa kuwasiliana, wananfunzi wanakaa darasani na kusoma? Vyote hivyo tunafanya lakini bado hatuonekani kwamba tunafanya vizuri kama vyuo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu cha pili wanachoangalia ni shughuli za kitafiti kwenye mitandao ya vyuo vyetu. Je, kuna shughuli zinazoendelea za kitafiti? Je, Chuo kimesajiliwa na mamlaka husika kama TCU? Je, Chuo kinatoa degree ya kwanza, masters na Ph.D? Je, vyuo vinatoa elimu kwa kuwasiliana, na wanafunzi wanakaa darasani na kusoma? Yote hiyo tunafanya,a lakini bado hatuonekana kwamba tunafanya vizuri kama vyuo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kufanya huku vibaya kunasababishwa na viongozi wetu wa vyuo kukosa ubunifu kuonesha vitu vizuri ambavyo wamefanya. Ubunifu hamna, hiyo ndiyo sababu yangu ya kwanza. Sababu ya pili ni uvivu wa wanasayansi wetu wa Kitanzania kuchapisha, kuandika kwenye majarida ya Kimataifa ili sisi kama Taifa tuweze pia kutamba na kwenda kifua mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sababu ya tatu ni tovuti zetu za vyuo vikuu haziweki vitu, hazina taarifa ya vyuo vyetu vikuu. Hakuna taarifa za mambo mazuri tunayofanya. Matokeo mengi ya utafiti ambayo wenzetu wanafanya, yanabakia kwenye makabati na kwenye kuta nne za vyuo vikuu, hayatoki nje ya pale. Hizi ni sababu kubwa ambazo zinatufanya tusionekane tuko vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nini athari za kupata low rank ya Universities zetu? Athari ya kwanza ni heshima hakuna. Tunakosa heshimia tukijilinganisha na wenzetu wa nchi nyingine. Athari ya pili, ni umaarufu wa Maprofesa wetu na Wahadhiri wetu. Huwezi kujilinganisha kwamba na wewe ni Profesa ukatamba kabisa kama chuo chako hakipo pale, yaani your nowhere, huwezi kuonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunakosa nafasi ya kupata washirika wa kusaidiana nao kufanya utafiti. Huwezi kwenda kwa watu ambao labda ni vilaza ukafanya nao kazi, hapana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kingine ni kwamba wasomi wetu wanakosa nafasi. Kama hatuko vizuri, tunakosa nafasi kwenye masoko ya Kimataifa. Ushauri wangu nini kifanyike? Cha kwanza namwomba Mheshimiwa Waziri asimamie hili, Wahadhiri wote na wanafunzi wanaofanya Masters na Ph.D wajisajili kwenye Google Scholar, kwani mchakato wa kupata vyuo bora unatokea kwenye Google Scholar. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu cha pili, watafiti wetu wachapishe kwenye majarida ya kimataifa, tusiende kwenye zile journal za ajabu ajabu ambazo hata hazipo kwenye mifumo. Twende kwenye majarida ya kimataifa kama wanaume na wanawake wenye nguvu pia. (Makofi/Kicheko)

MBUNGE FULANI: Naam!

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri pia tuwe na sera ya kuweka machapisho yetu kwenye depository vyuo vyote, kwenye library zetu ziweze kuonekana online. Cha nne, tuoneshe abstract, hata tukishindwa kuonesha zile Ph.D na Masters ambazo vijana wetu wameandika, tuziweke online ili wanapochakata na sisi tuonekane tupo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, cha tano, matukio yanayotokea kwenye vyuo vyetu kama mikutano, tukienda kwenye makongamano, wanaangalia vitu vyote hivi viwekwe online ili wanapochakata na sisi tuonekane kwamba huwa tunashiriki kwenye hivyo vitu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, pia tukienda kufanya presentations kwenye Mikutano ya Kimataifa tuyaweke kwenye mitandao ya vyuo vyetu. La muhimu hapa niwaombe Wakuu wa Vyuo na Wakuu wa Mabaraza ya Vyuo wasimamie hili kwa sababu kabisa sioni sababu ya sisi kuwa na low ranking. Nchi yetu inawekeza pesa nyingi sana kwenye elimu lakini kweli kabisa hatuko vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama mimi najua nilitoa mchango wangu na ndiyo sababu nimesimama hapa kwa nguvu kabisa, siogopi kuchangia kwamba tukaze viatu, tukaze uzi, twende vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nihitimishe kwa kusema kwamba hili suala la kuwa na nafasi za chini kwa vyuo vyetu siyo kitu chema, inatupunguzia heshima ya nchi yetu. Namwomba Waziri achukue hatua makini kabisa mapema kukabiliana na tatizo hili ambalo tukishakabiliana nalo mtatujengea heshima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)