Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Dr. Jasson Samson Rweikiza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bukoba Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

3

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. DKT. JASSON S. RWEIKIZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili nichangie katika bajeti ya Wizara ya Elimu. Nimpongeze na kumshukuru Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mheshimiwa Profesa Adolf Mkenda; Naibu Waziri, Mheshimiwa Omari Kipanga; Katibu Mkuu na Naibu wake na viongozi wote wa Wizara na watumishi wote wa Wizara kwa kazi nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee nimpongeze na kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kazi nzuri sana anayoifanya ya kuboresha elimu na hata sekta nyingine anazozisimamia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo pale Bukoba kwangu shule nyingi zimejengwa, madarasa mengi yamejengwa. Pale Mkoa wa Kagera leo tuna Chuo cha VETA, chuo kikubwa kizuri sana cha VETA kimejengwa, amekifungua mwaka jana yeye mwenyewe Mheshimiwa Rais na hivi ninavyoongea tunajenga Chuo Kikuu cha Dar-es-Salaam, branch ya Bukoba. Haya ni maendeleo makubwa ambayo kwa kweli nampongeza na kumshukuru sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa huku chini ngazi ya Wizara, Waziri na wasaidizi wake na watendaji wote, naomba tumsaidie Rais kwenye kazi hii, tumsaidie Rais kwa nguvu zote, kwa moyo wote, kwa bidii zote. Wamesema Wabunge hapa leo na siku zote wanasema, amesema msemaji wa mwisho hapa kwa mfano, uhaba wa Walimu ni tatizo kubwa sana kwenye shule zetu. Ni tatizo kubwa sana ambapo shule zimejengwa, madarasa yapo, lakini hakuna Mwalimu, sasa ni kama sifuri, kazi iliyofanyika ni zero.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina shule pale Bukoba, Shule ya Msingi Musira ina wanafunzi kasoro kumi tu wafike elfu moja, ina Walimu saba. Nina Shule ya Msingi Nakigando ina wanafunzi 840, ina Walimu sita, upungufu wa Walimu kumi na tano. Matokeo yake hawa watoto wanakaa pale, wanashinda wanacheza, hawafundishwi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina shule za sekondari, shule nzima haina Mwalimu wa hesabu, shule nzima haina Mwalimu wa kemia. Sasa haya ni matatizo makubwa ambayo nafikiri yako ndani ya uwezo wa Wizara kuyafanyia kazi na kuyatatua angalau kwa kiasi cha kutosha watoto wasome, wapate elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, shule za binafsi zimezungumziwa na Wabunge wengi hapa, Mheshimiwa Dkt. Kikoyo, Mheshimiwa Tunza, Mheshimiwa Minza amesema, Wizara iache kuziona shule binafsi kama washindani wao. Mheshimiwa Rais ana lengo la kuboresha elimu, elimu iwe na ustawi mzuri, ufanisi uonekane kwenye elimu na shule binafsi zinatoa mchango mkubwa kwenye eneo hili, kwenye kuboresha elimu. Sasa Wizara ya Elimu na Wizara nyingine kama Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa zinaiona hii sekta kama ni washindani wakubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niko kwenye sekta ya shule binafsi, naendesha shule binafsi na ni Mwalimu pia, nilifundisha huko zamani, kwa hiyo, ninachokisema nakifahamu. Majuzi hapa, mwaka jana, Wizara ilifuta kupanga wanafunzi wa kwanza mpaka wa mwisho, wakafuta kupanga shule ya kwanza mpaka ya mwisho. Kuna Mheshimiwa Mbunge aliuliza swali hapa, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia akajibu vizuri sana, akajieleza vizuri sana watu wakapiga makofi, lakini ukweli uko pale pale, walifuta hiki kitu kwa sababu ya kuogopa shule binafsi, kwamba zinafaulisha zinawazidi, kwa hiyo, ili kuondoa hii noma ya kuwazidi basi angalau kufuta wote tuonekane tunalingana. Huo ndio ukweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, watoto hawawezi kusoma bila usindani. Mtoto wa primary anasomaje? Hafahamu maana ya kusoma, lakini ile pride ya kujivunia kwamba, nimemzidi huyu, nimekuwa wa kwanza, nimekuwa wa kumi, nimewazidi thelathini, arobaini, inamwongezea motisha ya kusoma. Ukitoka mtihani amekuwa wa saba, amekuwa wa ishirini, amewazidi wenzake anaongeza motisha. Sasa wewe unafuta ranking? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni vita kati ya shule za Serikali na shule za binafsi, hii sio sawa. Kwa kweli, kufuta ranking wanaua elimu na ukiua elimu unaua nchi. Mheshimiwa Waziri, Profesa ataingia kwenye rekodi, kwenye historia kwamba, aliua elimu ya Tanzania kwa kufanya hiki kitendo cha kufuta ranking. Ushindani ndio kila kitu, hata kwenye maisha huku mtu anataka ajenge nyumba nzuri, avae vizuri kumzidi mwingine na shuleni hivyohivyo, mtoto akifaulu vizuri kumzidi mwenzake anajisikia anaongeza kasi anasoma kila siku anaongeza bidii na nchi inapata ufanisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine, kuonesha mapambano yaliyopo kati ya shule za Serikali na za binafsi. Mwaka jana matokeo ya darasa la saba, shule zaidi ya ishirini na kidogo hivi zilifutiwa matokeo kwamba, zimeiba mitihani, zikafutiwa matokeo, zikatangazwa, zikafutiwa vituo vya mitihani. Shule ya Serikali, Olympio, ilituhumiwa kwamba, imeiba mtihani, ikafutiwa matokeo. Haikutangazwa, haikufutiwa kituo, mpaka leo inaendelea na kituo chake. Sasa haya ni mambo gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, za private zimetangazwa sana, zimeharibiwa sifa, zimeharibiwa jina, ya Serikali Olympio haikutangazwa, ikaonekana yenyewe haina matatizo, walirudia mtihani kama wengine wote walivyorudia, japo kimya kimya. Sasa haya mapambano ya namna hii kwa kweli, sio kujenga au kuboresha elimu bali ni kupambana na sekta ya binafsi ili kuiondolea uwezo wake na utendaji wake mzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nyaraka hizi ambazo amezisema Mheshimiwa Kikoyo, amezitaja kwa idadi, amefanya utafiti. Nafikiri baadhi ya nyaraka watoe, watu- consult au hawa wahusika na wadau wawashirikishe. Unaposema unafuta mabweni shule ya awali mpaka darasa la nne, hujawauliza wenye shule wanaoendesha, hujawauliza wazazi waliowapeleka kwa hiyari yao, unaboresha unaharibu au unabomoa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, huyo Waziri anayemfutia mabweni ameomba kibali kwake kwamba, naenda kujenga shule ya bweni ya awali mpaka darasa la nne. Anampa kibali kwa maandishi, anacho, amekopa pesa benki amenunua vitanda, amejenga majengo, ameweka magodoro, kesho anamfutia kibali, anamfutia bweni, afanyaje? Alipe vipi hilo deni?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna njia nyingi za kuzuia ushoga. Kama ni ushoga, hakuna anayeupenda katika nchi hii, nina hakika, ziko njia nyingine nzuri za kuzuia ushoga, sio kufuta mabweni. Weka kamera, weka masharti magumu, idadi ya wanafunzi, toa mafunzo, watu wajifunze namna ya kuendesha shughuli hii bila kufuta.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna shule pale Bukoba mwenye shule Kaizirege yeye ni bweni tupu. Ukisema hakuna bweni ina maana shule imefungwa, imekufa hiyo, unataka kuua hizi shule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna kodi 18, naona nimepigiwa kengele, sitazisoma zote ningezitaja hapa. Kodi ya mapato, VAT, kodi ya ardhi, majengo, leseni, WCF, vibali vya wafanyakazi wa nje, kodi ya zimamoto, usalama kazini OSHA, LATRA, kodi ya ukaguzi, mitihani ya Taifa ina kodi, ada ya mitihani ya mock ya Wilaya, ya kata, ya nini, kuna michango kibao. Matangazo kodi, hata ukiandika kwenye basi lako ukaandika jina la shule unalipia, basi lako mwenyewe uandike jina la shule unalipia TRA, yaani mambo ya ajabu sana. Kodi ya service levy, sheria inazuia service levy kwenye shule wenyewe wanatoza service levy, UMISETA, UMITASHUMTA, usipotoa unakipata chamoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutafsiri mitihani na yenyewe inalipiwa, tunalipia siku hizi. Kutafsiri kutoka Kiswahili uende Kiingereza sharti ulipie shilingi 8,500 kila mtihani, kila mwanafunzi, yaani hii ni kuumiza wazazi na lengo ni kuua shule. Kwa hiyo, nafikiri ili kutafuta ufumbuzi wa mambo haya, nimesoma taarifa ya Kamati, sio iliyosomwa hapa, ile ni summary, ile taarifa kubwa nimeisoma; imependekeza tuunde chombo huru cha kusimamia elimu, chombo huru, tuondoe suala la ukewenza. Huwezi kuwa na wake wanne, halafu uchague mmoja ndiye awe msimamizi wa wenzake. Serikali ina shule na binafsi wana shule, halafu Serikali ndio isimamie shule zote hizi, hapana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ilivyo ile TCU ya vyuo vikuu, Vyuo Vikuu vya Serikali kama Dar es Salaam, vya binafsi, viko chini ya TCU au TCIA ya ndege, ATCL za Serikali, Precision Air, ninii, ziko chini ya hiyo, basi na hii elimu iwe na chombo cha kusimamia shule zote Tanzania ili tuweze kuwa na ufanisi mzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)