Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Afya

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Afya

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nimpongeze sana Waziri wa Afya Ndugu Ummy Mwalimu na Naibu wake Dkt. Godwin Mollel na wataalam wa Wizara ya Afya kwa kazi nzuri wanazofanya kwenye kutekeleza wa Ilani ya CCM.

Mheshimiwa Spika, mimi nitachangia kuhusu changamoto ya watu wenye ulemavu na kuhitaji viungo bandia.

Mheshimiwa Spika, hapa nchini kuna wenzetu waliopatwa na matatizo yaliyosababisha kukatwa viungo vya mwili kama miguu na mikono. Watu hawa wamekuwa wakipambana kuirudisha furaha ya awali ili angalau waweze kushiriki mambo mbalimbali katika jamii ikiwa ni pamoja na kufanya shughuli zao walizokuwa wakifanya awali.

Mheshimiwa Spika, Mtanzania yeyote anaweza kupatwa na ulemavu wa kiungo kutokana na sababu nyingi ikiwamo kuzaliwa na kilema, ajali na kuugua saratani au kisukari. Kutokana na hilo, idadi ya walemavu wa viungo vya miguu na mikono imekuwa kubwa.

Mheshimiwa Spika, viungo bandia vina nafasi kubwa katika kutatua tatizo hilo. Hapa Tanzania ni watu wachache wameweza kupata huduma na idadi ya waliopo nyumbani ni kubwa zaidi kuliko wanaopata huduma hiyo.

Mheshimiwa Spika, naomba ieleweke kwamba kukatwa kiungo siyo mwisho wa maisha au kushiriki katika shughuli za kimaendeleo. Elimu ikitolewa, tafsiri inaweza kuwa tofauti kabisa na kuwarudishia matumaini ya kuishi Watanzania wenzetu waliokata tamaa.

Mheshimiwa Spika, uhitaji wa viungo bandia hapa nchini umeongezeka sana kutokana na ajali zitokanazo na matumizi ya vyombo vya usafiri kama pikipiki ambapo kumesababisha mrundikano wa wahitaji wa viungo bandia vya miguu na mikono.

Mheshimiwa Spika, waathirika wengi hufika hospitali, lakini wagonjwa hao wanapotajiwa kiwango cha fedha zinazohitajika ili wapatiwe huduma, idadi kubwa huondoka na hawarudi tena kutokana na gharama kubwa.

Mheshimiwa Spika, hospitali chache zenye huduma hizi ni pamoja na KCMC, Bugando, Taasisi ya Tiba ya Mifupa Muhimbili (MOI) na Dodoma General Hospital.

Mheshimiwa Spika, gharama za huduma hii huwa ni kubwa kutokana na bei ya malighafi ambazo huagizwa kutoka nje ya nchi. Kwa mfano, utafiti niliofanya nimebaini kuwa gharama za kuweka mguu (kutegemea na hospitali) ni kati ya shilingi milioni 1.5 hadi 3.5. Mkono ni takribani shilingi milioni mbili hadi 4.5. Gharama hizi ni kubwa sana kwa Mtanzania wa kawaida.

Mheshimiwa Spika, pamoja na bei kuwa juu, Mfuko wa Bima ya Afya (NHIF) hautoi malipo kwa watu wenye matatizo ya kuwekewa viungo bandia. Hii imekuwa ni changamoto kubwa hasa kwa watoto wanaokua, kwani huhitaji kabadilishiwa viungo mara kwa mara kila maumbile yao yanapobadilika.

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo yangu hapo juu, naishauri Serikali yafuatayo; kwanza naishauri Serikali kuandaa sera zitakazowezesha upatikanaji wa viungo hivyo kwa urahisi kutokana na hali ya uhitaji kuongezeka.

Pili, naishauri Serikali ijumuishe huduma hizi katika Bima za Afya (NHIF) ili watu waweze kupata huduma hiyo kwa uhakika.

Mheshimiwa Spika, tatu, naishauri Serikali ifanye tafiti ili kuwa na kanzidata ya waathirika na wahitaki wa viungo bandia.

Nne, naishauri Serikali kupitia vyuo vyetu hapa nchini izalishe idadi ya wataalamu watakaokidhi hitaji la kutoa huduma kwa wahitaji wa viungo bandia hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, tano, naishauri Serikali ipeleke huduma ya viungo katika hospitali zote za mikoa hapa nchini.

Sita, naishauri Serikali ihamasishe wadau kuanzisha vituo vya kutengeneza viungo bandia katika maeneo mbalimbali hapa nchini.

Saba, naishauri Serikali iwapatie ajira vijana wahitimu wa fani ya viungo katika maeneo mbalimbali hapa nchini; na nane, nishauri Serikali itoe elimu kwa uMma kuhusu uwepo wa viungo bandia ili wanufaike na huduma hii.

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo yangu hapo juu, naunga mkono hoja.