Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Afya

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Afya

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, napenda kuwashukuru na kuwapongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Dkt. Philip Isdor Mpango, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mawaziri na viongozi wote wa Wizara ya Afya kwa uongozi wao na utendaji uliotukuka.

Mheshimiwa Spika, napenda pia kutumia fursa hii kukupongeza wewe binafsi, Naibu Spika na uongozi wote wa Bunge kwa uongozi wenu mahiri na wenye ubunifu wa hali ya juu katika kuongoza mhimili wa Bunge.

Mheshimiwa Spika, napenda kumpongeza Waziri wa Afya kwa hotuba nzuri iliyojaa ubunifu mkubwa na imedhihirisha utayari wa Serikali katika utekelezaji wa sera ya afya ikienda sambamba na ustawi wa jamii na maendeleo endelevu na hii ni mojawapo ya nguzo kuu katika utayari wetu wa ushindani wa kimataifa (national competitiveness). Bajeti hii inaenda sambamba na Dhima ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2021/2022 – 2025/2026 ambayo ni Kujenga Uchumi Shindani na Viwanda kwa Maendeleo ya Watu.

Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha Awamu ya Sita, Serikali kupitia Wizara ya Afya, imetekeleza miradi mingi ya miundombinu ya afya. Katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya na kwa kushirikiana na TAMISEMI imeendelea kutekeleza kwa ufanisi mkubwa miradi ya Hospitali ya Wilaya na vituo vitano vya afya vya Kata za Ikukwa, Ilembo, Santilya, Ilungu na Swaya. Vituo vyote vitano vinaendelea kutoa huduma kwa ufanisi mkubwa hasa huduma ya watoto na wakina mama. Hospitali ya Wilaya pamoja na vituo vya afya vimekamilika na maandalizi ya vifaa tiba yapo katika hatua za mwisho ili vianze kutoa huduma kwa ukamilifu.

Mheshimiwa Spika, katika kipindi hiki tunapopambana na majanga magonjwa ya mlipuko ikiwemo la corona virus (covid-19), tumejifunza umuhimu wa utayari wa huduma ya afya hasa kwenye zahanati, vituo vya afya na hospitali na hivyo Serikali iongeze msukumo wa kupeleka vifaa tiba na kumalizia vituo vya afya na zahanati zilizojengwa kwa nguvu za wananchi. Katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya, wananchi wa Kata za Igoma, Isuto wamejenga vituo vya afya na kuna maendeleo mazuri ya kukamilisha na pia Mji Mdogo wa Mbalizi wenye wakazi zaidi ya 150,000 ujenzi wa kituo cha afya haujakamilika.

Mheshimiwa Spika, hivyo napendekeza Serikali kutoa kipaumbele katika bajeti hii kwa vituo vya afya hivi ili vianze kutoa huduma. Pamoja na vituo vya afya vya Ilungu, Igoma, Isuto na Mbalizi, napendekeza kukamilisha zahanati zote ambazo zimejengwa kwa nguvu za wananchi.

Mheshimiwa Spika, kutokana na maboresho ya miundombinu ya hospitali na vituo vya afya, Serikali ihakikishe bajeti ya mwaka huu inaendelea kujielekeza zaidi kwenye ajira ya madaktari na watumishi wa afya kwa ujumla. Pamoja na maboresho hayo ya miundombinu, vifaa tiba na ajira kwa watumishi, napendekeza Serikali ikamilishe mpango kabambe na Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote na hasa kwa wazee na wenye mahitaji maalum.

Mheshimiwa Spika, napendekeza Serikali iangalie jinsi ya kuboresha Bohari ya Madawa (MSD) ikiwa ni pamoja na Serikali kuhakikisha inaongeza mtaji wa MSD na kuboresha muundo wa shirika ili uendane na jukumu kubwa kutoa huduma kwa tija na ufanisi. Katika kipindi hiki ambapo Serikali inaangalia kuanzisha Bima ya Afya kwa Wote, kipaumbele kielekezwe kwenye maboresho ya upatikanaji wa madawa pamoja na madawa na kuwezesha huduma ya hospitali zetu kutoa huduma bora zaidi kwa ukanda huu wa Afrika.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.