Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Afya

Hon. Mariamu Nassoro Kisangi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Afya

MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Nami kwanza nianze kumshukuru Mungu kwa kunipa uwezo wa kusimama kwenye Bunge lako Tukufu hili katika Bunge hili la Bajeti leo ikiwa mara yangu ya kwanza kusimama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru na kukupongeza sana kwa uendeshaji wako wa Bunge pia napenda nimshukuru Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan, pongezi hizi nampa kwa yale yote aliyoyafanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alitembea nchi nzima kuitangaza Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2020/2025, katika ukurasa wa 124 mpaka 141 wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi, Mheshimiwa Rais wetu ameitekeleza kwa vitendo. Ninasema hivyo katika ukurasa wa 31 wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi, kifungu cha 88 kuanzia kifungu kidogo (a) mpaka
(k) ameonesha Ilani ile kwamba kutafanyika ujenzi na ukarabati wa vituo vya afya, ujenzi wa hospitali za Wilaya, ujenzi wa hospitali za Mikoa, ujenzi wa hospitali za Kanda. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hayo yote Mheshimiwa Rais wetu ameyaweza. Pia ameeleza upatikanaji wa vifaatiba, kusafisha damu, dialysis, CT scan, MRI. Hivyo vyote vitafanyika katika sekta ya afya na hayo Mheshimiwa Rais ameyatekeleza kwa vitendo. Pia ameeleza katika ilani hiyo hiyo kuongeza watumishi katika kada ya afya. Hilo linaendelea kutekelezwa lakini limeanza kutekelezeka kwa hayo yote pia amesema matibabu ya kibingwa yapatikane ya figo, moyo, uzazi (kupandikiza uzazi). Hayo yote ndugu zangu yanatekelezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wakina mama tulikuwa na changamoto kubwa ya uzazi kuita ugumba, sasa hivi uzazi unapandikizwa katika hospitali zetu za Dar es Salaam za Tanzania, wanapandikiza uzazi kwa akina mama na tunaweza kupata watoto na jambo la ugumba sasa limeondoka. Hayo yote ni makubwa ambapo ameyafanya Mheshimiwa Rais wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hayo anayoyafanya kwa kweli tunastahili tumpongeze na tunampongeza sana sana sana kwa sababu ameweza yale aliyoyataka kuyatekeleza, ameyasimamia na yametekelezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya pongezi hizo napenda sasa nimpongeze Mheshimiwa Waziri na Naibu wake Waziri, kwa kazi kubwa anayoifanya. Ni Waziri mahiri na Naibu Waziri mahiri wana ushirikiano mzuri kwa kweli tunashukuru. Pia watenda kazi Waheshimiwa Makatibu Wakuu na Naibu Makatibu Wakuu na Watendaji wote wa Wizara hii kwa pamoja wanafanya kazi nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa nirudi katika mchango wangu. Mchango wangu nitaanza na Hospitali ya Muhimbili. Kwa kweli mambo mazuri yanafanyika katika Hospitali ya Muhimbili na niipongeze sana Serikali. Nilisimama hapa kuomba wodi ya wagonjwa wa akili Muhimbili kwamba imeachwa ikiwa chakavu, chafu haijapata urekebisho. Hivi ninavyokwambia, wodi imekarabatiwa vizuri bado sehemu chache. Kwa maana hiyo Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi ni sikivu, inachukua maoni yetu na inayafanyia kazi. Wodi ile iko vizuri bado asilimia kama 20 tu kukamilika kabisa. Hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia katika Mfumo mzima wa matibabu. Katika Hospitali ya Muhimbili kumekuwa na mabadiliko na mageuzi makubwa. Mimi nikiwa nje alikuja binti kuniambia amesema mimi nimelazwa pale Muhimbili lakini nilipotoka mama nakwambia angalia baada ya miaka miwili tutazungumza mengine Muhimbili tutakuwa kama India labda. Baada ya miaka miwili mambo niliyoyaona ndani, ananiambia binti tu kama wa miaka 28 umeona nini ananiambia mama siyo ile Muhimbili unayoijua wewe. Muhimbili imebadilika, ina mambo mazuri, ina matibabu mazuri. Kwa hiyo, mimi nalipongeza na wananchi wanapongeza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na pongezi hizo iko changamoto Muhimbili. Changamoto ni wananchi wanaoenda kuangalia wagonjwa bado hawajapata sehemu sahihi ya utulivu. Kule kunakuwa na wagonjwa wengine mahututi hawajiwezi. Mgonjwa wako akiwa mahututi huwezi kuwa na akili ya kukaa nyumbani, kwa vyovyote utakuwa mazingira yale yale unasubiri. Sasa pale unaposubiri inakuwa tatizo. Niiombe Serikali itenge eneo maalum, wale watu wanaosubiri wagonjwa wao wakae huko, wakisubiri wagonjwa wao baada ya masaa matatu manne kwenda kuwaona. Kwa kawaida sisi Waafrika tunafarijika zaidi unapougua ukimuona ndugu yako wa karibu. Utapewa matibabu ya kila aina, utapewa kila huduma na Nesi lakini ukimuona ndugu yako wa karibu unafarijika zaidi. Hivyo hilo nalo tulizingatie kwa sababu wale wagonjwa wanakuwa wanahitaji counsel na kuwa-counsel kwa kwanza kumpa mtu ambaye anampenda ili aweze kupata nafuu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia naipongeza kuna wodi maalum ya wazazi ambayo imeanza kuzingatia, wao wanakwenda na wenza wao na watu wa kuwahudumia, iko pale Muhimbili hapa jirani na kanisani hapa, kuna wodi nzuri tu ya wazazi lakini bado ni ya kulipia, tumeanza ninayo imani huko tunakoenda tutaangalia mifumo hiyo, kwa sababu hata tunapoenda kwenye nchi za wenzetu mgonjwa amelala pale lakini hapa kunakuwa na kochi la muuguzaji anamuangalia mgonjwa wake. Najua tulikotoka ni mbali na tunakoenda ni mbali. Hapa tulikofika siyo haba, tunamshukuru Mungu kwa yote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba sasa nizungumzie Taasisi ya Afya ya Ocean Road ya kansa. Taasisi ile imekuwa na ongezeko kubwa la wagonjwa siku hadi siku, imekuwa na changamoto kubwa ya ucheleweshaji wa vifaa vya matibabu kutokana na taratibu za kikodi. Sasa niiombe Serikali kuwa ile taasisi inategemewa na watu wengi na tunaona wakina mama ndiyo wanaongoza kwenye kuwepo pale wagonjwa wa kansa ya kizazi, lakini pia zaidi siyo kina mama hata akina baba kansa ya tezi dume inazidi kushamiri ukienda unawakuta wengi tu pale wana matatizo hayo. Sasa vifaa vile tunavihitaji kwa afya, inakuwaje tena kunakuwa na tatizo la kikodi?

Mheshimiwa Spika, Serikali iweke mifumo sahihi na iliyo wazi. Leo tunakwenda kununua wenyewe kwa fedha zetu za Tanzania, tunaenda kununua vifaa nje tulete kwenye hospitali yetu ya Ocean Road vinakwama, je, Mfadhili akitaka kutuletea vifaa ndiyo vitaingiaje kama sisi wenyewe vina kwama kwa matatizo ya kikodi. Naomba hilo mliangalie Serikali na Wizara ya Fedha tunavihitaji, tatizo la kansa ni kubwa watu wanahitaji huduma hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa nije kwenye hospitali ya Mloganzila, kwa kweli tunashukuru sana hospitali ipo nzuri lakini nayo changamoto yake kubwa ni gharama za matibabu. Wagonjwa, mtu anaumwa akiulizwa unanipeleka wapi? Mlaganzila, aah! naenda kufa mama, nini? Watoto wangu wataweza hizo bili? Eeh! Ile hospitali hivi mfumo wake hasa wa bill ukoje? Mbona watu wanashindwa kuelewa? Kwa sababu mwisho wa yote mtu yule anaugua, anakufa, maiti inakwama, Mbunge hukai Bungeni, unahangaika, unateseka, unaambiwa ukamkopeshe mtu hela za kwenda maiti, nazipata wapi ghafla shilingi milioni saba, nane? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaiomba Serikali siyo Mloganzila tu, Muhimbili, Mloganzila ituwekee mpango sahihi juu ya hizi tiba, watu wanakwama, kila ukienda yaani mpaka tunaogopa, ukifika Muhimbili tu ukienda maeneo ya watu wengi utakumbana na tatizo hilo. Ukiwa Bungeni utakumbana na simu hizo. Kweli tunakwenda pale, wengine tunawaelezea lakini wako watu ambao hamjui hata Mbunge wake, hivi huyu anatokaje?

Mheshimiwa Spika, ninaiomba Serikali iweke utaratibu mzuri utakaoeleweka, kwamba huyu mtu ana uwezo na ikiwezekana mtu aambiwe mapema, umeingia hapa kwenye wodi hii itakubidi ufanye hivi, uweke advance hii ili hapa ukitoka tena isiwe tatizo. Ninaona Mheshimiwa Waziri unatoa taarifa, unajitahidi kutoa taarifa, jamani maiti isizuiwe lakini inafika sehemu hali ni ile ile. Sasa hii kitu sisi kama wananchi tunafanyaje kutoka hapo?

Mheshimiwa Spika, sasa nije kwenye suala zima la afya ya mama na mtoto. Mimi niombe Serikali…

SPIKA: Dakika moja malizia kengele imeshagonga ya pili.

MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Spika, namalizia mchango wangu. Naiomba Serikali iangalie huduma ya afya ya mama na mtoto iwe bure, bure ya kweli. Mama kliniki afanye bure, kwa sababu hata wanaoenda na bima unachajiwa. Sasa kwa nini na sisi tunataka afya ya mama na mtoto iwe bure kwa wote?

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)