Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Afya

Hon. Dr. Alfred James Kimea

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Korogwe Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Afya

MHE. DKT. ALFRED J. KIMEA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii nami niweze kuchangia kwenye Wizara hii ya Afya. Awali ya yote, nitumie fursa hii kuushukuru uongozi wa Wizara; moja, dada yangu Mheshimiwa Ummy Mwalimu, na kaka yetu Mheshimiwa Dkt. Godwin Mollel. Pia nawapongeza Dkt. Self Shekalaghe pamoja na dada yetu Grace Maghembe kwa kazi kubwa wanayoifanya kuhakikisha sekta ya afya kwenye nchi hii inapewa kipaumbele.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo, naishukuru na kuipongeza Serikali yetu ya Awamu ya Sita kwa kazi kubwa ambayo imeifanya hasa kwenye sekta ya afya. Wote tunashuhudia kazi kubwa Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ameifanya kwenye sekta hii ya afya. Wote tunashuhudia ujenzi wa hospitali za kikanda, hospitali za rufaa za mikoa, hospitali za wilaya na vituo vya afya na zahanati. Kimsingi, Serikali yetu imefanya kazi kubwa sana, hivyo hatuna budi kuipongeza.

Mheshimiwa Spika, hususan kwenye Jimbo langu la Korogwe mjini, kazi kubwa kwenye sekta ya afya imefanyika, hivyo sina budi kuipongeza Serikali yetu. Mfano, kwenye jimbo langu la Korogwe Mjini kwa kipindi hiki, Mheshimiwa Dkt. Samia akiwa Rais, ameshatujengea vituo vya afya viwili. Moja, kwenye Kata inaitwa Mgombezi na kingine kwenye Kata ya Kwamsisi. Pamoja na hilo, tumejengewa EMD kwenye hospitali yetu ya Wilaya na zahanati karibu kwenye kila Kijiji. Kwa hiyo, hiyo ni kazi kubwa ambayo Serikali yetu imeifanya kwenye sekta ya afya na hatuna budi ya kuipongeza sisi kama wawakilishi wa wananchi.

Mheshimiwa Spika, pamoja na jitihada kubwa ambazo Serikali imefanya, bado ziko changamoto chache ambapo leo napenda kuzieleza ili Wizara yetu hii ya Afya ikapate kuzichukua na kuzifanyia kazi, hasa nitajikita moja kwa moja kwenye Jimbo langu la Korogwe Mjini.

Mheshimiwa Spika, ni kweli tumejengewa vituo vya afya kama nilivyoeleza hapo mwanzo, lakini hadi sasa hivi bado hatujaletewa vifaa tiba. Hivyo naomba Wizara, Mheshimiwa Waziri, basi tupatiwe vifaa tiba ili vituo vile vya afya vizuri kabisa ambavyo Serikali imejenga viende kufanya kazi na wananchi wa Korogwe waweze kunufaika na matunda ya Serikli yao ya Awamu ya Sita.

Mheshimiwa Spika, ukiacha vifaa tiba, changamoto nyingine inayotukumba kwenye Halmashauri yetu kwenye sekta ya afya ni upungufu mkubwa wa watumishi kwenye sekta hiyo. Kwenye Halmashauri yetu ya Korogwe Mjini, ili kukidhi mahitaji ya sekta ya afya tunatakiwa kuwa na wafanyakazi zaidi ya 700, lakini hadi sasa tuna wafanyakazi chini ya 300, hivyo tuna upungufu wa wafanyakazi 400.

Mheshimiwa Spika, upungufu huo hasa kwa wataalam wa maabara, wauguzi pamoja na wafamasia. Hivyo, tunaishauri na tunaiomba Serikali yetu ikapate kuendelea kuajilri watumishi wa afya kama ilivyofanya hapo awali ili wakapate kuweza kuongezeka na vituo vile ambavyo tumejenga vikapate wataalamu ili wananchi wetu waweze kuhudumiwa vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, changamoto nyingine ambayo napenda kuizungumzia leo, ni changamoto ya usafiri. Kwenye Halmashauri yetu ya Korogwe, kwenye jimbo langu, kwenye hospitali zetu tuna uhaba mkubwa sana wa usafiri hasa ambulance lakini pamoja na magari mengine ya administrative supervision na kazi nyingine. Hivyo, tunaiomba Serikali ikapate Kwenda kutupatia ambulance kwa ajili ya vituo hivi vya afya lakini pamoja na hospitali yetu ya wilaya.

Mheshimiwa Spika, changamoto nyingine ambayo napenda kuieleza kwenye sekta ya afya kwenye jimbo langu ni uchakavu wa miundombinu. Nilikwisha kueleza hapa Bungeni si mara moja kwamba, Hospitali yetu ya Korogwe, hospitali yetu ya wilaya ni chakavu sana na imechoka ilijengwa tangu mwaka 1952 na haikidhi kabisa matakwa ya kuhudumia watu wetu kwa kipindi hiki. Nimekwisha kuomba mara nyingi lakini nipende kuishukuru Serikali kupitia Wizara ya TAMISEMI, kwenye bajeti hii imetutengea shilingi milioni 900 kwa ajili ya ukarabati wa hospitali ile.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa na ushauri kidogo mahali hapa, naomba Waziri wa Afya akae na Waziri wa TAMISEMI, ili wapate kukubaliana jambo hili. Hospitali yetu ya Korogwe ambayo ni chakavu na hospitali nyingine kwenye nchi hii, hospitali zile kongwe na chakavu zimepelekewa fedha kwa ajili ya ukarabati shilingi milioni 900.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu, fedha hizi zisiende kufanya ukarabati hatutaona value for money, fedha hizi ziende kujenga majengo mapya. Safari hii mmetupatia milioni 900 basi tucahgue majengo gani yatajengwa na milioni 900 safari hii na mwakani mtupatie nyingine zikajenge majengo mengine. Mkisema muende kukarabati hela zitisha na hamna kitu kitakacho onekana pale. Hatutapata value for money kwa ajili vijengo ni vidogo designing yake ni ya miaka 60 iliyopita, tunakwenda kukarabati kitu gani?

Mheshimiwa Spika, hivyo ninamuomba Waziri wa Afya akae na akabualiane na Waziri wa TAMISEMI, wakubaliane ili hizi hela zisiende kufanya ukarabati. Watu watakwenda kupiga piga rangi, watabadilisha mabati, tiles kidogo hamna kitu kitakachoonekana baada ya miaka miwili tutakuwa na uhitaji mwingine. Hivyo, fedha hizi ziende kujenga majengo mapya naamini miaka miwili mpaka mitatu tutapata hospitali mpya kabisa ambazo zitakidhi mahitaji ya karne hii, sio kukarabati hozpitali za miaka 50 iliyopita. Huo ndio ulikuwa ushauri wangu.

Mheshimiwa Spika, la mwisho, Mheshimiwa Waziri, naomba hili ulielewe vizuri dada yangu, najua wewe ni mpambanaji na unaweza. Serikali imefanya pakubwa, imejenga majengo, inaajiri wataalam, vifaa tiba na hadi sasa hivi tuna madawa ya kutosha.

Mheshimiwa Spika, changamoto tuliyokuwa nayo ni malalamiko ya wagojwa juu ya wauguzi na wataalam kwenye hospitali zetu. Kumekuwa na malalamiko mengi kwenye hospitali zetu za halmashauri wagonjwa wanalalamika hawawi–treated vizuri na wauguzi wetu. Hivyo, Mheshimiwa Waziri, ushauri na rai yai yangu kwako, hebu fanya uchunguzi kwenye hospiali za Halmashauri ya Korogwe Mjini lakini na hospitali nyingine kwenye taifa hili uweze kuangalia ni kwa ajili gani wagonjwa wanalalamikia wauguzi.

Mheshimiwa Spika, kama shida ipo, basi mfuatilie mjue ni shida gani inawezekana wauguzi wetu wanakuwa over worked, inawezekana watu ni wachache au hawapati stahili zao vizuri. Basi muende kufuatilia changamoto hizi ili muweze kuzitibu ili waweze kuhudumia wananchi wetu vizuri. Mnafanya kazi kubwa lakini wagonjwa wetu wasipohudumiwa vizuri itakuwa ni kazi bure, hivyo Mheshimiwa Waziri nakuomba.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hilo ninatamani pia wawe wanapewa elimu ya mara kwa mara ethical education na vitu vingine. Waambiwe ni namna gani wao ni muhimu kwenye afya ya watanzania. Mheshimiwa Waziri, hayo ni machache ya kwangu niliyokuwa nayo.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii, nilikuwa na hayo machache kwenye bajeti hii ya Wizara ya Afya. Ahsante sana. (Makofi)