Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Afya

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Afya

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa fursa, na ninaomba niendelee pale nilipoachia.

Mheshimiwa Spika, kwa pesa ambazo Serikali imetoa katika Wizara hii ya Afya, tumeona Wizara imefanya mambo mengi makubwa ambayo ni faraja kwa Watanzania wote. Kuna huduma za kinga ambapo tunapata chanjo za pepopunda, kifaduro, kupooza, surua mpaka UVIKO. Kuna huduma za lishe, huduma za usafi wa afya na mazingira, huduma za afya mipakani kwa wasafiri wanaoingia Tanzania kuzuia ujio wa magonjwa mapya na huduma za kibingwa ambazo zimefanywa na vijana wetu wa Kitanzania.

Mheshimiwa Spika, nampongeza sana Waziri, juzi niliguswa hasa nilipomwona yule mtoto aliyekuwa na Selimundu mkamleta hapa, mkatuambia dada yake, Esther, ndiye aliyetoa uroto akamsaidia kaka yake, na yule mtoto amepona, Waziri na wataalam wetu, tunawapa big up, hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naiomba Serikali, hawa mabingwa wetu wa figo, wa kupasua ubongo bila kupasua fuvu, moyo na Selimundu tuendelee kuwapa nguvu ili waendelee kuwahudumia Watanzania. Chonde chonde, najua mmeshaanza, lakini tuongeze nguvu zaidi, kwa sababu ukienda kwenye Kliniki za Selimundu, utaona ule huruma vile vitoto vinavyoteseka. Kama tiba tayari imeshapatikana, naomba sana tuendelee kuwapa nguvu Wizara ili watekeleze hilo.

Mheshimiwa Spika, niongee kwa kifupi kuhusu Hospitali ya KCMC, ni hospitali bingwa inayofanya vitu vingi. Pale kuna uhaba wa madaktari na watumishi wengine. Wana-operate at fifty percent capacity. Kwa hiyo, naomba mwaongezee watumishi ili waendelee kutoa huduma kwa Watanzania ambao wanaopelekwa pale kupata tiba.

Mheshimiwa Spika, sasa nizungumzie masuala machache kwenye jimbo langu kabla sijachangia kitu ambacho nilitaka kusema. Naishukuru Serikali, imetujengea Hospitali ya Wilaya pale Mabogini. Ni eneo ambalo lina watu wengi, karibu 20.3 percent ya wakazi wa jimbo langu wametoka pale. Kwa hiyo, tunashukuru sana, hospitali ile imekamilika. Naendelea kuomba Wizara itupelekee vifaa, dawa na vitu vingine ili wananchi waanze kupata huduma. Katika Hospitali ya Kibosho, nilikuwa nimemwomba Waziri anipatie digital x-ray, bado wanangojea kule Kibosho Hospital. Chonde chonde, dada yangu Mheshimiwa Ummy, hii ni ahadi, wananchi wanaingojea, mwendelee kutusaidia.

Mheshimiwa Spika, mchango wangu wa leo utajikita kwenye changamoto ya watu wenye ulemavu na wanaohitaji viungo bandia. Hapa Tanzania kuna wenzetu wengi ambao wana ulemavu na wanahitaji viungo bandia kwenye miguu na mikono. Kinachosababisha hao watu wawe na ulemavu ni nyingi. Kwanza, wanaweza wakawa wamezaliwa hivyo; ya pili, wanaweza kuwa wamepata ajali; wengine wameugua saratani na kisukari wakaishia kukatwa mikono na miguu; na sasa hivi hali ilivyo, vijana wetu wa bodaboda wamejiajiri kule, wanaendesha boda boda na bahati mbaya tunawagonga, yeye na abiria wanaishia kukatwa mguu au mkono.

Mheshimiwa Spika, sasa idadi ya hawa wagonjwa imekuwa kubwa na ninaomba Serikali iangalie kwa jicho la pekee kwa sababu hili kundi hatujaliangalia vizuri. Linahitaji viungo bandia na hawa watu wanahitaji warudie maisha yao ya zamani ili waweze kuchangia kwenye uchumi wa Taifa, lakini kwa kuwa hakuna hivi viungo, basi wanakuwa na mateso makubwa sana.

Mheshimiwa Spika, ni kwa nini watu wachache ndio wamepata hii huduma? Ni kwamba, kwanza kabisa hospitali zilizopo zinazotoa huduma ya viungo bandia ni chache hapa nchini. Kwa haraka haraka ninajua kuna KCMC, kuna Bugando Hospital, kuna MOI na Dodoma General Hospital. Hiyo ni sababu ya kwanza. Kwa hiyo, tunaomba huduma hii isambae kwenye hospitali za mikoa ili watu watibiwe kwenye hospitali zao za mikoa huko huko.

Mheshimiwa Spika, sababu ya pili ni gharama za viungo kuwa ni kubwa sana. Viungo bandia, kumwekea mtu mguu, kwa utafiti nilioufanya mimi ni kati ya shilingi milioni 1.5 mpaka shilingi milioni 3.5; na mkono ni kati ya shilingi milioni mbili mpaka shilingi milioni 4.5. Sasa kwa Mtanzania wa kawaida, hao wenye saratani waliokatwa mikono na miguu, ni wazee ambao hawajiwezi kabisa. Kwa Mtanzania wa kawaida, hii gharama ni kubwa sana. Naomba Serikali iwaangalie hawa watu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kitu kingine kikubwa ni kwamba Mfuko wetu wa Taifa wa Bima ya Afya, mfuko wetu pendwa, hautoi huduma kwa viungo bandia. Yaani wewe ukiugua, kama ukikatwa mguu, unatakiwa ujilipie mwenyewe. Namwomba Waziri atakapo kuja ku-wind-up hapa atusaidie kwa sababu kuna watu wanateseka huko, ni wengi kweli kweli.

Mheshimiwa Spika, sasa nitoe ushauri kwa Serikali kwamba, chonde chonde, ijumuishe viungo bandia kwenye Mfuko wa Taifa wa Bima yetu ya Afya. Watu wanapopata ajali akikatwa mguu, kama anahitaji kiungo bandia, basi iwe kwenye huduma ambazo zinaweza zikatolewa na Mfuko wa Taifa wa Bima yetu ya Afya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kitu cha pili, naishauri Serikali, ikiwezekana tufanye utafiti. Kuna watu wengi sana wako huko ambao, akishaenda hospitali akiambiwa gharama ni kubwa, anarudi nyumbani kwenda kufa peke yake tu. Tufanye utafiti, tupate kanzidata ya wagonjwa ni wangapi ambao wana hili tatizo ili tuweze kuwasaidia.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu wa tatu kwa Serikali ni kwamba Vyuo vyetu Vikuu vya Afya ambavyo vipo vingi, vimetapakaa nchi nzima, vifundishe wataalam wa hii fani ili waweze kuwahudumia Watanzania wenzao ambao wana hili tatizo. Kama nilivyosema awali, napendekeza pia hii huduma isiishie kwenye zile hospiatli nne tu ambazo zipo sasa hivi, iende kwenye hospitali zote za mkoa. Kila mkoa uwe na kitengo ambacho kitakuwa kinasaidia hawa wagonjwa ambao wana hili tatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu mwingine kwa Serikali, ikiwezekana ihamasishe wadau wa maendeleo au Serikali yenyewe, kila mahali penye hii huduma pawe na Unit ya kutengeneza hivi viungo bandia ili watu waweze kupata huduma hapo kwa hapo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu wa mwisho ni kwamba, wahitimu ambao wameshahitimu hapa nchini, tunao ambao wamesoma KCMC, Serikali iwape ajira na iwapeleke huko mikoani ili waweze kutoa huduma kwa watu ambao wana hili tatizo la viungo bandia.

Mheshimiwa Spika, kingine muhimu, elimu itolewe kwa watu ambao wameshapata hili tatizo kwamba ukikatika mkono au mguu siyo mwisho wa maisha. Unaweza ukavaa kiungo bandia ukaendelea na shughuli zako kama ilivyokuwa awali. Ikiwapendeza, mbadilishe sera itakayotoa umuhimu wa kutatua tatizo hili katika nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, mwisho kabisa niseme kwamba wagonjwa wengi ambao wana hili tatizo la kukatwa miguu na mikono, hukwazika kwa kiwango kikubwa cha gharama ambazo nimezitaja hapa. Naiomba Serikali, chonde chonde, tuangalie namna ya kuweka kwenye mifumo yetu ili ndugu zetu ambao wamepata haya matatizo waweze kuhudumia na Serikali yao pendwa.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)