Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji

Hon. Jumaa Hamidu Aweso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Pangani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji

WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, awali ya yote kwanza nimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya njema pamoja na ninyi sote na kuweza kuchangia bajeti ya Wizara yetu ya Maji. Waheshimiwa Wabunge, Mwenyezi Mungu awabariki sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Bunge lako Tukufu limeweza kujadili bajeti yetu ya Wizara ya Maji ya Mwaka 2023/2024 niliyoiwasilisha hapa Bungeni tarehe 10 Mei, 2023.

Mheshimiwa Spika, naomba nitoe shukrani zangu za dhati kwako wewe binafasi kwa kazi kubwa na usimamizi mzuri katika Bunge lako hili Tukufu lakini kama kiongozi kijana yako mengi ambayo nimejifunza kutoka kwa Spika wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo moja ambalo nimejifunza kutoka kwako, kwamba hata uwe kiongozi na cheo kikubwa namna gani usisahau ulipotoka. Hata uwe na nyadhifa kubwa namna gani usiwasahau unaowaongoza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimepata dhamana ya kuwa Waziri wa Maji, niliwahi kufika pale Mbeya, pamoja na kuwa Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, hujaacha hata siku moja kuwasemea wananchi wako katika Jiji la Mbeya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka nikutie moyo, upo msemo unaosema” ukipigana vita ugenini nyumbani lazima kuwe na amani” pamoja na bajeti hii ambayo tunayopitisha, tunajua ombi ambalo ulilotupa kwetu sisi kama wizara, tunatekelea mradi wa bilioni 117 pale Mbeya na Advance payment tumekwishaitoa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii kumpongeza Naibu Spika, pamoja na wenyeviti wote wa Kamati, kwa namna walivyoweza kusimamia bajeti yetu ya Wizara yetu ya Maji. Lakini kwa namna ya kipeke usione vyaelea ujue vimeundwa. Leo tunapongezwa Wizara yetu ya maji sio jambo jepesi sana. Mageuzi haya ambayo sisi kama viongozi wa Wizara ya Maji ambao tumeshirikiana na wenzangu haikuwa Rais. Kwa sababu tulipoyaleta katika Bunge lako Tukufu tulipata baraka zote. Hatuna cha kuwalipa Waheshimiwa Wabunge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo kabla sijaja kuhitimisha bajeti yetu, hivi mchana nilikuwa nimekaa na watendaji wetu wa wizara tulikuwa tunaangalia na kuweza kutoa commitment ya utekelezaji wa zile hoja ambazo zimetolewa na Waheshimia Wabunge. Moja wa mtendaji wetu alisimama na akasema Mheshimiwa Waziri, naomba utufikishie salamu kwa waheshimiwa wabunge. Pamoja na ukurugenzi wangu nimefanya kazi katika Wizara ya Maji leo inafika miaka 20. Wizara yetu hii ya Maji ilikuwa wizara ya kero na lawama tu. Kila tukija Bungeni hali ilikua ni tete sana. Leo Waheshimiwa Wabunge wanatupongeza, Waheshimiwa Wabunge, Mungu awabariki sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, funzo ambalo mmetupatia sisi kama viongozi na watendaji wa Wizara ya Maji, huna sababu ya kujitutumua wewe fanya kazi watu wanaona. Mmetutia moyo, mmetutupia nguvu kubwa sana. Commitment ambayo nimepewa na watendaji wetu wa Wizara ya Maji, kusema katika Bunge hili Tukufu na kumwambia Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, wanasema kama betri ambalo lilikuwa linachajiwa sasa liko full charge watafia site. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wametoa slogan katika kikao ambacho kilichokaliwa leo, wamesema slogan ya sasa ya Wizara ya Maji, itakuwa Die empty. Watatumia maarifa yao, watatumia nguvu zao kuhakikisha azma ya Rais wetu Mama Dkt. Samia Suluhu Hassan, kuhakikisha maelekezo na target za Chama cha Mapinduzi kwamba itakapofika mwaka 2025, asilimia 85 ya upatikanaji wa maji vijijini na asilimia 95 ya upatikanaji wa maji Mjini tunakwenda kuitekeleza kwa dhati kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wamenituma niwaeleze waheshimiwa wabunge, pongezi ambazo mmezitoa wanadeni kubwa sana. Wanasema kwamba ukicheza ngoma lazima uangalie na jua. Maji ni pamoja na uhai, maji ni pamoja na huduma muhimu lakini maji ni siasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge, michango yenu ambayo mmeieleza katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, utekelezaji wake maana yake ni kuhakikisha kwamba mnarudi. Kwa hiyo, sisi watendaji wa Wizara ya Maji, pamoja na kazi ya kupeleka maji lakini tuna kazi ya kulinda majimbo ya Waheshimiwa Wabunge katika kuhakikisha mnarudi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wizara yetu ya Maji kama nilivyoeleza hakuna hata mmoja asiyejua. Mheshimiwa Rais, aliwahi kuhutubia katika Bunge hili la Jamhuri ya Muungano tarehe 22 Aprili, alinisimamisha pale akatoa maelezo mahususi kwamba, yeye ni mama na hataki kusikia, hataki kuona wamama wa Taifa hili wanahangaika juu ya adha ya maji. Pia, akaenda mbali zaidi akaniambia, Waziri wa Maji, wewe unawaambia watendaji wako ukinizingua nitakuzingua.

Mheshimiwa Spika, hakuna siku ngumu katika maisha yangu kama siku ile. Niliweza kukaa na watendaji wangu kwa kina nikawauliza swali moja, je, hii kazi tunaiweza au hatuiwezi? Wameniambia hii kazi tunaiweza. Nataka niwambie pongezi hizi ambazo waheshimiwa mmezitoa, nataka nizirudishe kwa watendaji wote wa Wizara ya Maji. Waheshimiwa Wabunge, pongezi hizi zote ambazo mmezitoa naomba nizirudishe kwa Rais wangu Mpendwa, Samia Suluhu Hassan, ambae ameasisi kauli ya kumtua Mama ndoo kichwani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, moja ya chanagamoto kubwa ya Wizara yetu ya Maji juu ya utekelezaji wa maji ni ufinyu wa bajeti. Ipo miradi ambayo sisi tumeikuta ambapo hata mimi sijawahi hata kumaliza chuo au sekondari. Kwa Mfano, ukienda Serengeti kulikuwa kuna mradi unaitwa Mugumu na kweli mgumu kweli kweli. Zimepita awamu zote mradi ule haujakamilika. Waziri ukija hapa kimbembe chake si mchezo. Mradi ule Mugumu umemalizwa na Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna miradi ilikuwa ya kichefuchefu ambapo imejengwa unaweza ukawa kiongozi ukafika pale ukauzindua mradi, maji yanatoka leo ukiondoka unaondoka na maji yako. Wananchi wanateseka pesa zimetolewa, Mwakitolyo, Nyantukuza kule Nyang’wale lakini Mheshimiwa Rais alitupa maelekezo miradi ile ambayo ilikuwa ikiitwa kichefuchefiu ambayo tuliianisha 177, Waheshimiwa Wabunge mlipitisha mageuzi ya kuanzisha wakala wa maji vijijini RUWASA kwa ajili ya kwenda kutatua matatizo ya maji. Miradi 157 yote tumeikwamua watu wanapata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wizara yetu ya Maji, ilikuwa inafanya sasa mageuzi. Nini? kwa maana ya designing manual, ipo miradi ilikuwa inajengwa kwa gharama kubwa sana. Kwa mfano, ukienda kwa Kaka yangu Festo, kuna miradi ambayo ilitakiwa kutekelezwa zaidi ya billioni sita, sisi tukasema hapana. Matamba - Kinyika, tulifika pale tukasema miradi hii haiwezi kutekelezwa hivi. Wewe unapokuwa Mhandisi wa Maji wewe umesomea maji. Badala ya kumpa mkandarasi hebu tuone uwezo wako, mradi ule umejengwa kwa bilioni mbili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukienda Shinyanga Vijijini mradi ambao unaitwa Muze Group ambao ulitaka kutekelezwa kwa zaidi ya bilioni tano tukasema hapana. Tunaposema mhandisi wa maji wewe umesomea maji unaweza kufanya hiyo kazi. Tumewapa ile kazi wameweza kutekeleza hata bilioni haijakamilika mradi umekwisha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Ukienda zako Babati mradi ambao unaitwa Singu Sibino, na Kamati ilifika imejionea, ulitakiwa kujengwa na mkandarasi kwa zaidi ya bilioni 20, tukasema hapana wataalamu mtafanya hii kazi. Wameifanya, na leo hata bilioni 12 haijakamilika na ule mradi unaenda kukamilika na watu wanapata maji.

Mheshimiwa Spika, nini maana yangu; niwashukuru sana viongozi wetu wakuu. Mheshimiwa Rais, Makamu wa Rais, Mheshimiwa Waziri Mkuu alikuja kutufungulia, nakumbuka pale Chuo Kikuu cha Mipango; Design Manual kwamba kila mhandisi wa maji katika Wizara ya Maji anapotaka ku-design lazima afuate design manual.

Mheshimiwa Spika, hatuweze kutekeleza miradi ya maji hapa Dodoma eneo moja lakini kila tenki saizi moja lakini gharama tofauti, haiwezekani. Tumeanzisha Chuo cha Maji kwa minajili ya kuwatumia wataalamu wasaidie sekta ya maji, mageuzi haya leo tunawapongeza ni kazi kubwa ambazo mmezifanya Waheshimiwa Wabunge, Mwenyezi Mungu atawabariki sana na mtakumbukwa katika historia ya Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukitaka kufika haraka nenda zako mwenyewe, lakini ukitaka kufika mbali nenda na wenzako. Nitumie nafasi hii kumshukuru sana Naibu Waziri Maryprisca Mahundi, nitumie nafasi hii kumshukuru sana Katibu Mkuu wangu wa Wizara ya Maji Engineer Nadhifa Kemikimba - STK, mama wa sheria, taratibu na kanuni. Pia nitumie nafasi hii kumshukuru Naibu Katibu Mkuu wetu wa Wizara yetu ya Maji Engineer Cyprian Luhemeja, kwa muda mfupi na Menejimenti ya Wizara ya Maji na watendaji wote wa Wizara ya Maji Mwenyezi Mungu ndiye atakayewalipa; tutafanya kazi. Hii ni Wizara ya Maji si wizara ya ukame, tutafanya kila linalowezekana kuhakikisha Watanzania waishio mijini na vijijini wanapata huduma ya maji safi na salama.

Mheshimiwa Spika, ukimuona kobe juu ya mti amepandishwa, mara kwa mara nasema. Niishukuru Kamati yako kwa maoni, ushauri, maelekezo na maagizo mbalimbali. Leo tunaona faida yake jamii ipo tu, ukiishirikisha utafanikiwa, usipoishirikisha utakwama. Sisi kama Wizara ya Maji hatutakuwa kikwazo kwa kamati yetu, sisi Wizara ya Maji hatutakuwa kikwazo kwa Waheshimiwa Wabunge na wananchi wote katika kuhakikisha tunatekeleza miradi yetu ya maji na iwe na matokeo chanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja yangu leo imechangiwa na jumla ya Waheshimiwa Wabunge 75, lakini Wabunge watatu akiwemo Mheshimiwa Mtaturu wamechangia kwa maandishi. Kwa muda mfupi ambao nimepewa haitakuwa rahisi kujibu kwa kina hoja zote zilizotolewa. Ningependa kuahidi mbele ya Bunge hili tukufu, kwamba hoja zote za Waheshimiwa Wabunge tutazijibu kwa maandishi na kuziwasilisha kuingizwa kwenye kumbukumbu za Bunge. Hivyo ninaomba nitumie muda huu mfupi niliopewa kutoa ufafanuzi wa baadhi ya hoja zilizotolewa kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, moja, hoja ya Kamati za Kudumu za Maji na Mazingira, kukamulisha malipo ya wakandarasi, National Plan, National Water Grid, Non-Revenue water, mapitio ya Sera ya Taifa, Mradi wa Maji wa Tunduma, Mradi wa kukabiliana na mabaliko ya tabianchi Simiyu, vipi kuhusu utekelezaji wa mradi wa maji wa Ziwa Tanganyika, kwa maana ya Kigoma, Rukwa na Katavi, bili za maji na maunganisho ya gharama za maji.

Mheshimiwa Spika, labda nianze juu ya maji katika Jiji letu hili la Dodoma. Kabla Serikali haijahamia Dodoma mahitaji ya maji katika Jiji la Dodoma ilikuwa lita milioni 44, lakini kupitia mamlaka yetu ya maji DUWASA ilikuwa na uwezo wa kuzalisha lita milioni 66. Tulikuwa na maji mengi kuliko mahitaji.

Mheshimiwa Spika, lakini baada ya Serikali kuhamia hapa Dodoma ongezeko kubwa la watu na mahitaji yameendana sambamba. Leo ukienda Dar es salaam maeneo mbalimbali unaona namna ujenzi unavyofanyika. Leo ukenda maeneo ya Singida maeneo ya Nara ujenzi unafanyika. Kwa hiyo baada ya kuongezeka kwa idadi ya watu tumefanya tathmini na tumeona mahitaji katika Jiji la Dodoma ni lita milioni 133 lakini uwezo wa mamlaka yetu kuzalisha ni lita milioni 68. Hapa kuna haja ya kufanya kila linalowezekana ili kuhakikisha Jiji hili la Dodoma linapata maji.

Mheshimiwa Spika, tuna mipango ya muda mfupi lakini tuna mipango ya muda mrefu. Mipango ya muda mfupi tumetumia wataalamu wetu wa rasilimali za maji. Tunatambua maji yaliyo chini ya ardhi ni mita za ujazo bilioni 21, tumewaambia wafanye kila linalowezeka watuoneshe wapi kuna mengi katika Jiji hili la Dodoma, kwa sababu chanzo cha maji tunachokitegemea peke yake ni cha Mzava.

Mheshimiwa Spika, niwapongeze sana wataalam wetu wa rasilimali za maji wamepata maji mengi Nzuguni na tumechimba visima vitano vyenye uwezo wa kuzalisha lita zaidi ya lita milioni saba, tunaziingiza kwenye mfumo ambapo zitaweza kuongeza maji kwa asilimia 11. Maji haya ambayo mradi wake tunauanzisha pale Nzuguni utaweza kuwanufaisha wananchi zaidi ya 75,000. Nini maana yake? Maeneo korofi ambayo yalikuwa na kero kubwa sana ya maji, Nzuguni yenyewe na maeneo ya Ilazo, Kisasa na Swaswa yatapata huduma ya maji safi na salama.

Mheshimiwa Spika, nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge, Mheshimiwa Kunti amezungumza Mheshimiwa Mavunde anazungumzia Jiji la Dodoma, nataka niwambie mradi huu tunakwenda kuukamilisha mwezi wa nane ili kuweza kupunguza adha katika Jiji hili la Dodoma.

Mheshimiwa Spika, zipo jitihada kubwa ambazo tunazozifanya. Tunajua leo mvua badala ya kuwa fursa wakati mwingine imekuwa ikileta maafa. Tumeona mvua inanyeesha inapotea baharini, tunaona mvua inanyesha nyingine inapotelea kwenye mito lakini wananchi hawana maji. Mwelekeo wa Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ni juu ya uvunaji wa maji, kwamba maji badala ya kuwa maafa sasa yawe fursa. Tumejielekeza juu ya ujenzi wa mabwawa, na huo ndio mwelekeo wa Kamati yetu. Kwamba kuwa na ujenzi wa mabwawa madogo makubwa na ya kimkakati ili kuhakikisha kwamba meneo haya kame ambayo hata ukichimba kisima hupati maji tunakwenda kuchimba mabwawa. Nataka niwahakikishie, Mheshimiwa Mbunge wa Kiteto, Mbunge wa Meatu na Mbunge wa Ngorongoro, kwamba tunakwenda kuchimba mabwawa. Mheshimiwa Rais ameshatupatia mitambo kwa ajili ya kuchimbia mabwawa.

Mheshimiwa Spika, yapo mabwawa ambayo yalikuwa yakisomeka tu kwenye documents, Bwawa la Kidunda na Bwawa la Farkwa; lakini dhamira njema na uthubutu wa Rais wetu, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan leo tunakwenda kuyatekeleza mabwawa haya, haijawahi kutokea Waheshimiwa Wabunge. Mlikuwa mkizungumza kwenye Bunge hili mnashauri kila mara mbona utekelezaji hautokei?

Mheshimiwa Spika, leo miradi mingi ambayo tulikuwa tukiitekeleza midogomidogo leo pale Dar es salaam tume- experience water crisis; baada ya pale tulijenga mradi wa bilioni zaidi ya 23 kwa fedha za ndani, ametoa Rais na mradi tumekamilisha. Amesema adha ile hataki aione tena. Mradi wa zaidi ya bilioni mia tatu naa ambao tulikuwa tukisubiri wafadhiri Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan anasema tunaenda kuutekeleza kwa fedha za ndani. Amekwishatoa bilioni 49 na mkadaarasi yupo site, Mungu atupe nini ndugu zangu?

Mheshimiwa Spika, Bwawa la Farkwa ambalo tulikuwa tukilizungumza kila kukicha; leo nataka niwaambie tumezungumza na wenzangu hapa katika commitment ambazo tunazozifanya, kwamba kabla ya tarehe 30 mhandisi mshauri apatikatene kazi ya kuanza hilo bwawa ianze na mkandarasi apatikane ili mradi huu wa Bwawa la Farkwa uweze kutekelezwa kwa sababu fedha tumekwishapata na Mheshimiwa Rais ametupa, hatuna kisingizio.

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge, dhamira njema Rais wetu ya kumtua mwana mama ndoo kichwani hapa Dodoma inatamia.

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge wamezungumza, Kaka yangu Moni amezungumza, na Mheshimiwa Kunti, kwamba mradi huu wa Bwawa la Farkwa maji yanaelekezwa Dodoma vipi kuhusu Chemba? Nataka niwaambie, ukikaa na waridi lazima unukie. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lengo la bwawa hili, pamoja na kuyapeleka maji Dodoma lakini wanufaika wa kwanza watakuwa Wana-Chemba. Mpango wetu ni kuhakikisha hadi Bahi tunayapeleka maji ili wananchi wa Bahi wapate maji. Pamoja na hilo Mheshimiwa Rais anatuelekeza kwamba tuna rasilimali toshelevu hivyo lazima tutumie Ziwa Victoria kuhakikisha kwamba tunaleta maji hapa ambapo pia atawasaidia wananchi wa Singida. Itoshe kusema kwamba Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan ni suluhu ya matatizo ya Watanzania. Tumpigie makofi mengi sana Rais wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, limezungumzwa hapa suala la pamoja na haya mageuzi ambayo tunayafanya, na mimi kuna baadhi ya mambo lazima nikubali. Yapo maeneo ambayo tunafanya vizuri lakini pia yapo maeneo ambayo hatufanyi vizuri. Msema kweli ni mpenzi wa Mwenyezi Mungu.

Mheshimiwa Spika, tunasema kwamba vijijini tuna asilimia 77 lakini ukweli kuna baadhi ya maeneo ukienda, hata mimi Waziri wa Maji wakati mwingine napata unyonge. Ukienda Kilindi hali siyo nzuri, ukienda Ushetu kwa kaka yangu Chereheni hali siyo nzuri, ukienda Meatu hali siyo nzuri. Lakini nataka niwaambie, kwa muda mfupi ambao tumefanya, mpaka sasa tuna vijiji Tanzania takribani 12,318. Pamoja na jitihada zilifanywa na fedha zilizotolewa tumeweza kufikia vijiji zaidi ya 9,000 kwa muda mfupi. Sasa hivi tuna deni la vijiji zaidi ya 3,000.

Mheshimiwa Spika, nini maana yetu? Tunatambua tuna rasilimali za maji juu ardhi mita za ujazo bilioni 105 na pia tuna maji chini ya ardhi mita za ujazo bilioni 21. Nataka niwaambie Waheshimiwa Wabunge, sehemu ambapo tukichimba kisima tutapata maji tunakwenda kuchimba kisima kwa sababu magari tunayo. sehemu ambapo tunaona kabisa ukichimba kisima haupati maji tunakwenda kuchimba mabwawa kwa sababu vifaa tumekwishapewa. Nataka niwatie moyo Waheshimiwa Wabunge, ukiona giza nene ujue kumekucha, baada ya dhiki siyo dhiki bali baada ya dhiki ni faraja na faraja yetu ni Mheshimiwa Rais Samia Suluhu hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hii kazi tunaiweza, tunaiweza sana na tutafanya kila linalowezekana kuhakikisha adhma ya Mheshimiwa Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan ya kumtua mwana mama ndoo kichwani inatimia. Kwa hiyo Mheshimiwa wa Ushetu umezungumza hili suala, tumetuma wataalamu wanafanya tathmini. Acha wamalize kazi, tutahakikisha hatuwezi kufikisha maji maeneo mengine ilhali Ushetu wasipate maji. Tutaweka historia katika Jimbo la Ushetu.

Mheshimiwa Spika, amezungumza dada yangu hapa, Mheshimiwa Rehema wa Bulyanhulu na mama yangu Mama Sitta kuhusu Urambo, Kaliua na Sikonge. Ni kweli maeneo haya yana changamoto, na ndiyo maana nasema yapo baadhi ya maeneo hatukufanya vizuri. Sisi Waheshimiwa Wabunge tulikuwa na mradi hapa unaitwa miji 28. Mradi huu ni wa muda mrefu, ulikuwa ukizungumzwa tu Bungeni. Mheshimiwa Rais alipoingia muda mfupi ameweza ku-unlock mradi ule na tumeweza kusaini na makandarasi.

Mheshimiwa Spika, tukawa na changamoto ya msamaha wa kodi; na hapa nitumie dhati ya moyo nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha pamoja na Naibu Waziri wa Fedha, Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha pamoja na Naibu Makatibu Wakuu wote na kamishna wa bajeti; wametutendea haki sisi Wizara ya Maji. Nataka niwaambie Mheshimiwa Rehema, Mheshimiwa Kakunda na Mheshimiwa Mama Sitta unyonge basi. (Makaofi)

Mheshimiwa Spika, msamahawa kodi kwa wakandasi wale ambao ni kwa ajili ya miji 28 umetoka na advance payment imekwishatolewa, kwa hiyo, hawana kisingizio, kazi yao ni kwenda kutekeleza mradi kwa sababu mradi ule fedha zake zote zipo. Na ninataka niweke commitment, nipo tayari kufanya ziara rasmi ili tukafanye mikutano Kaliua, Sikonge na Urambo ili kwenda kuwakabidhi wakandarasi kwa sababu advance payment wamekwishapewa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka niwaambie Waheshimiwa Wabunge, tumezungumzia fedha zilizotolewa, na hata angalieni bajeti yetu ilivyonono kitabu kizima. Fedha hizi zinahitaji usimamizi na ufuatiliaji. Ndiyo maana nilizungumza kwamba ukiona hapa tunasema mradi umefanya vizuri ni kwa sababu umesimamiwa vizuri. Hii kazi peke yangu Waheshimiwa Wabunge sitaiweza, lazima tukubali kushirikiana. Ndiyo maana nilizungumza, ukisoma Ezra inasema; “Inuka hii shughuli inakuhusu na ukaitende kwa moyo mkuu.” Sisi wasaidizi wa Mheshimiwa Rais tupo pamoja na ninyi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, miradi yetu hii tukienda kuisimamia vizuri matokeo yataonekana, na matokeo yakionekana nini maana yake, ukisoma Isaya 12:3 inasema; “Kwa shangwe mtachota maji katika visima vya wokovu.” Kwa hiyo niwaombe sana Waheshimiwa Wabunge twende tukasimamie hili jambo ili liende vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, imezungumzwa kwamba tuna rasilimali toshelevu, kwa mfano maeneo ya Kigoma, Katavi na Rukwa. Mimi mwenyewe nimefika, nilipangiwa ziara na watendaji wangu, nilighairisha, nikasema hebu tusikie mawazo ya Waheshimiwa Wabunge. Kwa kweli nimeamini, wakati mwingine tutoe nafasi kwa Waheshimiwa Wabunge, ninyi ni consultancy wa ukweli, mnatoa mawazo kwa maslahi ya Watanzania na kwa ajili ya kumsaidia Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Spika, nitawapa mfano mmoja; study za Wizara ya Maji zilikuwa zinasema maji Liwale hakuna, zinasema hivyo; mimi nikasema haiwezekani, tukaja kwa Mheshimiwa Mbunge. Kweli, study zinasema, lakini hebu ngoja twende. Tukaenda tena, leo tumechimba visima maji ni bwerere. Nataka nikuhakikishie Mheshimiwa Liwale, tutaweka historia ambayo ilikuwa imekata tamaa kwa muda mrefu. Hii ni kazi kubwa na nzuri ya Rais wetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan.

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge wa Kigoma Katavi na Rukwa wamezungumzia suala la Ziwa Tanganyika, na mimi mwenyewe nimekwenda kujiridhisha na Katibu Mkuu amekwenda kujiridhisha. Nimefika mpaka kwenye chanzo pale Kalema. Nikiri na kusema kwa dhati kabisa dada yangu Aida umezungumza na Waheshimiwa Wabunge wote mmezungumza, kwamba Ziwa Tanganyika ndilo suluhu ya changamoto ya maji katika mikoa ile. Niwaombe sana Waheshimiwa Wabunge twendeni tukaweke historia ya pamoja. Leo hapa ninavyozungumza naisikia sauti ya Rais wangu juu ya moja ya maelekezo ambayo ametupatia akiwemo na kiongozi wetu katika Bunge, Mheshimiwa Waziri Mkuu, ni kwamba, mawaziri chukueni hatua; tunakwenda kuchukua hatua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hatua tunayokwenda kuchukua ni kumwajiri mhandisi mshauri ili aweze kwenda kufanya usanifu juu ya ujenzi wa mradi huu. Suala la fedha tutakaa na Mheshimiwa Rais, kama maeneo mengine tulivyotekeleza Mheshimiwa Rais wetu atakwenda kutekeleza mradi huu na wananchi hawa waweze kupata huduma ya maji safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, imezungumzwa hapa, pamoja na mageuzi haya tunayoyafanya lakini sasa hivi tunakwenda kwenye mabadiliko ya tabia ya nchi, vipi kuhusu Sera ya Maji? Sera ya maji imeanzishwa 2002 leo 2023.

Mheshimiwa Spika, ni kweli Sera yetu imepitwa na wakati, na ndiyo maana hata katika vipaumbele ya Wizara tumesema lazima twende tukafanye mapitio ya Sera yetu. Kamati pia imelizungumzia hilo.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Kihenzile amezungumza, nadhani hili wala halihitaji mjadala. Maelekezo ya Mheshimiwa Spika wa Bunge pamoja na Bunge lako ni kuhakikisha kwamba twende tukaipitie hii Sera ili ije kuendana na mazingira ya sasa na kasi ambayo anaifanya Mheshimiwa Rais wetu ili kuhakikisha kwamba tunafanya mageuzi na kuleta matumaini makubwa kwa Watanzania.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ni kuhusu suala la gridi ya maji ya taifa. Mwenyezi Mungu ameijalia nchi yetu. Ukienda Kanda ya Ziwa kuna Ziwa Victoria, ukienda mkoa wa Ruvuma kuna mto Ruvuma, ukienda Kigoma, Rukwa na Katavi kuna Ziwa Tanganyika. Pia ukienda Mbeya kuna Mto Kiwila, ukienda kila eneo; leo ukienda zako Mtwara, ukienda kusini kuna Mto Rufiji.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais ametupa maelekezo, kwamba twende tukahakikishe; hii i ndiyo ajenda yake, na Waheshimiwa Wabunge hii kazi tumeshaianza. Leo hii ukienda zako Ziwa Victoria tunayachukua maji ya Ziwa Victoria tunakwenda kupeleka maji katika Jimbo la Rorya, tunayapeleka Tarime Mjini hadi Tarime Vijijini.

Mheshimiwa Spika, ukienda pale Musoma upo mradi wa bilioni 134, mradi mkubwa, tumejenga hadi tenki kubwa la Bahima. Ukienda Mgango Kiabakali na Butiama tuna mradi wa zaidi ya bilioni 70 kwa ajili ya kutumia Ziwa Victoria. Ukienda Mwanza, leo tumeona mahitaji katika Jiji la Mwanza ni lita milioni 154, mamlaka yetu ya maji ina uwezo wa kuzalisha lita milioni 90.

Mheshimiwa Spika, tuna mradi wa bilioni 69 wa Butimba sikulisaidia tu Jiji la Mwanza, maji yale yanakwenda mpaka Magu na yanakwenda mpaka Jimbo la Misungwi.

Mheshimiwa Spika, achana na hilo, leo hii tunazungumza mradi ambao tulikwishautekeleza ya kuyatoa maji kuyaleta Shinyanga, tumeyapeleka Tabora, tumeyapeleka Igunga, tumeyapeleka Nzega. Mheshimiwa Rais anatueleza kwamba sasa hivi tanayapeleka Igalula, lakini tunayapeleka Kaliua, tunayapeleka Sikonge na tunayapeleka mpaka Urambo kwa Mama Sitta, tumpigie makofi mengi sana Rais wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, achana na hilo, leo imekuja hoja hapa ya Ziwa Tanganyika, hii ndio Gridi ya Taifa ambayo tunatakiwa kwenda kuifanya, tunakwenda kuweka historia hii. Nilizungumza hata Baba wa Taifa alivyokuwa anakwenda kupigana vita vya Idd Amini, alisema maneno machache tu kwamba, uwezo tunao, nia tunayo na sababu pia tunayo. Sababu ya kwenda kujenga mradi huu wa Ziwa Tanganyika kwa maeneo haya tunayo na Mheshimiwa Rais kazi hii alishaianza. Ukienda Kigoma Jimbo ambalo lina kata 19, amejenga mradi wa bilioni 42, zaidi ya kata 19 zimepata maji. Mradi ule tumeshaufanyia extension, tumepeleka mpaka Mwandiga, nini sasa kilichobaki? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mradi ule uongezewe kufanyiwa extension na huyu Mhandisi Mshauri aliyepatikana maeneo ya Rukwa na Katavi waende kupata huduma ya maji safi na salama. Leo tunakwenda kutumia Mradi wa Maji wa Mto Ruvuma, target yetu katika miji hii 28 tunaendea kuanza. Mkandarasi yuko site, tunayatoa maji ya Mto Ruvuma tunayapeleka katika Jimbo la Nanyumbu ambalo lilikuwa na shida kubwa sana ya maji, lakini maji yanayofika Nanyumbu tutayashusha mpaka Masasi ili kuhakikisha Jimbo la Masasi wanapata huduma ya maji safi na salama.

Mheshimiwa Spika, ukienda kwa Mheshimiwa Mkuchika, tuna mradi mkubwa wa Makonde. Mradi una umri mkubwa umekuwa chakavu kuliko mimi Waziri wa Maji, leo Rais ameshatupatia bilioni 84. Tunayatoa maji pale kwa Mheshimiwa Mkuchika Newala tunayapeleka Tandahimba kwa Mheshimiwa Katani, yanafika mpaka kwa Mheshimiwa Chikota. Huo ndio uelekeo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mradi ambao ulikuwa umekwama wa Same - Mwanga, ambao mradi wenye uwezo mkubwa wa uzalishaji mkubwa si kuwasaidia Wanamwanga na Same, mradi ule unafika hadi Tanga. Achana na hilo, tuna mradi wa zaidi ya bilioni 170, ambapo tunakwenda kuyachukua maji ya Mto Pangani. Mkandarasi yupo site maji yale yanaenda Korogwe, Muhenza mpaka Kilindi huko, lakini mpaka katika Jimbo la Pangani. Kwa hiyo, huo ndio uelekeo.

Mheshimiwa Spika, hata ukienda zako Mbeya, ulizungumza katika Bunge lililopita, pale tuna Mto Kiwira tukichukua Mto Kiwira, nitapeleka katika Jiji la Mbeya lakini katika maeneo mengine. Umeona kazi tuliyoifanya, safari moja huanzisha nyingine, safari tumeianza acha tuiendeleze.

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge wasisahau miradi hii mikubwa inahitaji fedha nyingi, lakini Rais wetu ameonyesha uthubutu. Nilivyokuwa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kulikuwa somo likuwa linaitwa haya mambo ya civics, civics, development studies. Tuliambiwa development is the progressive change from low level to higher level. Maendeleo ni mchakato na Rais wetu amekwishayaanza na maendeleo yanaonekana na namna Wabunge wanavyompongeza. Kikubwa tumpe ushirikiano, yale mambo ambayo tulikuwa tunaamini hayawezi kufanyika, leo yanafanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo Maendeleo katika Sekta ya Maji na Tanzania yanaanza na mimi. Maendeleo ya Taifa letu yanaanza na wewe, maendeleo ya Taifa letu yanaanza na sisi sote kwa kushikamana.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine lilizungumzwa na Mheshimiwa Shonza, Mheshimiwa Hasunga na Mheshimiwa Stella juu ya utekelezaji wa mradi katika Jimbo la Tunduma la kuyaleta maji Vwawa, Mloo. Tumeshakubaliana kabla ya Mwezi wa Saba mkandarasi atakuwa amepatikana, tunakwenda kuanza utekelezaji wa mradi wa maji katika kuhakikisha tunapeleka maji katika Eneo la Tunduma.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ambalo tumelizungumza, hatuwezi tukawa na Wizara ambayo haina National Water Master Plan, haya ni maoni ya Kamati, haya ni maoni ya Waheshimiwa Wabunge, lakini pia sisi katika vipaumbele vyetu vya Wizara tumeliona hili. Tunalipokea acha twende tukalifanyie kazi juu ya utekelezaji wake.

Mheshimiwa Spika, Mradi wa Simiyu, huu ni mradi mmoja wa miradi ambayo utekelezaji wake ulikua mgumu. Tulikuwa na miradi mitatu, Mradi wa Same - Mwanga, Mradi wa Miji 28 pamoja na Mradi huu wa Simiyu. Tuliwaita wafadhili KfW, tulikaa nao ofisini. Huu ni mradi wa muda mrefu sana na Serikali pale imeahidi, tutapoteza imani ya Serikali yetu, tunaomba twende juu ya utekelezaji. Waheshimiwa Wabunge wali mtamu sana kwa maini, lakini ukikaa sana unakuwa kiporo na kiporo kikaa sana kina chacha na mwisho wake kinaumiza tumbo. Wafadhili wale wametuelewa… (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Waziri dakika mbili, malizia.

WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, wafadhili wale wametuelewa na nataka niwaambie Wabunge wa Mkoa wa Simiyu, naomba wa-note tarehe hii hapa, kwamba tarehe hii 30 Mei tunakwenda kusaini mradi ule ili kuhakikisha Wanasimiyu kwa maana ya Bariadi, Itilima wanaenda kupata huduma ya maji safi na salama.

Mheshimiwa Spika, kwa namna ya kipekee niendelee kukushukuru na niendelee kumshukuru Mheshimiwa Rais pamoja na Bunge lako tukufu pamoja na Kamati yote na Watendaji wote wa Wizara ya Maji, Wenyeviti wa Kamati bila kusahau familia yangu. Ninachotaka kusema sisi tutafanya kazi usiku na mchana kuhakikisha Watanzania wanapata huduma ya maji safi na salama.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naafiki.