Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji

Hon. Anthony Peter Mavunde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Dodoma mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji

NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi. Kipekee kabisa nichukue fursa hii kumshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa uwekezaji mkubwa alioufanya kwenye sekta hii ya maji, ambao unakwenda kuleta mapinduzi makubwa.

Mheshimiwa Spika, kipekee kabisa nichukue fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na watendaji wote katika Wizara ya Maji kwa kazi kubwa ambayo wanaifanya katika kuhakikisha kwamba wanatatua changamoto za maji kwa Watanzania.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri Juma Aweso ni kijana ambaye pia anatoa somo kwa vijana wengine wanaopewa dhamana namna ya kutekeleza majukumu yao. Anajitahidi sana kufanya kazi vizuri na tunamwombea kila la kheri kwa Mwenyezi Mungu akamilishe kazi hii kubwa ambayo anaendelea kuifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sisi Wizara ya Kilimo tunafanya kazi kwa ukaribu sana na Wizara ya Maji. Tumeshuhudia hivi karibuni mapinduzi makubwa kabisa kwenye sekta hii ya maji juu ya uingizaji wa mitambo zaidi ya 25 ambayo itasaidia katika uchimbaji wa visima na mabwawa. Mabwawa haya yatakwenda kuongeza vyanzo vya maji ambayo yatatumika pia kwa ajili ya matumizi ya binadamu, na katika maeneo mengine pia wanufaika watakuwa wakulima wadogo wadogo katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, kazi inayofanywa na Wizara ya Maji inakwenda sambamba na ile inayofanywa na Wizara ya Kilimo ya uchimbaji wa mabwawa 100 katika bajeti kama tulivyoyasema ambayo yatagusa maeneo mbalimbali katika nchi yetu ya Tanzania. Hii inatupa uhakika katika ku-address changamoto za mabadiliko ya tabianchi ambapo moja kati ya jambo kubwa ambalo limekuwa na athari kubwa ni la ukame. Sasa tutapata nafasi ya kuweza kuyavuna maji na pia kuyatumia kwa ajili ya shughuli mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, tunaingia katika historia katika kipindi hiki cha bajeti hizi mbili; ya kilimo na ya maji, zikitekelezwa ipasavyo, maana yake tutakuwa na uhakika wa vyanzo vingi sana vya maji kupitia mabwawa haya na visima ambavyo vitachimbwa.

Mheshimiwa Spika, sisi Wizara ya Kilimo pamoja na TAMISEMI, Wizara ya Maliasili na Wizara ya Mifugo, mbele ya Mheshimiwa Makamu wa Rais tuliweka makubaliano ya kuhakikisha kwamba tunatunza vyanzo vya maji ili tuwe tuna uhakika wa vyanzo vyetu vya maji na kuhifadhi mazingira katika vyanzo vya maji.

Mheshimiwa Spika, katika miradi ambayo tutaitekeleza katika Wizara ya Kilimo hivi sasa, tutahakikisha mifereji tutakayoijenga katika miradi yote ya umwagiliaji, ambayo itakuwa inatumia vyanzo vya maji ya mito na maziwa, tutahakikisha kwamba, maji yale yakishatumika kwenye kilimo yawe na uwezo wa kurudi katika mito na yatumike katika shughuli nyingine. Hivyo, sisi pamoja na wenzetu wa Wizara ya Maji katika eneo hilo, tutahakikisha kwamba mifereji ambayo tutaijenga safari hii kwenye miradi mikubwa hii ambayo inaendelea, itakuwa ni ile ambayo haitakuwa na upotevu mkubwa wa maji tofauti na ilivyo hivi sasa.

Mheshimiwa Spika, mifereji mingi ya hivi sasa inapoteza maji zaidi ya asilimia 40 kwa sababu ya kukosa ile miundombinu rafiki ya kuweza kurudisha maji katika chanzo chake cha awali. Kwa hiyo, sisi kwa pamoja tutaifanya kazi hiyo. Sambamba na hilo, tutahakikisha tunatumia mabomba katika baadhi ya maeneo ili maji yatumike katika ufasaha wake mzuri pasipo kuleta changamoto yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja kubwa hapa ni kuzuia upotevu mkubwa wa maji, na bahati nzuri sana tunao wakulima wetu ambao wanafanya kilimo pembezoni mwa vyanzo vya maji, tumeshakaa pamoja na Wizara kwa ajili ya kutoa elimu juu ya matumizi sahihi ya maji lakini na kilimo cha kisasa ambacho hakitaharibu mazingira. Hiyo ndiyo kazi kubwa ambayo tutaifanya kwa pamoja na wenzetu wa Wizara ya Maji.

Mheshimiwa Spika, katika mikakati ambayo ukiiangalia katika Wizara ya Maji wamezungumza jambo zuri sana la namna pia ya kuondoa changamoto kubwa ya huduma ya usafi wa mazingira katika maeneo mengi. Kwa sababu mimi pia nipo katika eneo hili, nataka nitoe ushuhuda wa kazi nzuri inayofanywa na Wizara ya Maji katika eneo letu la hapa hapa Dodoma ambapo tumeshuhudia juzi tu Mheshimiwa Waziri Aweso amesimamia uingiaji wa mikataba mkubwa kabisa wa zaidi ya Shilingi bilioni 164 ambayo inakwenda kutatua changamoto kubwa ya usafi wa mazingira katika jiji la Dodoma na hasa katika kuhakikisha kwamba sehemu zenye changamoto ya huduma ya majitaka, hivi sasa zinakwenda kuwekewa mfumo mzuri ili kutatua changamoto hii.

Mheshimiwa Spika, katika eneo hili, umefanya katika maeneo mengi nchi nzima, lakini nataka nitoe ushuhuda kwamba, katika eneo hili la Dodoma, ambapo pia Wabunge wengi sana mnaishi na mmesema katika sehemu ya hoja zenu, kwamba Serikali inakwenda kuweka mradi mkubwa ambao utagusa kata 14 na bomba refu la kilometa 117 kwa ajili ya kuondoa majitaka katika maeneo mbalimbali ambayo imekuwa ni changamoto kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika hoja ambazo zimesemwa hapa ambazo nataka nizitolee ushuhuda kuonesha kazi nzuri inayofanywa na Mheshimiwa Waziri na timu yake nzima ni suala la maji katika eneo letu la hapa Dodoma Jiji, na nikiwa kama sehemu ya Serikali na vile vile kama kiongozi katika eneo hili, nataka nipongeze kazi nzuri ambayo Mheshimiwa Waziri ameifanya, juu ya changamoto mbalimbali ya maji kwa kutumia mfumo wa uchimbaji wa visima. Tumeona katika maeneo mengi hivi sasa huduma ya maji imeanza kupatikana hasa baada ya Mheshimiwa Waziri kuweka nguvu kubwa ya uchimbaji wa visima vya pembezoni. Tumeshuhudia mradi mkubwa wa Nzuguni ambao unakwenda kutatua changamoto kubwa katika maeneo ya Ilazo, Swaswa, Mlimwa C, pamoja na Kisasa. Vile vile na uchimbaji wa visima vingine virefu katika maeneo ya Makulu, Nala, Zuzu, Iyumbu na Chang’ombe. Haya maeneo yote yanakwenda kutatua changamoto kwa kiwango kikubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hii ilikuwa ni kutoa tu ushuhuda wa kazi kubwa na nzuri ambayo anaifanya Mheshimiwa Waziri katika eneo letu la hapa Dodoma, lakini kikubwa na katika kumalizia hoja yangu, nataka tu nimhakikishie kwamba sisi Wizara ya Maji pamoja na Wizara ya Kilimo tutafanya kazi kwa pamoja kuhakikisha tunatatua changamoto za msingi na hasa katika kilimo ambacho hakitaharibu mazingira ili kwa pamoja basi, wakulima wanufaike na vyanzo vya maji, lakini na vile vile tuweze kuyatunza maji kwa ajili ya mazingira.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. Nakushukuru sana kwa nafasi. (Makofi)