Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nimpongeze sana Waziri Jumaa Aweso na Naibu wake Engineer Maryprisca Mahundi, Katibu Mkuu Engineer Kemikimba pamoja na wataalam wa Wizara ya Maji kwa kazi nzuri wanayofanya.

Mheshimiwa Spika, Waziri na timu yake wamekuwa mfano wa kuigwa kwenye kutatua changamoto za maji na kuwatua akinamama ndoo kichwani, kwani maji ni haki ya msingi kwa binadamu wote.

Mheshimiwa Spika, kwa ujumla inatia faraja kuona upatikanaji wa maji vijijini unaongezeka kama alivyoonesha kwa kina katika hotuba yake ya bajeti ya mwaka huu wa 2023/2024.

Mheshimiwa Spika, katika jimbo langu la Moshi Vijijini kuna changamoto ya upatikanaji wa maji ya bomba katika maeneo yafuatayo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza, Kata ya Mabogini ina wakazi wengi wapatao 57,231 na kuna changamoto kubwa ya maji ya kunywa. Katika Kata ya Mabogini kuna changamoto ya maji katika vijiji vya Mabogini, Muungano, Chekereni, Maendeleo, Mtakuja na Mserekia. Ninaomba Wizara ipeleke maji katika vitongojj ambavyo havijapata maji katika vijiji vilivyotajwa.

Mheshimiwa Spika, pili, Kata ya Kimochi ina zaidi ya wakazi 16,046. Kata hii ina vijiji vya Mowo, Sango, Shia, Miami, Lyakombila na Kisaseni. Eneo lote linahudumiwa na MUWSA.

Tunaishukuru Serikali kwa jitihada za awali kuwafikishia wakazi wa eneo hili maji, ila bado kuna changamoto kubwa sana ya upatikanaji maji katika maeneo mengi hasa Kijiji cha Sango, Shia na Kisaseni. Ninaiomba Serikali itutengee pesa za kutosha ili maji yafike maeneo yote ya kata hii vikiwepo vijiji vya maeneo ya tambarare.

Mheshimiwa Spika, katika Kata ya Uru Kusini yenye vijiji saba vya Okaseni, Kimanganuni, Rua, Kariwa, Longuo A, Kitandu na Shinga ina takribani wakazi 31,557 na ina miradi mitatu ya Mang'ana, Kisimeni na Mbora. Changamoto ya miradi hii ni maji kidogo katika mifumo ambayo hayatoshelezi. Naiomba Serikali isaidie, kwani mbali na hivyo vijiji kuna taasisi ya Chuo Kikuu cha Kikatoliki Mwenge. Kuna shida kubwa sana ya maji hapo chuoni. Ninaiomba Wizara iangalie namna ya kusaidia.

Mheshimiwa Spika, nne, Kata ya Arusha Chini yenye wakazi 13,977 kuna shida ya maji katika Vijiji vya Mikocheni na Chemchem. Sasa hivi ni watu wa Kirua Kahe wanatoa huduma ya maji ya kuuza katika maeneo haya. Maji huuzwa kwa bei ya juu na si salama kwa matumizi ya binadamu. Kata hii inahudumiwa na RUWASA. Ninaiomba Wizara ijenge mradi kwa kutumia maji ya kutoka Mto Ronga na Kikuletwa.

Mheshimiwa Spika, tano, katika Kata ya Uru Kaskazini yenye wakazi 10,817 MUWSA haijatekeleza ahadi ya kuunganisha vijiji vya Msuni na Njari. Kuna chanzo cha maji Uru Kaskazini ambacho hupeleka maji Kata ya Uru Kusini na Kata ya Pasua ya Manispaa ya Moshi Mjini. Wananchi wananyanyasika sana kwani maji ya eneo lao hayawasaidii. Ninaiomba Wizara iunganishe Vijiji vya Msuni na Njari ili wananchi wapate maji.

Mheshimiwa Spika, katika Kata ya Old Moshi Magharibi, kuna wakazi 8,431 na kuna mradi wa maji wa Tela Mande ambao umekamilika. Mradi huu una maji mengi sana na ya ziada ambayo kwa sasa yanahudumia wananchi wa ukanda wa milimani.

Mheshimiwa Spika, vijiji na vitongoji vya kata hii vilivyopo ukanda wa tambarare kama kile cha Mandaka Mnono na Saningo havina maji ya bomba. Ninaiomba Wizara iwapelekee maji wananchi hawa walioko ukanda wa tambarare.

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo yangu hapo juu, naunga mkono hoja.