Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, napenda kuwashukuru na kuwapongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Dkt. Philip Isdor Mpango, Makamu wa Rais wa wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mawaziri na viongozi wote wa Wizara ya Maji, kwa uongozi wao na utendaji uliotukuka.

Mheshimiwa Spika, napenda pia kutumia fursa hii kukupongeza wewe binafsi, Naibu Spika na uongozi wote wa Bunge kwa uongozi wenu mahiri na wenye ubunifu wa hali ya juu katika kuongoza mhimili wa Bunge.

Mheshimiwa Spika, napenda kumpongeza Waziri wa Maji, kwa hotuba nzuri iliyojaa ubunifu mkubwa na imedhihirisha utayari wa Serikali katika utekelezaji wa ustawi wa jamii na maendelo endelevu, na hii ni mojawapo ya nguzo kuu katika utayari wetu wa ushindani wa kimataifa (national competitiveness). Bajeti hii inaenda sambamba na Dhima ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2021/2022 – 2025/2026 ambayo ni Kujenga Uchumi Shindani na Viwanda kwa Maendeleo ya Watu.

Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha miezi kumi ya bajeti ya 2022/2023, Serikali kupitia Wizara ya Maji imetekeleza miradi mingi ya maji. Katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya inatekeleza kwa ufanisi mkubwa miradi ya vijiji vya Simambwe, Usoha Njiapanda, tembela, Iyawaya, Izyira, Ruanda, Ilembo, Inyala, Igoma, Iwalanje, Galijembe, Tembela, Pashungu, Shigamba, Santilya, Inyala Ilembo, Mshewe, Muvwa, Njelenje, Mapogoro, Mjele, Chang’ombe, Ipwizi, Ikukwa, Simboya, Itimba, Utengule, Ihombe, Idugumbi, Iwala, Ilota, Ikhoho na pia mradi mkubwa katika Mji wa Mbalizi. Miradi yote hiyo imetekelezwa kwa ufanisi mkubwa, ingawa kunahitajika uboreshaji wa miundombinu ya mabomba hasa katika mradi wa Mbalizi kuna upotevu mkubwa wa maji kutokana na uchakavu wa mabomba yaliyokuwepo awali.

Mheshimiwa Spika, pamoja na mafanikio hayo makubwa, katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya bado kuna changamoto kubwa ya maji salama kwa wananchi katika maeneo mengi ya vijijini. Pamoja na kuwepo kwa vyanzo vingi vya mseleleko (gravity), asilimia kubwa ya vijiji havina maji salama. Nashukuru kwa kuwepo bajeti ya mradi mkubwa wa Mto Kiwira ambao utakuwa mkombozi wa maeneo mengi ya Mkoa wa Mbeya na hata Mkoa wa Songwe. Napendekeza Serikali iendelee kutekeleza miradi ya maji ikiwa ni pamoja na kuweka mkakati wa kuhakikisha upatikanaji wa maji unakuwa endelevu na mafanikio ya kupunguza gharama za miradi na pia utekezaji uwe wa haki na haraka na kwa ufanisi mkubwa.

Mheshimiwa Spika, napendekeza Serikali iweke msukumo mkubwa wa kuharakisha utekelezaji wa miradi iliyomo kwenye Mradi wa Bonde la Mto Songwe (Songwe River Basin Development Programme - SRBDP), wenye ofisi zake Kyela, Tanzania. Mradi huu unaotekelezwa kwa pamoja na Serikali za Tanzania na Malawi, ni muhimu sana kwa sasa kutokana hasa na ujenzi wa mabwawa ambayo pamoja na manufaa mengine, yatasaidia kupunguza mafuriko ya Bonde la Kyela. Mabwawa haya yamelenga kuzalisha umeme, kilimo cha umwagiliaji, shughuli za uvuvi na hata utalii ambao unahitajika sana katika Wilaya ya Mbeya na ukanda wote wa Nyanda za Juu Kusini.

Mheshimiwa Spika, kutokana na changamoto za tabianchi, kumekuwepo na uharibifu mkubwa wa mazingira na ongezeko la upungufu wa vyanzo vya maji. Uharibifu unaotokana na shughuli za kibinadamu umepelekea misitu mingi kuharibiwa na uchomaji moto, ukataji misitu kwa matumizi ya mkaa, na hata kilimo kwenye vyanzo vya maji.

Mheshimiwa Spika, napendekeza Serikali iongeze msukumo wa Wizara za Maji, Kilimo, Maliasili, na Mazingira kufanya kazi kama timu moja ili kukabiliana na janga hili kubwa ikiwemo ujenzi wa mabwawa makubwa katika maeneo yanayokumbwa na mafuriko. Kama ilivyo kwa athari za mafuriko ya Kyela, hata Ziwa Rukwa linaathirika sana na kujaa mchanga na udongo unaosombwa na mito kutokana na mmomonyoko wa udongo.

Mheshimiwa Spika, kutokana na mahitaji ya maji kwenye kilimo, mifugo na hata mahitaji ya mabwawa kwa ajili ya kuzuia mafuriko ikiwemo kwenye miundombinu yetu ya reli na barabara, kuna haja na kuwepo kwa taasisi moja kuratibu na kusimamia mipango ya matumizi ya maji. Nchi yetu ina neema kubwa ya maji na hii ni fursa ya kipekee kutumia haya maji kama mojawapo ya nguzo kuu kukuza uchumi wetu.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.